Header Ads

MAHAKAMA YAMNG'ANG'ANIA PONDA





Na Happiness Katabazi
HATIMAYE Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imemuona Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Sheikh Ponda Issa Ponda  na wenzake 49  wana kesi ya kujibu.

Sambamba na kuwaona washitakiwa wote  wana kesi,Hakimu Mkazi Victoria Nongwa pia ameamuru  Ponda na  wenzake wapande kimbani na kuanza kujitetea kuanzia kesho na keshokutwa.

Uamuzi huo ambao ulikuwa ukisubiri kwa shahuku kubwa, ulitolewa jana  saa 5:24 asubuhi na Hakimu Nongwa ambapo hakimu huyo alianza kuikumbusha mahakama kuwa washitakiwa wote wanakabiliwa na  kosa la kula njama kutenda kosa, kuingia kwa jinai katika kiwanja cha Chang’ombe Markas, kujimilikisha kiwanja hicho kwa jinai, wizi wa malighafi zenye thamani ya Sh.milioni 59  na kosa la tano ni uchochezi ambalo linamkabili Ponda na mshitakiwa wa tano (Mukadamu Abdallah).

Hakimu Nongwa alisema kabla ya kuanza kuandika uamuzi wake alipitia ushahidi wa 17 na vielelezo 13 vilivyowasilishwa na upande wa jamhuri unaotetewa na wakili Mwandamizi wa Serikali, Tumaini Kweka , mahakama imeuchambua ushahidi huo na kuona kuna mashahidi ambao ni viongozi wa Bakwata  walitoa ushahidi ulioonyesha kuwa kiwanja cha Chang’ombe Markas zamani kilikuwa ni mali ya Bakwata lakini Bakwata ikaamua kubadilishana kiwanja hicho na Kampuni ya Agritanza Ltd.

Hakimu Nongwa alisema pia ushahidi ulitolewa na upande wa Jamhuri unaonyesha Bakwata ipo chini ya waumini wa dini ya Kiislamu wote nchini,  na kwamba kuna baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu hawakuridhishwa na uamuzi wa Bakwata kuamishia umiliki wa kiwanja hicho kwa kampuni ya Agritanza Ltd.
Hakimu huyo akichambua hoja za wakili wa utetezi, Nassor Juma na Njama alizowasilisha Februali 28 mwaka huu, zilizoomba mahakama hiyo iwaone washitakiwa hawana kesi ya kujibu kwa sababu kesi inayowakabili si ya jinai ni ya madai ambayo inahusu mgogoro wa ardhi ambao ilipaswa ikasikilizwe katika Mahakama ya Ardhi na siyo Mahakama ya Kisutu.

“Kwanza kabisa mahakama hii inapenda kuweka wazi kuwa haina mamlaka ya kusikiliza kesi za migogoro ya Ardhi ….na ieleweke wazi kuwa mahakama hii haijamzuia mtu yoyote anajiona ana maslahi katika uuzwaji wa kiwanja hicho kwenda katika Mahakama ya Ardhi kufungua kesi ya kupingwa uuzwaji wa kiwanja hicho na pia mahakama yangu haiwezi kuzungumzia kesi za ardhi….na hoja hiyo ya wakili Nassor naifananisha  mfano baba anaamua kuuza ardhi  halafu wake wanakuwa hawajaridhika na uamuzi huo , watoto wanaweza kwenda kufungua kesi mahakama ya ardhi kupinga uamuzi huo wa baba yao….kwa kwa kifupi tu mahakama hii inasema hivi kesi hii ni ya jinai na mahakama hii ina mamlaka ya kuisikiliza”alisema Hakimu Nongwa.

Hakimu Nongwa alisema kwa mujibu wa kielelezo cha nne, tano, 11,13  ni maelezo ya onyo yaliyotolewa na baadhi ya washitakiwa wakati wakihoji wa polisi, na ndani ya maelezo hayo ambayo yalipokelewa kama vielelezo na mahakama hiyo yaonyesha washitakiwa hawakuridhishwa na uamuzi wa Bakwata wa kuibadilishana ardhi ile na kampuni ya Agritanza na ndiyo maana washitakiwa hao wakaamua kwenda kuweka kambi tangu Oktoba 12-17 mwaka jana, katika kiwanja hicho kwa lengo la kukikomboa kiwanja hicho ambacho washitakiwa wanadai ni mali ya waislamu ambacho kimeporwa na kwamba aliyekipora ndiye ataenda mahakamani.

“Licha ya wakili wa washitakiwa Nassor katika majumuisho yake alizama ndani kabisa hadi kufikia hatua ya kusema ushahidi wa jamhuri hauna uzito wowote,mahakama hii inaona katika hatua wakili huyo hakupaswa kuingia ndani hadi kupima uzito wa ushahidi uliotolewa na upande wa jamhuri kwani tayari kuna ushahidi wa upande wa jamhuri unaonyesha washitakiwa 48 walikiri kukamatwa wakiwa ndani ya kiwanja hicho  isipokuwa wa Ponda na Mkadamu ambao hawakukumatwa katika eneo hilo.

“Na ieleweke wazi kila kesi ina mazingira yake na kesi hii tunaona kabisa kuna washitakiwa katika maelezo yao ya onyo walikiri kukamatwa katika eneo hilo…sasa mahakama hii imefikia uamuzi kuona upande wa jamhuri umeweza kujenga kesi yao na hivyo imewaona washitakiwa wote wana kesi ya kujibu ili washitakiwa hao wapate fursa ya kujitetea kwa kuileleza mahakama kuwa katika kiwanja siku hiyo wavyokamatwa walikuwa wakitafuta nini’ alisema Hakimu Nongwa.

Aidha alisema anaiarisha kesi hiyo hadi kesho na kesho kutwa ambapo washitakiwa hao wataanza kupanda kizimbani kujitetea.Kesi hii inasikilizwa chini ya ulinzi mkali wa vyombo vya ulinzi na usalama ambapo baadhi ya wanausalama uketi ndani ya ofisi ya mapokezi ya mahakama hiyo kwaajili ya kuwapokea wageni wote wanaingia mahakamani na kisha kuwapekua kwa kifaa maalum.

Kesi hiyo ya kwa mara ya kwanza ilifunguliwa mahakamani hapo Oktoba 18 mwaka jana  ambapo washitakiwa hao wanakabiliwa na makosa matano likiwemo kosa la kula njama kutenda kosa,kuingia kwa jinai, kujimilikisha eneo kwa njia ya jiani, wizi wa malighafi zenye thamani ya Sh.milioni 59 na uchochezi.

Wakati huo huo, Hakimu Mkuu Mkazi Ilvin Mugeta  aliarisha kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma inayomkabili Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Usafirishaji (UDA), Idd Simba na wenzake hadi Aprili 4,5 mwaka huu, kwasababu upande wa jamhuri hakuleta mashahidi kwaajili ya kuanza kuisikilizwa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Machi 5 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.