Header Ads

KESI YA LULU YAFUNGWA KISUTU,YAAMISHIWA MAHAKAMA KUU

*Dhamana ya Hassanor yasikilizwa, uamuzi utatolewa Jumatatu
Na Happiness Katabazi
UPANDE wa serikali katika kesi ya kuua bila kukusudia inayomkbaili msanii wa filamu nchini Elizabeth Michael maarufu kama Lulu ambaye anadaiwa kumuua bila kukusudia msanii mwenzake Steven Kanumba, jana ulimsomea kwa mapana kesi inayomkabili mshtakiwa huo (Comittal Procedings).
Wakili Mwandamizi wa Serikali Shadrack Kimaro   mbele ya Hakimu Mkazi Mmbando alidai kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya kumsomea maelezo ya awali mshtakiwa huyo na  alianza kwa kumsomea maelezo uya mashahidi ambao anakusudia kuwaleta katika kesi hiyo  na maelezo ya onyo  ya mshtakiwa huyo  pamoja na kuvitaja vielelezo watakavyovitumia katika kesi hiyo hiyo itaakapoanza kusikilizwa Mahakama Kuu.
Wakili Kimaro alieleza kuwa pia wataleta mashahidi tisa  na vielezo  ikiwemo ramani ya eneo la tukio kwenye chumba alichofia marehemu Kanumba, ripoti ya uchunguzi wa kifo na maelezo ya onyo ya Lulu.
Aliwataja mashahidi hao wanaokusudia kuwaleta katika kesi hiyo ni  Sethi Kamugisha (24) ambaye alikuwa akiishi na Kanumba, Sophia Kassim (45) ambaye alimpangisha Kanumba, Dk Paplas Kagaiga (29) ambaye alikuwa daktari wa Kanumba, Esther Zefania (40) askari polisi Oysterbay, Morris Sefwao mkazi wa Kijitonyama, Mrakibu wa Polisi (ASP) Daniel Shilla kutoka ofisi ya Mkuu wa Upelelezi mkoa wa Kinondoni, Dk Magreth Ibobo (40) ambaye aliombwa na familia ya Kanumba kusimamia upasuaji wa mwili, Inspekta Mwesiga (35) Afisa Uhamiaji kutoka kituo cha Horohoro Tanga na Ditective Sajent Renatus wa kituo cha polisi Oyesterbay.
Akisoma maelezo ya onyo ya Lulu mbele ya Hakimu Mkazi Augustina Mmbando, wakili wa serikali, Shadrack Kimaro, alidai kuwa Lulu alitoa maelezo hayo Aprili 7 mwaka huu katika kituo cha polisi Oysterbay mbele ya askari wa kituo hicho Ditektive Sajent Renatus.
Alidai kuwa Lulu alizaliwa mwaka 1994 na kwamba alimaliza kidato cha nne katika shule ya Sekondari ya Midway na baada ya hapo aliendelea na shughuli za sanaa ambazo aliianzia kuzifanya tangu mwaka  2000.
Kimaro alidai Lulu alifahamiana na Kanumba kwa muda wa miaka 10 na walikuwa wakifanyakazi za sanaa ya uigizaji pamoja  na Januari mwaka huu ndipo walipoanza rasmi mahusiano ya kimapenzi.Katika  mahusiano yao ya kimapenzi hawakuwahi kuishi pamoja isipokuwa alikuwa akienda nyumbani kwa marehemu anapojisikia na alikuwa wakati mwingine akilala huko.
Wakili huyo alidai kuwa katika kipindi cha miezi minne ya mahusiano yao walikuwa wakigombana mara chache lakini sababu kubwa ilikuwa ni wivu wa mapenzi kwa sababu wote walikuwa hawaaminiani katika mahusiano..
Pia wakili huyo alidai kuwa Aprili 5 mwaka huu Kanumba na Lulu walitumiana ujumbe mfupi wa simu. Baadhi ya jumbe hizo zilisomeka hivi.
Kanumba: Uniheshimu, unanidharau, unanijibu unavyotaka wewe.. nakupenda sana..this love kill me soon..vipi baby mzima umekula? nakupenda mke wangu..natarajia kwenda USA hivi karibuni je nikuletee zawadi ipi kwa ajili ya birthday yako?
Alidai kuwa Lulu alimjibu kwa kumtumia ujumbe wa kumtuliza kama vile nakupenda mme wangu..niletee zawadi yoyote ile lakini ujumbe mwingine haukumbuki na kwamba walipatana siku hiyo hiyo.
Alidai kuwa jioni ya siku hiyo Lulu alimpigia simu Kanumba na baada ya muda mfupi alikwenda nyumbani kwake Sinza Vatican. Alidai kuwa alipofika kwa Kanumba chumbani kwake alimkuta akinywa pombe ambayo ilikuwa imechanganywa na soda na ghafla simu yake iliita na alipotoka nje kutaka kwenda kuisikiliza Kanumba alimfukuza hadi barabarani.
Alidai kuwa baada ya kumkimbiza  alimkamata na kuanza kumpiga vibao na mateke huku akilalamika kwamba anamdharau na alimpeleka hadi chumbani ambapo alichukua panga lililokuwa chini ya kitanda na kuanza kumpiga kwa ubapa.
Alidai kuwa baada ya kumpiga kwa upanga   ghafla alitupa panga chini huku akiwa amesimama alianza kupumua kwa taabu na baada ya muda mfupi alipojigonga ukutani na kuanguka chini. Alidai baada ya kuanguka, Lulu alikimbia na kwenda kujifungia chooni kwa hofu na baada ya muda alitoka na maji na kwenda kummwagia Kanumba lakini hakuamka.
Alidai kuwa baada ya kuona hali hiyo alishikwa na hofu na kuamua kukimbia kwenye ufukwe wa Coco Beach.Alidai kuwa akiwa huko alipewa taarifa kuwa Kanumba amefariki na ndipo alipompigia simu rafiki yake ili aende kumsaidia kuendesha gari waelekee kwenye msiba.
Kwa mujibu wa maelezo ya mashahidi yaliyosomwa mahakamani hapo inadaiwa kuwa Aprili 6 mwaka huu saaa 3 usiku Kanumba akiwa nyumbani kwake, alimwambia mdogo wake Sethi asitoke kwakuwa kuna mahali wanataka kwenda hivyo amsindikize na kwamba alikuwa akinywa kinywaji aina ya Wisky.
Inadaiwa kuwa ilipofika majira ya saa 6 usiku Lulu alifika nyumbani kwa Kanumba na kuingia hadi chumbani na baada ya muda walianza kugombana na baada ya kuanguka mapovu yalianza kumtoka mdomoni.
Aidha alileza kuwa  baada ya Kanumba kuanguka, mdogo wake aliwasiliana na daktari wa Kanumba na baada ya kufika aligundua kuwa Kanumba tayari alikuwa amefariki lakini alishauri apelekwe hospitali ndipo walipoamua kumpeleka hospitali ya Taifa Muhimbili ambapo baada ya kupimwa iligundulika kuwa amefariki.
Na  baada ya Kanumba kufariki, Lulu alitoroka na baada ya kutafutwa aliwekewa mtego na kukamatwa saa 11 alfajiri katika eneo la Bamaga na kupelekwa kituoni Oysterbay.Uchunguzi wa awali wa polisi ulionyesha kuwa hakukuwa na jeraha lolote kuanzia kichwani hadi mwilini.
Baada ya kusomwa maelezo hayo Hakimu Mmbando alimuhoji Lulu kama ana lolote la kuongea na baada ya kujadiliana na wakili wake, Lulu alijibu kuwa ana cha kuongea.
“Mahakama hii inaziarifu pande zote mbili katika kesi hii kuwa kesi yenu leo imefikia mwisho katika mahakama hii  hivyo jarada la kesi hii linaamishiwa mahakama kuu  tayari kwaajili ya kuanza kusikiliza  na kwamba  Lulu utaendelea kuishi rumande  hadi pale utakapokea wito toka Mahakama Kuu wa kukuita kwaajili ya kesi yako.”alisema Hakimu Mmbando na kuahirisha kesi hiyo.

Wakati huo huo Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, jana isikiliza ombi la kuomba apatiwe dhamana Mwenyekiti wa Mpira wa Soka mkoa wa Pwani(COREFA),Hussein Othman Hussein 'Hassanor' na wenzake sita wanaokabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi ya Sh bilioni 1.1 ambapo wanadaiwa walisafirisha kontena na pembe za ndovu kinyume cha sheria kutoka Tanzania kwenda Hong Kong nchini China.

Jaji Zaina Mruke alisikiliza ombi hilo ambapo Hassanor alikuwa akiwakilishwa na wakili wa kujitegemea Richard RWeyongeza ambao upande wa Jamhuri ulikuwa ukiwakiliwa na mawakili wa serikali waandamizi Biswalo Mganga, Mutalwemwa Kishenyi, Benard Ikokola ambapo hata hivyo mawakili wa serikali waliomba Hassanor asipewe dhamana kwasababu ametenda kosa la kesi hii wakati tayari anakabiliwa na kesi ya awali Na.209/2011 iliyopo mahakama ya KIsutu mbele ya Hakimu Devota Kisoka ,na kisheria mtu yoyote anayetenda kosa wakati yupo ndani ya dhamana ,mshtakiwa huyo anatakiwa asipewe dhamana.

Jaji Mruke aliarisha kesi hiyo jana saa 12:20 jioni hadi jumatatu saa tatu asubuhi ambapo atakuja kutoa uamuzi wa ama ampatie dhamana Hassanor na wenzake au laa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Desemba 22 mwaka 2012.
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Desemba 22 mwaka 2012.

No comments:

Powered by Blogger.