Header Ads

MANJI,MWALUSAKO WAKIMBILIA MAHAKAMA YA RUFAA


Na Happiness Katabazi

MWENYEKITI wa Klabu ya Yanga Yusuph Manji na Katibu Mkuu wake, Lawrence Mwalusako, jana walifika katika Mahakama Kuu Diveshi ya Kazi Dar es Salaam lakini hawakusimama kizimbani kujieleza ni kwanini wasichukuliwe hatua za kisheria  kwa kosa la kudharau amri ya mahakama.

Manji ambaye pia ni mfanyabiashara na Mwalusako walifika mbele ya Msajili wa mahakama hiyo Mohamed Gwae lakini hawakuhojiwa chochote kwasababu jalada la kesi limepelekwa Mahakama ya Rufani  kwaajili ya kufanyiwa marejeo.

Katika kesi hiyo timu ya  Yanga inadaiwa  kukiuka umuzi  uliyokwishatolewa na mahakama hiyo ambayo iliitaka timu hiyo iweke  mahakamani Sh milioni 106, kwasababu ilishindwa kuwalipa walalamikaji  katika kesi hiyo, ambae ni Kipa wa zamani wa timu hiyo  Stephen Marashi na beki raia wa Malawi, Wisdom Ndlovu.

Jalada la kesi hiyo hiyo   limeitwa Mahakama ya Rufaa  baada ya mdaiwa (Timu ya Yanga), kuwasilisha ombi katika mahakama hiyo ya Rufani  linaloiomba mahakama hiyo ifanye marejeo ya uamuzi uliotolewa na Mahakama Kuu Diveshi ya Kazi ambao uliitaka timu hiyo  iweke kiasi hicho cha fedha mahakamani.

Jana Msajili Gwae alisema kuitwa kwa Manji na Mwalusako tena mahakamani hapo, kutategemea uamuzi utakaotolewa na Mahakama ya rufaa.

Ombi hilo la Yanga la linaloomba Mahakama ya Rufaa ifanyie  marejeo uamuzi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi , waliliwasilisha Machi 25 mwaka huu, chini ya hati  ya dharura likiomba mahakama hiyo ya juu kabisa nchini iitishe jalada la kesi ya msingi ili iweze kuupitia mwenendo mzima wa kesi hiyo iliione uamuzi huo ulikuwa sahihi.

Kwa mujibu wa hati ya kiapo kilichoapwa na mdaiwa wa pili ( Mwalusako) inayounga mkono ombi hilo, Oktoba 11 mwaka jana waliwasilisha ombi la marejeo  pamoja na kuwasilisha  ombi la kusitisha utekelezaji wa tuzo ya kuwalipa wachezaji hao.

Kwa mujibu wa hati hiyo, Februali 5 mwaka huu, Msajili Gwae ilikataa ombi la kusitisha utekelezaji wa hukumu hiyo na kuwataka Yanga kuweka fedha hizo mahakamani wakati wakisubiri uamuzi wa ombi la marejeo.

Anadai  kuwa, utekelezaji dhidi ya walalamikaji umekwenda kinyume na utaratibu kwa kuwa msuluhishi alishindwa kuzingatia nafasi ya mlalamikaji katika suala hilo, pia Klabu hiyo haina mali yoyote ya kuweza kutekeleza tuzo hiyo.

Katika kesi ya msingi, Marashi na mwenzake, wameiomba mahakama kumfunga jela mwenyekiti huyo na katibu wake, baada ya timu hiyo kushindwa kutekeleza amri ya mahakama, ikiamuru kiasi hicho kulipwa.

Kamisheni ya Usuluhishi na Upatanishi iliiamuru Yanga iwalipe wachezaji hao fedha hizo kutokana na kukatisha mkataba wao kinyume cha  taratibu, na walitakiwa kulipwa wiki mbili kuanzia tarehe ya hukumu.

Yanga iliingia kwenye mgogoro na wachezaji hao, baada ya kuvunja nao mikataba mwaka 2010 kutokana na sheria mpya ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kuzitaka klabu kuwa na nyota watano tu kutoka nje, hivyo kuwaacha Ndlovu, Mkenya John Njoroge na Mtanzania Marashi. Njoroge alilipwa milioni 17.

Walalamikaji hao wanadai kuwa, walisajiliwa na Yanga kwa mkataba wa miaka miwili kuanzia Machi 18, 2010, wanadai Julai 17, 2010, wakiwa wanajiandaa na kipindi kingine kipya cha msimu wa ligi, Kocha Mkuu wa Yanga, Kostadin Papic aliwaambia kwa mdomo kwamba wao si wachezaji wa Yanga.

Walidai kwa mujibu wa mkataba, Yanga walitakiwa kuwasiliana nao kuhusu kukatisha mikataba yao ndani ya siku saba kabla ya tarehe iliyokuwa imewekwa na TFF, kwa timu za ligi kuu kuwasilisha majina ya wachezaji watakaoachwa jambo hilo liliwakosesha nafasi ya kucheza katika timu nyingine.

Kamisheni iliamuru, Ndlovu alipwe sh. milioni 57 kama mshahara wa miaka miwili, sh. milioni 1.8 kama gharama za usafiri wa kumrejesha Malawi na sh. milioni 20 kama fidia ya kumkosesha nafasi ya kucheza.

Kwa upande wa Marashi, Yanga iliamriwa imlipe sh. milioni 18 kama gharama za kutia saini mkataba na mshahara kwa miaka miwili, sh. milioni 10 kwa kupoteza nafasi ya kucheza na sh. 500,000 kama malipo aliyopaswa kulipwa wakati anatia saini mkataba wa 2009 hadi 2010.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Machi 28 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.