Header Ads

TUMECHOSHWA NA UKATILI WA MADAKTARI

Na Happiness Katabazi JANUARI 30 mwaka huu, gazeti hili lilichapisha makala niliyokuwa nimeiandika mimi iliyokuwa na kichwa cha habari kisemacho ‘Ni mgomo wa madaktari kweli au? Walivyogoma mara ya pili ulioanza Machi 7 mwaka huu, niliandika makala ndefu iliyokuwa na kichwa cha habari kisemacho ‘Madaktari waungwana hawasifiwi ushenzi’.Haikuchapishwa na gazeti hili kwasababu ambazo sitazitaja adharani ila niliisambaza kwenye mitandao ya kijamii. Na ndani ya makala hizo mengi niliyokuwa nimeyabashiri ndiyo sasa yameanza kujitokeza na tunayashudia.Lakini leo tena naandika makala ya tatu kuhusu mgomo huu wa tatu ulioanza wiki iliyopita naninasisitiza tena mgomo huo ni batili na umedharau amri ya Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, ambayo wiki iliyopita ilitoa amri ya kutangaza mgomo huo kuwa ni haramu lakini cha kushangaza madaktari wetu ambao ni wasomi ndiyo wamekuwa mstari wa mbele kukaidi amri hiyo halali ya mahakama na mhimili wa serikali kisheria ndiyo unatakiwa uhakikishe amri hiyo na nyingine za mahakama zinatekelezwa kwa vitendo na sivinginevyo umeshindwa kusaidia utekelezaji wa amri hiyo kwa kuwakamata madaktari hao waliokaidi amri ya mahakama na kuwafikisha mahakamani ili wajibu mashitaka ya ni kwanini wamekaidi amri ya mahakama. Matokeo ya kushindwa kutekeleza amri hiyo ya mahakama ndiyo sasa kunasababisha maskini wenzetu ambao ni wagonjwa wanashindwa kutibiwa na wengine kudaiwa kupoteza maisha kwasababu ya madaktari hao ambao kwa makusudi wameamua kukaidi amri ya mahakama na serikali inaendelea kuwachekea. Ibara ya 13 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inasema “ Watu wote ni sawa mbele ya sheria,na wanayo haki ,bila ya ubaguzi wowote,kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria’. Sasa kwa Ibara hiyo ya Katiba inaanza kuonekana sasa baadhi ya madaktari waliogoma wapo juu ya sheria kwani wanakataa kutekeleza amri ya mahakama na serikali inawaacha watu hao waendelee kudharau amri hiyo wakati siku zote inafahamika kuwa nchi yetu inaongozwa na misingi ya sheria. Lakini ni serikali hii kupitia jeshi la polisi ndiyo imekuwa ikiakikisha amri mbalimbali zinazotolewa na mahakama zinatekelezwa kikamilifu lakini cha kushangaza serikali hii inashindwa kuwafikisha mahakamani madaktari hao wanaoikaidi amri hiyo jambo ambalo hivi sasa limeanza kutafsiriwa kuwa kada ya madaktari wapo juu ya sheria. Nikiachana na hilo nivigeukie vyombo vyetu vya habari kuhusu ushiriki wao katika mgomo huu wa madaktari,kwa namna moja au nyingine vyombo vingi vya habari vimekuwa vikitoa nafasi kubwa kwa madaktari wanaogoma na kuinyima serikali na jamii inayopinga mgomo huo kusikika kupitia vyombo vya habari na baadhi ya wanahabari wakiwa ndani na nje ya vyombo vya habari wamekuwa wakisikika wakikerwa na tabia hiyo ya madaktari ila wanaogopa kuandika makala na habari za kuwakosoa madaktari kwasababu ya kuhofia eti siku wakiugua na kwenda hospitalini huko wanaweza kujikuta wakichomwa sindano za sumu na madaktari hao. Hali iliyosababisha wananchi wengi katika mgomo wa kwanza na wa pili kuona madaktari wapo sahii na mgomo huu wa tatu kadri siku zinavyozidi kusonga mbele wananchi na baadhi waandishi wa chache wameanza kutowaunga mkono hadi kufikia kuwapachika majina mabaya madaktari hao kuwa wana roho za kikatili zaidi ya wa kikundi cha ‘Boko Haram’. Hii ni changamoto kwa sisi vyombo vya habari tujitazame upya na tuifanyie kazi. Hakuna ubishi kwamba madaktari wanadai maslahi yao na serikali katika mgomo wa pili uliyatimiza baadhi ya madai na ukaidi kuendelea kuyafanyia kazi madai yaliyosalia na hakuna ubishi kwamba wanafanyakazi katika mazingira magumu na pia nao wagonjwa nao wakati mwingine hawapatiwi tiba za uhakika kutoka kwa madaktari. Lakini cha kushangaza madaktari hawa wameonekana ni watu walafi na wabinafsi wanaotaka masulufi manono wapewe wao tu na kada nyingine zisipate,wameonekana kukosa subira,hawana imani na serikali yao ambayo ndiyo mwajiri wao na ndiyo anayewalipa mishahara na wengine walisomeshwa na serikali hiyo. Kwa mtindo huu ni wazi kabisa hawa wanaonekana hawana dhamila ya dhati ya kuitumikia serikali kwa moyo wa uzalendo kwani wamedhiirisha wazi kuwa muhimu kwao ni fedha kuliko kuokoa maisha na kutibia wagonjwa ambao ndiyo hasa wanasababisha wao wapate mshahara,wasome.Hivi bila wagonjwa nyie madaktari mngekuwa na hiyo ajira ya udaktari? Ni madaktari hawa hawa akiwemo huyo Dk.Steven Ulimboka wamekuwa wakiutangazia umma kuwa pale hospitali ya Muhimbili hakuna dawa wala vifaa, sasa mbona tumeshuhudia yeye Ulimboka ambaye amepigwa na watu wasiyojulikana akifikishwa hospitalini hapo na kulakiwa madaktari wenzake wakaanza kumtibia na jinsi gani walivyomakatili wakagoma kuwatibia wananchi wenzetu siku hiyo wakamkimbilia kumtibu Ulimboka kwa dawa na vifaa ambavyo vimenunuliwa kwa kodi zetu. Ni madaktari hawa hawa wanaojigamba kuwa wao ni madaktari bingwa sasa mbona wameshindwa kumtibia mwenzao hadi wamempeleka nje ya nchi akatibiwe? Tumesikia madaktari hawa ambao kila kukicha wanadai mishahara wanayolipwa ni midogo na mazingira ya kazi ni mabovu, tuwaulize hayo mamilioni waliyochanga ghafla ya kumsafirisha mwenzao wameyapata wapi? Kama wanauzalendo kweli wa Taifa hili ni kwanini hizo fedha walizozichangisha wangezitumia kununulia vifaa na kuviweka pale Muhimbili ili vije kumtibia mwenzao na watanzania wengine? Imeelezwa kuwa safari ya Ulimboka kwenda nje imegubikwa na usiri mkubwa,hivi kama siyo upuuzi ni kitu gani?Mnaficha nini na mnamficha nani kwamba Ulimboka ameenda kutibiwa nchi gani? Hivi leo hii mtu anaweza kwenda nje ya nchi bila kukata tiketi ya ndege,visa ambazo zitaonyesha anakwenda nchi gani? Kama mnaisi serikali ndiyo imemfanyia unyama ule na mkaamua kumuondoa kwa siri pale Muhimbili, hivi kwa akili zenu mnafikiri huko mlikopo mpeleka kutibiwa ndiyon serikali ya Tanzania haipo? Na kama mnafahamu serikali ndiyo imemtendea unyama huo pelekeni ushahidi mahakamani au pelekeni ombi mahakamani na kutaka muendeshe kesi binafsi(Private Prosecution). Hivi kama sio uhuni na ukatili tunafanyiwa na hawa baadhi ya madaktari wa serikali ambao mishahara yao inatokana na kodi zetu nini na wakati huu wanagoma bado wanaendelea kupewa mishahara? Na mbaya zaidi wananchi wanashindwa kuwachachamalia hawa madaktari lakini ingetokea vyama vya siasa vimeitisha maandano ya kupinga mfumuko wa bei,malipo ya Dowans ni sisi wananchi tungejitokeza kuundamana tena hata kama hayo maandamano ni haramu lakini hili la madaktari kuendesha mgomo haramu ambao wananchi wenzetu wanaumia na kupoteza maisha wala hatuonekani kabisa kulichukulia uzito wa aina yake.Sisi ni watu wa ajabu sana.Tumekuwa na kasumba ya kushabia mambo yasiyo na msingi ila mambo ya msingi ambayo yanatuhusu moja kwa moja hatuyatilii maanani. Rai yangu kwa madaktari wanaogoma, kama wanaona serikali haiwalipi vizuri siwaache hiyo kazi wakatafute kazi sehemu nyingine ambapo watalipwa mishahara minono?Kwanini muundelee kumng’ang’ania bwana(serikali) ambayo kwa akili zenu mnaona haiwajali na haiwapendi? Tanzania bado ina ardhi kubwa ambayo imegunduliwa kuwa ina madini, simuende basi kwenye ardhi hizo mkachimbe madini ili muwe na mahela mengi kama mnavyotaka kuliko kung’ang’ania kazi serikali ambayo nyie mnadai hamlipwi vizuri?Kwani mmekatazwa. Maana ninachokiona mimi hivi sasa hawa wanaogoma ni watu ambao kwa akili zao timamu wameamua kukiuka viapo vyao, wameichoka kazi ya kuwatibu wa gonjwa kwa kisingizio cha kudai maslahi manono,daktari mwenzao Ulimboka kafanyiwa ukatili.Sasa kama kafanyiwa ukatili na watu wasiyojulikana ni kwanini sasa mgomee amri ya mahakama,agizo la serikali la kuwataka mrejee kazini na mgome kuwatibu wagonjwa?Kwani ndiyo waliomfanyia ukatili huo? Mkae mkijua hizo roho za wananchi wenzetu zinazopotea kwaajili ya mgomo wenu ipo siku mtadaiwa na mungu na mathara yake mtayapata hapa hapa duniani kwani mungu amewapa vipawa mje mvitumie duniani kwaajili ya kuwahudumia watu wake,sasa nyie mnapingana na agizo la mungu na maadili ya taaluma yenu, minaamini ipo siku mungu atawaadhibu na msije kulia na mtu. Mwisho ni malizie kwa kuwataka wanaharakati na wale vyama vya siasa akiwemo Kada ya Chadema, Godbles Lema ambao wametoa matamko ya kulaani kitendo alichofanyiwa Ulimboka na Lema akasema akifa Ulimboka atalala barabarani, nawataka wageuze upande wa pili wa shilingi na waone kuwa kuna mamia ya wagonjwa wanakosa huduma na kupoteza maisha yao kwaajili ya mgomo huo haramu,mbona makundi hayo hatusikii yakitoa tamko ya kuwasema wananchi hao na kulaani mgomo huo haramu wa kisheria ambao mahakama ilisema mgomo huo ni batili?. Wewe Lema unayesema utalala barabarani Ulimboka akifa, tumuulize huyu Lema ni kwanini alishindwa kulala barabarani siku ile Jaji Gabriel Rwakibalila wa Mahakama Kuu Kanda ua Arusha alipotoa hukumu dhidi yake ambapo alimvua ubunge na kumfungia kugombea ubunge baada ya kumtia hatiani kwa makosa ya kutoa lugha chafu? Maana hukumu hiyo ndiyo imemfanya Lema hivi sasa awe kaka sisi tusiowabunge kwani analifuatilia bunge kupitia redio na televisheni, hapati tena posho na mshahara na hapewi heshima na stahili za kibunge tena,sasa tumuulize sasa alishindwa kulala barabarani kwa hukumu hiyo iliyokuwa ikumuhusu na imemwathiri yeye binafsi ndiyo leo hii atakuwa na ujasiri wa kufanya hivyo kwa Ulimboka ambaye hawana hata undugu? Nimalizie kwa kuwataadhalisha madaktari wetu kuwa huo mgomo haramu wanaoufanya ipo siku watakuja kutokea baadhi ya ndugu wa wagonjwa watakaofika mahospitalini hapo halafu mkatae kuwapa huduma watajiuliza maswali yafuatayo; Hivi hospitali hizo ni za serikali?Dawa na vifaa vya mahospitalini humo sizimenunuliwa kwa kodi za wananchi?Madaktari siwamesomeshwa kwa kodi za wananchi? Wakimaliza kujiuliza maswali hayo watamalizia kwa kuwadhuru na wala msije kulia na mtu kwani sikila mtu anaweza kuvumilia huo uhuni na ukatili mnaotufanyia. Mungu ibariki Tanzania,Mungu Ibariki Afrika 0716 774494 www.katabazihappy.blogspot.com Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Julai 3 mwaka 2012.

2 comments:

Anonymous said...

Kwamujibu wa bajeti ya mwaka 2012/2013 Mh.Selina Kombani ambae ni WNOR-Utumishi anasema serikali imetenga kiasi cha Tshs 3.7 Trillion kwaajili ya mishahara ya watumishi wote wa serikali wote Tanzania hivyo kwa madai ya Madaktari kama wakilipwa wanavyotaka inamaana watahitaji zaidi ya 2Trillion sasa hii ni haki kweli kwa watumishi wengine kubakiwa na hiyo 1.7Trillion tu?wakati huohuo Walimu nao wamedai kama serikali ikiwalipa kiasi hicho na wao wanataka kima cha chini kuwa 1million sasa hii nchi tunaipeleka wapi?au tunamkomoa nani kama sio kumuumiza mwananchi masikini ambae ndiyo mlipa kodi?Ombi langu ni kuwa tujitafakari kabla ya kufanya maamuziambayo mwisho wa siku yanakuja kutuumiza sisi wenyewe na hao wanaoshabikia watakuja kulia pale maisha yatakapokua magumu eti kwaajili ya kuwafurahisha watu wachache au kundi la watu.

Anonymous said...

Mgomo hu unapambishwa na watu wanaotafuta maslahi yao binafsi ,wanashindwa kuelewa kuwa uhai wa mwanadamu haununuliwi.
hivi hao wanaharakati kazi yao ni kutetea kikundi kidogo cha madaktari au kutetea wananchi? Siasa chafu za watu wasio na utu zinaharibu akili za watu na sasa wananchi wanakufa tu .mungu atalipa na ipo siku watajibu .
KIJO BISIMBA alionekana akiwa kwenye ambulance na DR Ulimboka,anatuambia nini watanzania? watu wangapi wamekufa tangu mgomo uanze? huyo ulimboka ndio wa muhimu kuliko watu wote nchi hii???? ANATETE NINI? AJITANGAZE TUJUE YEYE NI MWANASIASA ,tumechoshwa na haya yote na sasa wananchi watakapoanza kuchukua hatua na kuwapiga hao madaktari ndio watakapopelekana vizuri nje kutibiwa kwasababu hatutaruhusu wajitibie na dawa zetu na vifaa vilivyonunuliwa kwa kodi zetu.tumechoshwa na ukatili huuu.

Powered by Blogger.