Header Ads

KESI YA WIZI BARCLAYS

Mfanyabiashara aunganishwa na
Merey Balhabou

Na Happiness Katabazi

HATIMAYE serikali jana ilimuunganisha mfanyabiashara maarufu wa madini, Justice Rugaibura (36), mkazi wa Msasani Beach, jijini Dar es Salaam, katika kesi ya wizi wa dola za Kimarekani milioni 1.08 (sawa na sh bilioni 1.40) kwa njia ya mtandao wa kompyuta, mali ya Benki ya Barclays, inayomkabili Mkurugenzi Mtendaji wa Dar es Salaam Cement Muslim na mfanyabiashara maarufu wa mafuta nchini, Merey Ally Saleh (41), anayefahamika zaidi kwa jina la Merey Balhabou na wafanyakazi saba wa benki hiyo.


Wakili wa Serikali, Teophil Mutakyawa mbele Hakimu Mkazi Euphemia Mingi, alidai kesi hiyo ilikuja jana kwa ajili ya upande wa mashitaka kuweza kumuunganisha Rugaibura na washitakiwa wengine tisa, hivyo kufanya sasa kesi hiyo kuwa na washitakiwa kumi.

Akisoma hati hiyo ya mashitaka, Mutakyawa alidai kuwa ina jumla ya mashitaka 20, na kwamba Rugaibura ambaye anatetewa na wakili wa kujitegemea, Daudiosus Ishengoma, anakabiliwa na mashitaka kumi.

Mbali na Balhabou, washitakiwa wengine ni Meneja Mwendeshaji wa Kigamboni Oil Co. Ltd, Abdallah Said Abdallah (48), Winford Mwang’onda, Shubira Mutungi, Naima Saria, Upendo Mushi, Magreth Longway, Emmanuel Mukoni na Ramadhani Khamis.

Wakili huyo alidai kuwa, shitaka la kwanza ni la kula njama na kutenda kosa ambalo linawahusu washitakiwa wote ambapo Oktoba 29-30 mwaka jana, wanadaiwa kula njama katika eneo lisilofahamika jijini Dar es Salaam, walifanya udanganyifu na kuiibia benki hiyo dola za Kimarekani 1,081,263.00.

Shitaka la pili alidai ni la kughushi, kwamba Oktoba 27, mwaka jana, katika eneo lisilofahamika, walighushi ujumbe wa kasi wenye namba SEQ 000303, kuonyesha kwamba ni halisi na kuutuma kwenye akaunti Na. 0157001698 ya Ramadhani Mussa Hamisi, na kisha kuhamisha dola za Kimarekani 80,500, huku wakijua ujumbe huo umeghushiwa.

Shitaka la tatu linawakabili wafanyakazi wa benki hiyo ambalo ni la kusaidia kosa la wizi kwa kufungua akaunti feki Na. 0008001993 ya Kigamboni Oil Co. Ltd, iliyokuwa na dola za Kimarekani 700,767 na 299,974 bila akaunti hiyo kufunguliwa kwenye kaunta ya benki hiyo, kwa lengo la kuendelea kuiba dola za Kimarekani 1,000,741.00, mali ya benki ya Barclays.

Katika shitaka la nne, washitakiwa hao ambao ni wafanyakazi wa Barclays wanadaiwa kusaidia watu wengine kuiibia benki hiyo.

Inadaiwa kuwa, walifungua kinyemela akaunti Na. 0157001698 ya Ramadhani Mussa Khamisi iliyokuwa na akiba ya dola 80,500.00 ambapo ilimsaidia Khamisi kuendelea kuiba dola 80,500 mali ya benki hiyo.

Aliendelea kudai kuwa shitaka la tano ni la kufungua akaunti kwa njia haramu, linalomkabali Subira Mutungi pekee ambaye anadaiwa aliifungua bila mwajiri wake kujua na kisha kuingiza dola 299,974.00 kwenye akaunti Na.00080001993 ya Kigamboni Oil Co. Ltd, huku akijua kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.

Shitaka la sita linalomkabili Mutungi ni kwamba, Oktoba 28, mwaka jana katika makao makuu ya Barclays akiwa mwajiriwa wa benki hiyo, kama muingiza kumbukumbu wa benki, kwa nia ovu aliingiza isivyo halali dola 80,000.00 kwenye akaunti Na. 0157001698 ya Ramadhani Khamisi, huku akijua kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.

Shitaka la saba ambalo ni kwa ajili ya mshitakiwa wa sita (Mukono), ni la kujaribu kuiba, ambapo Novemba 3 mwaka 2008 katika makao makuu ya Barclays, bila halali yoyote, aliwasilisha hundi yenye namba 0000002 ya sh 60,000.00 na hundi yenye namba 000006 ya dola 40,000.00 kwa lengo la kutoa kiwango cha fedha kilichotajwa kutoka kwenye akaunti Na. 0222824801 ya Gralic Inter Traders Ltd.

Shitaka la nane ni la kujaribu kuiba, linalomhusu mshitakiwa wa sita, Mukono ambapo tarehe na wakati kama huo, alijaribu kuiba kiasi hicho cha fedha katika makao makuu ya Benki ya Stanbic.

Shitaka la tisa linamhusisha mshitakiwa wa saba (Khamis), ni la wizi, kwamba kati ya Oktoba 29-30 mwaka jana katika benki ya Barclays, tawi la Slipway, bila halali yoyote aliiba fedha taslimu dola za Kimarekani 80,500,000, mali ya benki hiyo.

Shitaka la kumi linalowakabili washitakiwa wa kwanza, pili, tatu, nne, tano, nane, tisa na kumi ni la kughushi, ambapo inadaiwa kwamba Oktoba 27 mwaka jana, walighushi ujumbe wa kasi wenye Na. SEQ.000305 ili kuonyesha ni halisi na kuutuma kwenye akaunti ya Kigamboni Oil Co. Ltd Na. 8001993 na kisha kuhamisha dola za Kimarekani 700,769.00.

Aliendelea kudai kuwa, shitaka la 11, pia ni la kughushi ambalo linawahusu tena washitakiwa wote hao, kwamba baada ya kughushi ujumbe huo wa kasi, walifanikiwa kuiba kwa kuhamisha dola za Kimarekani 299,974.

Shitaka la 12 ambalo linawahusisha washitakiwa wa nane, tisa na kumi (Said, Balhabou na Rugaibura), ni la wizi, kwamba wafanyabiashara hao Oktoba 30 mwaka jana katika muda tofauti katika makao makuu ya benki hiyo, bila halali yoyote waliiba fedha taslimu dola za Kimarekani 700,769.00 mali ya benki ya Barclays.

Wakili Mutakyawa alidai shitaka la 13 ni la wizi ambalo pia linawahusisha wafanyabiashara hao watatu, kwamba Oktoba 30 mwaka jana, katika makao makuu ya benki hiyo waliiba fedha taslimu dola za Kimarekani 299,974.00.

Shitaka la 14, linamhusu mshitakiwa wa kumi (Rugaibura), kwamba Oktoba 30 mwaka jana katika benki ya Stanbic tawi la May Fair bila halali yoyote kupitia akaunti Na. 0222824801 aliiba fedha taslimu dola za Kimarekani 200,000.00.

Shitaka la 15 ni la wizi ambalo linamkabili Rugaibura peke yake ambapo anadaiwa kuwa, Oktoba 31, mwaka jana katika tawi la Stanbic May Fair, alitumia akaunti Na. 012282480 na kuiba fedha taslimu sh 200,000,000 kwa kutumia hundi yenye Na. 000001, mali ya Barclays.

Shitaka la 16, Mutakyawa alidai pia linamhusu mshitakiwa wa kumi pekee (Rugaibura), la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu ambapo Oktoba 30, mwaka jana, kitika makao makuu ya Barclays, alijipatia fedha taslimu dola za Kimarekani 300,000.00 kupitia hundi yenye Na. 100103 toka kwa Daudi Salehe wa Kigamboni Oil Co. Ltd.

Baada ya kuwasilisha hundi hiyo, alidai malipo hayo yametoka kwa mteja wake, ambaye ni mwekezaji kwenye mgodi wa dhahabu mkoani Mara, huku akijua kwamba si kweli.

Shitaka la 17 ni kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu, linalomkabili pia Rugaibura, ambaye anadaiwa kuwa akiwa Mkurugenzi wa Gralic Traders Co. Ltd, Oktoba 30, mwaka jana katika benki ya Stanbic tawi la May Fair, kwa nia ovu, aliwasilisha hundi iliyoghushiwa Na.120795 na kujipatia dola za Kimarekani 345,000.00, mali ya Barclays.

Shitaka la 18 ni kwa ajili ya Rugaibura pekee la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu ambapo Oktoba 30 mwaka jana, katika makao makuu ya Barclays, alijipatia fedha taslimu sh 200,000,000 kupitia hundi Na.100020 kutoka kwa Daud Saleh wa Kigamboni Oil Co. Ltd.

Baada ya kughushi hundi hiyo, alionyesha kuwa ni halisi na kwamba hayo ni malipo halali ambayo amelipwa ili aweze kuendeleza mrandi wa uwekezaji wa mgodi wa dhahabu mkoani Mara.

Aidha, wakili huyo wa serikali alidai pia shitaka la 19, linamhusu mshitakiwa huyo peke yake, ambalo ni la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu, kwamba akiwa ni Mkurugenzi wa Gralic Traders Co. Ltd, tarehe hizo katika benki ya Stanbic tawi la May fair aliwasilisha hundi ya kughushi yenye Na.157856 na kufanikiwa kujipatia sh 300,000,000 mali ya Barclays.

Shitaka la 20 ni la Rugaibura la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu. Kwamba akiwa mkurugenzi wa kampuni hiyo, Oktoba 30 mwaka jana, katika Benki ya Stanbic tawi la May Fair, aliwasilisha hundi yenye Na.100102 kwa lengo la kujipatia dola za Kimarekani 445,000.00, mali ya Barclays.

Hata hivyo, washitakiwa wote walikana mashitaka yote na upelelezi wa kesi itakayotajwa tena Novemba 2, haujakamilika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Septemba 18,2009

No comments:

Powered by Blogger.