Header Ads

WAKILI AJITOA KESI YA WAFUASI 54 WA PONDA


Na Happiness Katabazi

WAKILI wa upande wa utetezi katika kesi ya wafuasi 54 wa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Issa Ponda ,Hamidu Ubaidi jana alitangaza kujitoa kuendelea kuwatetea washitakiwa hao kwa kile alichodai kuwa kesi hiyo imekuwa ikiendeshwa haraka na mfululizo na mahakama.

Kesi hiyo ambayo jana ilikuja kwaajili ya mshitakiwa wa 24 ananza kutoa utetezi wake lakini wakili Ubaidi mbele ya hakimu Sundi Fimbo aliomba kesi hiyo isiendelee kusikilizwa kwasababu yeye anawasilisha ombi rasmi la kujitoa .
“Naona sitawatendea haki washitakiwa ambao ni wateja wangu  kulingana na kesi hiyo ya maandamano haramu ya kutaka kwenda ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP), Dk.Eliezer Feleshi ili wamshinikize aondoe hati yake ya kumfungia dhamana Ponda, kwasababu kesi hii inavyokwenda haraka na mfululizo kwani sipati muda wa kuzungumza na kuwaandaa washitakiwa”alidai wakili Ubaidi.

Lakini hata hivyo ombi hilo lililamikiwa na wakili mwandamizi wa serikali Benard Kongora, Joseph Mahugo kwa madai hiyo ni mbinu ya kuichelewesha kesi hiyo isimalizike haraka kwani uongozi wa mahakama ndiyo uliotoa fursa ya kesi hiyo iendeshwa mfululizo tangu ilipofunguliwa mahakamani hapo Februali 18 mwaka huu.

“Mhesimiwa hakimu ni huyu huyu wakili Ubaidi,Jumatatu  na Jumatano aliomba kesi hii tuairishe mara kwa lisaa limoja lakini hakutokea …leo hii anakuja kuieleza mahakama kuwa eti anajitoa kuwatetea washitakiwa kwasababu kesi hii inaendeshwa mfululizo na hapati muda wa kuwaandaa washitakiwa wake….sisi upande wa jamhuri tunasema hii ni mbinu ya kutaka kuchelewesha kesi hii isimalizike mapema kwani ni uongozi wa mahakama ndiyo uliotoa fursa ya kesi hii kuendeshwa mfululizo hivyo sisi tunaona tutumie fursa hiyo kuendesha kesi hii”alidai wakili Kongora.

Kwa upande wake hakimu Sundi Fimbo aliarisha kesi hiyo hadi Machi 11 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya washitakiwa kuendelea kujitetea.

Wakati huo huo; Jumla ya washitakiwa tisa wa kesi ya uchochezi na wizi wa malighafi zenye thamani ya Sh. Milioni 59 inayomkabili Ponda na wenzake 49 ,waliyakana maelezo waliyoyatoa wakati wakihojiwa na jeshi la Polisi ambapo wakati walipokuwa wakihojiwa na jeshi la polisi walikiri kuwa walikamatwa katika eneo la kiwanja cha Markas Chang’ombe kinachomilikiwa na kampuni ya agritanza Ltd. Lakini jana wakati wakitoa utetetezi wao walikanusha kukamatwa eneo hilo na kwamba wao walikamatwa na polisi Oktoba 16 mwaka jana,wakiwa ndani ya msikiti wa shule ya Markas Chang’mbe wakisali sala ya Itikafu.

Washitakiwa hao ambao walikuwa wakiongozwa na wakili wao Nassor Juma, ni mshitakiwa 10,11,12,13,14,15,16 na 17.

Wakihojiwa na wakili Mwandamizi wa serikali Tumaini Kweka ni kwanini jana walipopanda kizimbani wametoa maelezo mapya wakati walipohojiwa na polisi walitoa maelezo ya kikiri kukamatwa ndani ya kiwanja hicho ambacho kiliuzwa na Bakwata kwa kampuni ya Agritanza Ltd.

Washitakiwa hao wakijibu swali hilo wengine walidai hawajui kusoma na kuandika na wengine wakadai kuwa hayo maelezo ni yao na saini ni zao ila hizo saini waliziweka kwenye hayo maelezo baada ya kulazimishwa na askari polisi na wengine walidai kuwa hawakufahamu ni kitu gani kilikuwa kikiandikwa na polisi waliokuwa wakiwahoji kwasababu polisi hawakuwasomea hayo maelezo yao, na mshitakiwa mwingine alidai maelezo aliyochukuliwa na askari yaliandikwa na wino wa blue na siyo mweusi kama alivyoonyeshwa jana nakala ya maelezo yake ambayo yapo mahakamani kama kielelezo na wakili Kweka.

Aidha kwa ujumla wao washitakiwa hao walidai kuwa polisi waliwafanyia unyama, waliwapora simu zao za mikononi,waliwatukana matusi ya nguoni na waliwapiga virungu na kwamba baadhi ya askari polisi waliokuwa wamekuja kuwakamata ndani ya msikiti walikuwa wananuka pombe na hawakuvua viatu wakati wanaingia ndani ya msikiti kuwakamata.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Machi 8 mwaka 2013

No comments:

Powered by Blogger.