Header Ads

TAKUKURU ISIWATISHE WABUNGE

Na Happiness Katabazi

BABA wa Taifa, hayati Julius Nyerere, aliwahi kusema kwamba ‘ukweli una tabia moja nzuri sana. Haujali mkubwa wala mdogo , haujali adui wala rafiki’.


Kuwahoji wabunge wakati Bunge linangojea kupokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa serikali kuhusu maazimio ya Kamati Teule yaliyotokana na uchunguzi wa kashfa ya kampuni ya kufua umeme ya Richmond ni ufisadi wa kupindukia.

Katika malumbano kati ya wabunge na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), taasisi hiyo imeungwa mkono na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kujaribu kuwahoji wabunge eti kuhusu sakata la kupokea posho mbilimbili.

Ukweli umeibuka kwamba zipo njama za kulizuia Bunge lisiwe na msimamo wa kuikataa taarifa itakayotolewa na serikali kuhusu utekelezaji wa maazimio ya Bunge kuhusu kashfa ya mkataba wa kampuni ya mfukoni ya Richmond.

Ni kweli kwamba katika ripoti aliyoiwasilisha aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge kuchunguza kashfa ya mkataba huyo, Dk. Harrison Mwakyembe, Februari mwaka jana, ilikubaliwa na kupitishwa na Bunge. Ndani ya ripoti hiyo liko pendekezo la kuwajibika kwa Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hosea.

Mtu huyo (Dk.Hosea) sasa amechukua jukumu la kutaka kuwahoji wabunge hasa Dk.Mwakyembe.

Ni zuzu gani asiyekuwa na hata chembe ya uelewa wa sheria za nchi hata ashindwe kugundua kwamba Takukuru inatumia vibaya mamlaka yake kulitisha Bunge kwa jambo ambalo halina maslahi kwa taifa letu?

Kama wabunge watakubali vitisho hivyo vya kitoto na wakashindwa kujadili kikamilifu taarifa ya serikali kuhusu utekelezaji wa maazimio ya Bunge kuhusu Richmond, hapo itakapowasilishwa ili kuifurahisha Takukuru, hilo litakuwa ni janga la kitaifa na vita dhidi ya ufisadi vitakuwa vimeshindwa na mafisadi wanaweza kushangilia kwa nderemo na vifijo na kugonganisha glasi za mvinyo!

Sheria ya rushwa haina kipengele chochote kinachozuia takrima na wala wabunge kupokea posho mbili, hivyo kupokea posho mbili si kuvunja sheria za nchi ambazo tumeridhia zituongoze.

Kumhoji mtu kwenye jambo ambalo halijakatazwa kisheria ni kumtisha, kumfunga mdomo, kumkera na kumdhalilisha na pia ni upotevu wa rasilimali za taifa.

Labda Takukuru pekee ndiyo isiyojua kwamba muda watakaoutumia kuwahoji wabunge kwa jambo la ajabuajabu na kuchekesha, unalipiwa na walipakodi hivyo ni hasara kwa taifa?

Waziri Mkuu alipojiingiza katika jambo hili kwa kuruhusu mahojiano hayo baina ya wabunge na Takukuru yafanyike, hakuzingatia kwamba taasisi inayohusika inatuhumiwa mbele ya Bunge kwa hiyo kuiruhusu iwahoji wabunge ni kutojua sheria na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

Tunasema tumechoka sasa kwani ni miaka miwili serikali inasuasua na kujikanyagakanyaga kutekeleza maazimio ya Bunge! Kuna nini ndani yake?

Ikiwa kikao hiki cha Bunge kitashindwa kuiwajibisha serikali na kulimaliza suala hilo, basi ni wajibu wa sisi wananchi kuiadhibu serikali na wabunge wake katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Kwa upande wa Takukuru ni wazi kuwa sasa taasisi hii imepoteza heshima yake kwa kuparamia baadhi ya mambo bila kufanya utafiti wa kina.

Imekuwa ikipeleka baadhi ya kesi mahakamani bila ya kuwa na ushahidi wa kutosha na inazingatia zaidi majungu na mizengwe ya kisiasa kuliko maslahi ya taifa.

Yawezekana kwamba baadhi ya viongozi wakuu wa taasisi hiyo hivi sasa ni sehemu ya ufisadi na ni wala rushwa, makuwadi siasa za uporaji wa rasilimali za wananchi.

Ndiyo maana sintashangaa wavuja jasho kuiita taasisi hiyo taasisi ya kuhamasisha rushwa na siyo kuzuia.

Nimalizie kwa kuwaasa wabunge kwamba katu wasikubali kuhojiwa na Takukuru kwa sababu hakuna sheria ya nchi yoyote waliyoivunja, na ninawataka Takukuru na wale wote ambao wanakerwa na wabunge kupata posho mbilimbili, waone wakati umefika sasa wa kuibana serikali ili ipeleke muswada bungeni ambao utazuia wabunge na wafanyakazi wa taasisi nyingine iwe kwenye sekta binafsi na serikalini kupokea posho mbili.

Sasa kama hilo tukishindwa kulifanya, tutabaki kubwatabwata na kubwabwaja mitaani na kwenye vyombo vya habari.

Ieleweke itakuwa ni sawa na kumvalisha mbu miwani. Wabunge waliopokea na wanaoendelea kupokea posho mbili hawajavunja sheria za nchi na Takukuru inalijua hilo vizuri tu ila kwa sababu imeamua kutumia vibaya taasisi yetu hiyo kwa maslahi ya watu wachache inaamua kufanya kama ifanyavyo.

Takukuru inataka kuwahoji wabunge ili kuwahamisha fikra wananchi na wabunge kuacha kufuatilia hoja kuu ya ufisadi inayosababisha umaskini wa kutupwa kwa wavuja jasho.

Nataka Takukuru na Waziri Mkuu Pinda mfahamu kwamba sisi baadhi ya wananchi na waandishi wa habari wenye misimamo thabiti na upeo wa kuona mbali, tunaofahamu vyema kusoma alama za nyakati ‘hatudanganyiki’! Hii imekula kwenu na si kwa wavuja jasho!

Mungu ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika

0716 774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Novemba 1, 2009

2 comments:

Anonymous said...

Dada happy watanzania walio wengi hawajui mamlaka ya kisheria walio nayo juu ya hiyo serikali yao. Kwakweli ulichokisema ni kweli tupu ya kwamba sisi waajili wa hii serikali ya awamu hii tunawajibu mmoja tu wa kuiwajibisha kwa kutotufanyia kazi tulizokubaliana watufanyie. Nadhani ipo haja kubwa ya kutoa elimu ya bure kwa kila mtanzania juu ya somo la NGUVU YA UMA na MAMLAKA YA UMMA.

Anonymous said...

Dada happy watanzania walio wengi hawajui mamlaka ya kisheria walio nayo juu ya hiyo serikali yao. Kwakweli ulichokisema ni kweli tupu ya kwamba sisi waajili wa hii serikali ya awamu hii tunawajibu mmoja tu wa kuiwajibisha kwa kutotufanyia kazi tulizokubaliana watufanyie. Nadhani ipo haja kubwa ya kutoa elimu ya bure kwa kila mtanzania juu ya somo la NGUVU YA UMA na MAMLAKA YA UMMA.

Powered by Blogger.