Header Ads

KESI YA SHEIKH PONDA ULINZI BALAA



Na Happiness Katabazi
ULINZI unaowekwa wakati wa kesi ya inayomkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Waislamu,Sheikh Ponda Issa Ponda, na wenzake 49,umevunja rekodi.

 Mwandishi wa habari hizi ambaye alifika saa moja asubuhi katika eneo hilo la mahakama alishuhudia askari wa kikosi cha kutuliza ghasia,na wanausalama wengine wakiwa wamevalia nguo za kiraia wakiwa wamebeba silaha nzito yakiwemo mabomu viunoni, na mbwa wa  12 wa jeshi la polisi wakiwa wamezingira ndani ya  nje ya mahakama hiyo kwaajili ya kuimarisha ulinzi kwasababu walikuwa wamepata taarifa kuwa kuna baadhi ya wafuasi wa Ponda walikuwa wamepanga kuja kufanya vurugu mahakamani hapo.

Ponda ambaye aliingia katika eneo hilo akitokea gereza la Segerea huku akiwa amesindikizwa na msafara wa magari ya maji ya kuwasha’ kikojozi’, na magari ya magereza, aliingizwa moja kwa moja hadi mabusu ya mahakama hiyo huku wanausalama waliokuwa wamesimama getini waliweka utaratibu wa kuwazuia wadhamini, ndugu na jamaa wa washtakiwa katika kesi hiyo kuingia ndani ya viwanja vya mahakama hiyo  hali iliyosababisha ndugu na jamaa hao kukaa nje ya jengo la Sophia House, tofauti na hapo awali ambapo wanausalama walilikuwa wakiwaruhusu mamia hayo ya wafuasi wake kuingia ndani mahakama hiyo hali iliyokuwa ikisababisha msongamano mkubwa na karaha katika chumba cha uendesheaji kesi hiyo.

Hata hivyo baadhi ya maofisa usalama waliliambia gazeti hili kwa masharti ya kutotajwa majina yao gazetini kuwa utaratibu huo waliouanzisha jana  wa kuimarisha ulinzi na kuzuia wafuasi wa Ponda na watu wengine ambao hawana shughuli yoyote wanaokuja kuifanya mahakamani hapo wakati kesi hiyo ikiwa inasikilizwa  wala kulikaribia jengo la mahakama hiyo ya Kisutu utakuwa ni endelevu na hawatasita kumchukulia hatua mtu yoyote atakayekaidi amri hiyo na kuongeza kuwa hadi jana polisi iliwakamata watu watatu ambao walikuwa wakilamizisha kuingia ndani ya eneo hilo la mahakama bila ya sababu inayompelekea huko.
Hata hivyo jana ndani ya ukumbi namba moja wa mahakama hiyo ambapo kesi hiyo ya Ponda uwa inasikilizwa hapo, ilikuwa ni tofauti kwani kulikuwa na washtakiwa, wanausalama, waandishi wa habari,mawakili na hakimu tu , hali iliyosababisha makundi hayo kufanya kazi yao kwa nafasi na hewa kupatikana na wananchi mbalimbali wakiwemo waandishi wa habari walivipongeza vyombo vya dola  kwa utaratibu huo mpya kwani wingi wa watu uliokuwa ukifurika wakati wa kesi hiyo pia ulikuwa ukiatarisha usalama na kusisitiza kuwa utaratibu huo uwe endelevu.

Wakili Mwandamizi wa Serikali Tumaini Kweka akiomuongoza shahidi wake wa nane, D/c-Sajenti Mkombozi Mhando  mbele ya Hakimu Mkazi Victoria Nongwa alidai kuwa  Novemba 11 mwaka jana, alikuwa Kituo Kikuu cha Polisi Kati akiwa na timu ya wapelelezi wenzake toka Temeke yeye alipewa jukumu la kumhoji mshitakiwa wa tano, Mukadam abdallah Swaleh ambapo alimpa haki zake zote.

Sajenti Mhando alidai katika ungamo aliloungama mshtakiwa huyo Mukadamu, mshtakiwa huyo alikiri kushiriki kikamilifu yeye na wenzake kuingia kwa jinai kwenye kiwanja cha Chang’ombe Markas ambacho kiwanja hicho kilikuwa mali ya Bakwata na kilishauzwa na kwamba alishiri kujenga msikiti wa muda katika eneo hilo na walikuwa wakisali katika eneo hilo kuanzia Oktoba 12 -17 mwaka jana, siku wenzake waliokuwa wakilala hapo kwa kipindi chote hicho kukamatwa na jeshi la polisi.

Sajenti Mhando alidai kuwa Mkadamu alimweleza kuwa yeye ni mjumbe wa Taasisi ilikuwa ikiongozwa na Ponda na kwamba Aprili mwaka jana, walipata taarifa toka kwa mwanafunzi wa kiislamu kuwa kiwanja hicho kimeuzwa na kwamba wao kama jumuiya waliamua kwenda kuona na Mufti Mkuu wa Tanzania,Sheikh Shaban Bin Simba  kumuuliza kuhusu hilo na Simba aliwajibu kuwa ni kweli Bakwata imeishakiuza kiwanja hicho kwa njia halali kwa kampuni ya Agritanza Ltd.

“Mkadamu katika ungamo lake alieleza kuwa baada ya Mufti kuwaeleza hayo wao kama jumuiya ya kiislamu waliamua kwenda kwa aliyenunua na kumwambia asiendelee na ujenzi wa kiwanja hicho kwani kiwanja hicho ni mali ya waislamu siyo na ilipofika Oktoba 12 mwaka jana,baada ya Swala ya Ijumaa,ndiyo Mkadamu na wenzie walivamia eneo hilo kwa lengo la kulitwaa eneo lao  ambapo waliweka kambi hapo hadi Februli 17 mwaka jana ambapo walijenga na msikiti wa muda na wafuasi wengine walikuwa wakilala katika eneo hilo, ila yeye Mkadamu hakuwa akilala hapo”alidai Mhando na kuomba maelezo hayo ya ungamo liloungamwa na mshitakiwa huyo anaomba yapokelewe kama kielelezo.

Hata hivyo wakili wa washtakiwa Mansoor Nassor alipinga maelezo hayo yasipokelewe kwasababu kifungu cha 50(1)(a) cha Sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 , yataka mtuhumiwa achukuliwe maelezo ndani ya  saa nne tangu alipokamatwa  na hapa maelezo ya onyo ya Mkadamu yanonyesha Mhando alimchukua Novemba Mosi mwaka jana  wakati tayari mshtakiwa huyo alishakuwa amekamatwa siku tano nyuma akiwa mahabusu  na kwamba kifungu cha 50((1)b cha sheria hiyo ya makosa ya Jinai kina mpa haki ofisa wa polisi  kuongeza masaa  ya  kumchukua maelezo mshtakiwa na kwamba shahidi aliyepo mahakamani (Mhando)hakuna sehemu yoyote inaonyesha aliongeza muda wa kumchukua maelezo na kwamba kifungu cha 51(a)  cha sheria hiyo pia ina mpa mamlaka ofisa wa polisi kwenda mahakamani kuomba mahahakama imuongezee muda wa kumhoji mshtakiwa huyo lakini kwa makusudi shahidi huyo alishindwa kufanya hilo.

“Mheshimiwa hakimu pia kwa makusudi shahidi huyu amekiuka matakwa ya kifungu cha 57(2) (a) cha Sheria hiyo  ambacho kina mtaka ofisa wa polisi kuandika maelezo ya mshitakiwa kwa mtindo wa swali na jibu lakini maelezo ya Mkadamu yameandikwa kwa mtindo wa stori tu na siyo kwa mtindo wa swali na jibu…na kwasababu hiyo sisi upande wa utetezi tunapinga maelezo haya yasipokelewe  kwasabababu yamekiuka matakwa ya vifungu hivyo vya sheria”alidai wakili Mansoor.

Kwa upande wake wakili mwandamizi wa serikali Tumaini Kweka, alidai kuwa kutokana na hali hiyo,sheria ipo wazi na inataka mahakama iendeshe uchunguzi na upande wa jamhuri upo tayari kuleta mashahidi wa tatu kuja kuthibitisha kuwa maelezo ya onyo ya Mkadamu yalichukuliwa kwa kufuata taratibu zote za kisheria.Hata hivyo wakili Mansoor alidai hakuna haja ya mahakama kufanya uchunguzi kwani udhahifu wa maelezo hayo uliofanywa na shahidi huo wakati akimchukua maelezo upo wazi hali iliyosababisha hakimu Nongwa kusema anakubaliana na ombi la wakili wa jamhuri lilotaka ufanyike uchunguzi wa tuhuma hizo na kwamba anaiarisha kesi hiyo hadi leo ambapo upande wa jamhuri utaleta jumla ya mashahidi watatu kuja kudhibitisha kuwa kuwa maelezo ya mshtakiwa hayo yalikidhi matakwa ya kisheria na  kisha atatolea uamuzi ama yapokelewe au yasipokelewe.

Baada ya kesi hiyo kuairisha Ponda wakati akitoka ndani ya viwanja vya mahakama hiyo, wafuasi wake wachache ukilinganisha na siku za nyuma walikuwa wamekaa na wengine kusimama katika jengo la Sophia House walimpungia mkono na kusema Takbiri Takbir. Na Ponda aliondoshwa katika viwanja hivyo na kupelekwa gereza la Segerea saa 5:21 asubuhi.

Wakati huo huo; ilipofika saa 6:40 mchana  ,jumla  ya washtakiwa  54 walioandamana isivyohalali  Ijumaa iliyopita Ilala jijini Dar es Salaam,walifikishwa mahakamani hapo mbele ya Hakimu Mkazi Sundi Fimbo wakikabiliwa na makosa ya manne.
Jopo la mawakili waandamizi wa serikali linaloongozwa na Bernad Kongora, Peter Njiku, Nassor Katuga, Zuberi Mkakatu  na Joseph Mahugo walidai mbele ya Hakimu Fimbo kuwa  washtakiwa hao ni Salum Bakari Makame, Said Idd Ally na wenzao 51 ambapo makosa ya  kula njama  kutenda kosa,kufanya mkusanyiko haramu,kufanya maandamano ambayo yalikatazwa na jeshi la polisi na kosa nne ambalo linamkabili mshitakiwa wa kwanza,pili na watatu  ni la kushawishi wananchi kutenda mnakosa hayo Februali 15 mwaka huu, huko wilaya ya Ilala Dar es Salaam,na washitakiwa walikana mashitaka yote na wakili Kongora akadai upelelezi wa kesi umekamilika na wanaomba mahakama iwapatie tarehe ya kuanza kusikilizwa.
Aidha wakili Kongora alidai hata hivyo Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), ametoa kibali chake cha kuzuia dhamana kwa mshtakiwa wa kwanza, pili na watatu chini ya kifungu cha 148(4) cha Sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, na kwamba kwakuwa washitakiwa wanakabiliwa na makosa ya kuvuruga amani ,upande wa jamhuri unaoiomba mahakama ifunge dhamana za washtakiwa wengine 51 wa kesi hiyo hadi hali ya usalama itakapotengamaa. Hakimu Fimbo alisema inapowasilisha hati ya DPP ya kuzuia dhamana kwa washtakiwa mahakama yake inakuwa imefungwa mkono na hivyo haiwezi kuipinga hati hiyo ya DPP na kwamba pia mahakama yake imekubali ombi la wakili wa jamhuri ya kuwafunguia dhamana washtakiwa hao 51 licha mashitaka yanayowakabili yanadhamana kwa mujibu  wa sheria hadi pale hali ya usalama itakapotengamaa na akaiarisha kesi hiyo hadi leo itakapokuja kwaajili ya upande wa jamhuri kuwasomea maelezo ya awali washitakiwa hao na kuamuru washitakiwa waende gerezani.
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Februali 19 mwaka 2013

No comments:

Powered by Blogger.