Header Ads

KORTI YAKATAA SAMAKI WA MAGUFULI KUGAWIWA BURE

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, imelikataa ombi la upande wa mashitaka katika kesi ya uvuvi haramu inayowakabili raia 37 wa kigeni waliokamatwa kwenye meli ya Tawariq 1, la kutaka uruhusiwe kugawa samaki hao bure.


Uamuzi huo ulitolewa jana na Jaji Razia Shekhe baada ya kubaini hati ya kiapo kilichoambatanishwa na ombi hilo kuwa na dosari za kisheria.

Jaji Shekhe alizitaja dosari hizo kuwa ni upande wa mashitaka kushindwa kueleza kampuni au mtu aliyefanya tathimini ya samaki hao pamoja na kutotaja thamani yake.
“Kwa sababu ya dosari hizo, mahakama hii inatupilia ombi la upande wa mashitaka ulioiomba mahakama iwaruhusu kugawa bure samaki wale ambao ni kielelezo,” alisema Jaji Shekhe.

Awali, wakili wa utetezi Ibrahimu Bendera alipinga ombi hilo kwa madai kuwa samaki hao ni kielelezo na kwamba kinachotakiwa kisheria ni samaki hao wauzwe na fedha zitakazopatikana zihifadhiwe mahakamani.

Kabla ya upande wa mashitaka kuwasilisha ombi hilo mwishoni mwa mwezi ulipita, Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, John Magufuli alikaririwa kwenye vyombo vya habari akiutangazia umma kwamba samaki hao watagawiwa bure na kwamba taratibu za kuwagawa zinafanyika.

Wakati Magufuli akitoa taarifa hiyo kwa umma, upande wa mashitaka ulikuwa haujawasilisha ombi la kutaka samaki hao wagawiwe bure na wala mahakama haikuwa imetoa uamuzi wa samaki kugawiwa.

Washitakiwa katika kesi hiyo wanadaiwa kuwa kuwa Machi 8 mwaka huu, majira ya saa sita usiku katika ukanda wa Bahari ya Hindi, ndani ya eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, walikamatwa wakivua samaki bila leseni.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Desemba 4 mwaka 2009

No comments:

Powered by Blogger.