Header Ads

MWANZO,MWISHO WA KESI YA LIYUMBA

Na Happiness Katabazi

JANA Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Eliezer Feleshi, iliandika historia nyingine ya kushinda baadhi ya kesi za jinai inazozifungua katika mahakama mbalimbali nchini.


Historia hiyo ambayo ni dhahiri imeleta faraja kwenye ofisi hiyo ya DPP ambayo hivi karibuni imekuwa ikisakamwa vikali na jamii kwamba imekuwa haifanyi vyema katika baadhi ya kesi, ni kwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kumhukumu kwenda jela miaka miwili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu (BoT), Amatusi Liyumba (62) aliyekuwa akikabiliwa na kosa la matumizi mabaya ya ofisi ya umma baada ya kumkuta na hatia.

Liyumba alikuwa anatetewa na mawakili wa kujitegemea; Majura Magafu, Jaji Mstaafu Hillar Mkate, Onesmo Kyauke na Hudson Ndusyepo.
Kesi hii imekuwa ikivuta hisia za watu wengi wa kada tofauti.
Ufuatao ni mtiririko mzima wa kesi hii tangu ilipofunguliwa hadi jana ilipomalizika kwa kutolewa hukumu.

Januari 27, 2009:
Liyumba na Kweka walifikishwa kwa mara ya kwanza saa nane mchana mbele ya Hakimu Mkazi Hadija Msongo wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, na kusomewa hati ya mashtaka Na.27/2009. Shitaka la kwanza lilikuwa ni matumuzi mabaya ya ofisi ya umma baada ya kufanya upanuzi wa mradi wa ujenzi wa jengo la minara pacha la Benki Kuu (BoT) bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa benki hiyo na shtaka la pili ni la kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221.

Hata hivyo, Hakimu Msongo alisema ili washtakiwa wapate dhamna ni lazima kila mmoja atoe fedha taslimu au hati ya mali yenye thamani ya sh bilioni 55, kutotoka nje ya Jiji la Dar es Salaam bila kibali cha mahakama na kuwasilisha hati ya kusafiria mahakamani. Walishindwa kutimiza masharti hayo.

Februari 17, 2009:
Hakimu Mkazi Msongo alimpatia dhamana iliyozua utata Liyumba peke yake ambaye aliwasilisha hati ya kusafiria iliyoisha muda wake, hati ya nyumba yenye thamani ya sh milioni 800, kinyume kabisa na masharti aliyoyatoa Januari 27. Liyumba alitoka gerezani na kurudi nyumbani kwake huku Kweka akiendelea kusota rumande kwa kushindwa kutumiza masharti ya dhamana.

Februari 20, 2009:
Hakimu Mkazi Msongo, saa nane mchana aliwaita kwa dharura wadhamini wawili wa Liyumba na kuwaeleza kuwa ameifuta dhamana ya mshtakiwa baada ya kubaini kuna dosari, na akatangaza kuufuta uamuzi wake wa kumpatia dhamana. Hata hivyo siku hiyo Liyumba hakuwepo mahakamani kwani haikuwa tarehe ya kesi yake. Hali hiyo ilisababisha wananchi na vyombo vya habari kueneza uvumi kwamba mshitakiwa huyo ametoroka.

Machi 2, 2009: Mawakili wa Liyumba waliwasilisha kwa maandishi ombi mbele ya Hakimu Mkazi Msongo la kutaka mahakama hiyo itumie kifungu cha 225(1-4) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai 2002, kinachotamka kuwa, ndani ya siku 60, upelelezi kesi husika uwe umekamilika, vinginevyo ifutwe.

Machi 13, 2009:

Hakimu Mkazi Msongo aliamua kujitoa kwa madai kuwa mwenendo wa kesi hiyo umekuwa ukilalamikiwa na waendesha mashtaka na mawakili kupitia vyombo vya habari.

Machi 20, 2009:
Uongozi wa Mahakama ya Kisutu ulimpangia Hakimu Mkazi, Waliarwande Lema kusikiliza kesi hiyo ikiwa ni siku chache baada ya hakimu Msongo kujiondoa.

Machi 30, 2009:
Hakimu Mkazi Lema alianza kuiendesha kesi hiyo.

Aprili 2, 2009:
Hakimu Mkazi Lema alisikiliza ombi lililowasilishwa na wakili wa utetezi, Majura Magafu lililoomba mahakama iifute kesi hiyo kwa sababu siku 60 zimepita na jamhuri haijakamilisha upelelezi wa kesi hiyo.

Aprili 23, 2009:
Hakimu Mkazi Lema alitoa uamuzi wa ombi hilo. Alisema baada ya kupitia hoja za mawakili wa pande zote mbili, amebaini kuwa licha ya siku 60 kupita na ni kweli upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika, haoni kama haki za msingi za washtakiwa zimevunjwa, hivyo akatupilia mbali ombi hilo.

Mei 27, 2009:
Hakimu Lema aliwafutia kesi Liyumba na Kweka baada ya kukubaliana na ombi la mawakili wao kwamba hati ya mashtaka ina dosari za kisheria. Lakini wakati wakifurahia uamuzi huo, walikamatwa tena na makachero wa polisi waliofurika mahakamani hapo, muda mfupi baada ya kuachiwa na kupelekwa katika kituo cha polisi Salender.

Mei 28, 2009:
Saa nane mchana Liyumba alikifishwa peke yake mahakamani hapo na kusomewa hati mpya ya mashtaka na wakili wa serikali, Prosper Mwangamila aliyekuwa anasaidiana na Wakili Kiongozi Justus Mulokozi na John Wabuhanga mbele ya Hakimu Mkazi Nyigumalila Mwaseba ambapo alidai mshtakiwa anakabiliwa na mashtaka mawili ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221.

Mei 29, 2009:
Hakimu Mwaseba alitoa uamuzi wa kulegeza masharti ya dhamana kwa Liyumba. Alisema ili apate dhamana atatakiwa atoe fedha taslimu au hati ya mali yenye thamani ya sh milioni 300, wadhamini wawili watakaosaini bondi ya sh milioni 50 kila mmoja, kutotoka nje ya Jiji la Dar es Salaam hadi kwa kibali maalum na kusalimisha hati ya kusafiria mahakamani.

Masharti hayo ni tofauti na awali, ambapo masharti ya dhamana yake yaliangukia chini ya kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, ambayo yanamtaka mshtakiwa atoe nusu ya fedha au hati ya mali yenye thamani ya sh bilioni 110. Upande wa jamhuri haukurizika na uamuzi huo, wakakata rufaa Mahakama Kuu.

Juni 1, 2009:
Jaji Geofrey Shaidi alisikiliza ombi la kupinga kulegezewa masharti dhamana kwa Liyumba lililowasilishwa mbele yake na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Eliezer Feleshi, ambapo kwa mujibu wa ombi hilo, DPP alipinga masharti ya dhamana yaliyotolewa na Mahakama ya Kisutu.

Juni 15, 2009:
Jaji Shaidi alitoa uamuzi kuhusu ombi hilo la DPP na akasema anakubaliana nalo. Akaamuru kuwa mshtakiwa anapaswa apewe dhamana, akatakiwa atoe fedha au hati ya sh bilioni 110. Na akaamuru jalada la kesi hiyo lirudishwe Mahakama ya Kisutu na apangiwe hakimu mwingine. Liyumba alishindwa kutimiza masharti hayo ya dhamana hivyo kulazimika kusota jela hadi jana.

Julai 28, 2009:
Uongozi wa Mahakama ya Kisutu ulimpanga hakimu Eva Nkya kuendelea na kesi hiyo huku ikisuburi Jaji Mkuu Agustino Ramadhani aipangie jopo la mahakimu wakazi kwa ajili ya kuanza kuisikiliza kesi hiyo, na wakili kiongozi wa serikali, Justus Mulokozi aliiambia mahakama kuwa upelelezi umekamilika.

Agosti 25, 2009:
Hakimu Mkazi Nkya alisema jaji mkuu tayari ameishapanga jopo la mahakimu wakazi kwa ajili ya kusikiliza kesi hiyo na kwamba litaongozwa na Mkasimongwa atakayesaidiwa na Mlacha na Mwingwa.

Septemba 7, 2009:
Kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya upande wa jamhuri kumsomea maelezo ya awali mshtakiwa, lakini hata hivyo siku hiyo hakuweza kufika mahakamani kwani alikuwa akiugua gerezani, hivyo usikilizwaji wa awali uliahirishwa.

Septemba 25, 2009: Wakili wa serikali, Mulokozi mbele ya jopo hilo, alimsomea maelezo ya awali mshtakiwa.

Oktoba 1, 2009:
Upande wa jamhuri ulianika orodha ya mashahidi wake 15 na kwamba unakusudia kuleta vielelezo 13.

Oktoba 19, 2009:
Kesi ilikuja kwa ajili ya kuanza kusikilizwa mfululizo hadi Oktoba 23, lakini siku hiyo haikuweza kusikilizwa kwa sababu shahidi wa kwanza wa upande wa mashtaka hakuweza kutokea mahakamani kwa sababu ni mgonjwa, hivyo ikaahirishwa.

Oktoba 22, 2009:
Shahidi wa kwanza ambaye ni mchunguzi kutoka Takukuru, Seif Mohamed (50), aliiambia mahakama kuwa mabadiliko ya upanuzi wa ujenzi wa Minara Pacha (Twin Tower), yaliidhinishwa na Bodi ya Wakurugenzi wa BoT.

Oktoba 23, 2009:
Shahidi wa pili ambaye ni Meneja wa Masuala ya Bodi ya Wakurugenzi wa BoT, Justo Tongola (46), alieleza kuwa hajawahi kuona wala kusikia bodi hiyo ikilalamikia utendaji kazi wa Liyumba.

Novemba 18, 2009:
Shahidi wa tatu ambaye ni Mkurugenzi wa Fedha BoT, Ruta Angelo (50), aliiambia mahakama kuwa mshtakiwa huyo hakuwa na uamuzi wa mwisho katika mradi wa ujenzi huo.

Novemba 24, 2009:
Shahidi wa tano ambaye ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na mjumbe wa bodi ya BoT, Dk. Natu Mwamba (49), alidai kuwa hana kumbukumbu ya idadi ya maombi na kiasi cha fedha za nyongeza kilichokuwa kikiletwa na menejimenti kwenye bodi ya wakurugenzi ili ipatikane idhini.

Novemba 26, 2009:
Shahidi wa saba ambaye ni mkadiriaji wa gharama za majengo, Harold Herbert Webb (78), aliiambia mahakama kuwa hapakuwepo na hasara katika ujenzi wa majengo hayo.
Webb ambaye ni raia wa Uingereza, alidai hapakuwepo hasara yoyote licha ya kuwapo kwa mabadiliko ya ujenzi na kiasi cha fedha kuongezeka kutoka dola dola 357 hadi dola milioni 756. Kiasi chote hicho kilitumika kwenye mradi wa ujenzi huo.

Januari 26, 2010:
Shahidi wa nane ambaye ni Naibu Gavana wa BoT, Juma Reli (54), alisema ameshindwa kuithibitishia mahakama kuhusu hasara iliyopatikana katika mradi huo kwa sababu hadi sasa ripoti ya mwisho ya matumuzi ya fedha za mradi huo haijakamilika. Sambamba na hilo, katika hali isiyotarajiwa, upande wa mashtaka ulisema unakusudia kupunguza idadi ya mashahidi wake kutoka 15.

Machi 15, 2010:
Kesi ilikuja kwa ajili ya mashahidi wa upande wa jamhuri kuendelea kutoa ushahidi, lakini katika hali iliyoshtusha waudhuriaji wa kesi hiyo, Wakili mwandamizi wa serikali, Juma Mzarau aliiambia mahakama kuwa baada ya wao kupitia kwa kina nakala ya mwenendo wa kesi hiyo, ulionyesha ni mashahidi wanane waliotoa ushahidi na vielelezo 13 vilitolewa mahakamani hapo na wamefikia hatua muafaka ya kuifunga kesi yao kwa mujibu wa kifungu cha 231 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002.

Ombi hilo la kuifunga kesi yao lilikubaliwa na mahakama, na Kiongozi wa jopo, Mkasimongwa akatoa amri kwa upande wa utetezi ulete majumuisho yake kwa njia ya maandishi mahakamani Machi 22, upande wa jamhuri nao uwasilishe ya kwao Machi 29, na Aprili 9 mwaka huu, mahakama hiyo itatoa uamuzi wa mshtakiwa huyo ana kesi ya kujibu au la.

Machi 22, 2010:
Mawakili wa Liyumba waliwasilisha majumuisho yao kwa maandishi na wakaiomba mahakama imuone mteja wao hana kesi ya kujibu na imuachilie huru kwa sababu upande wa mashtaka umeshindwa kuthibitisha kesi yao.

Machi 29, 2010:
Mawakili wa upande wa jamhuri waliwasilisha majumuisho saa 9:21 alasiri na waliomba mahakama imuone mshtakiwa ana kesi ya kujibu kwa sababu wameweza kuithibitisha kesi yao.

Aprili 9, 2010:
Kiongozi wa jopo, Mkasimongwa kwa niaba ya wenzake alitoa uamuzi wa majumuisho hayo na alimfutia shtaka la pili ambalo ni la kusababisha hasara, na mahakama ikamuona Liyumba ana kesi ya kujibu katika shtaka la kwanza ambalo ni la matumuzi mabaya ya ofisi ya umma.

Aprili 16, 2010:
Mawakili wa Liyumba waliwasilisha mahakamani majina ya mashahidi watano wanaokusudia kuja kumtetea mshtakiwa.

Aprili 22, 2010:
Liyumba alitoa utetezi wake na akadai kuwa serikali haijui itendalo dhidi ya kesi iliyomfungulia. Na akaiomba mahakama izingatie ukweli wakati wa kutoa hukumu dhidi yake Mei 24 (jana) badala ya kuwasikiliza watu wasiojua watendalo.
Maneno hayo mawili ‘hawajui watendalo’ yanafanana na yale aliyotumia Yesu Kristo, anayeaminika kuwa ni mwokozi wa waumini wa Kikristo wakati akieleza kitendo cha Wayahudi waliokuwa wakimsulubisha (Luka 23:34).

Alipomaliza kujitetea alipanda kizimbani shahidi wake ambaye alikuwa Kaimu Katibu wa BoT na Katibu wa Bodi ya benki hiyo ambaye ni mwanasheria kitaaluma, Bosco Kimela (52), aliyeieleza mahakama kuwa shtaka linalomkabili Liyumba hastahili kushtakiwa nalo kwani hajalitenda. Na wakili Magafu akasema kutokana na ushahidi wa mashahidi hao wawili, upande wa utetezi unafunga kesi hiyo.

Hivyo hakimu Mkazi Mkasimongwa akaamuru pande zote mbili Mei 7 mwaka huu, zilete kwa njia ya maandishi majumuisho yao ya kuiomba mahakama imuone mshtakiwa ana hatia au la. Lakini hata hivyo tarehe hiyo ilipofika na kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kutajwa wakili wa serikali Ponsian Lukosi alimweleza hakimu mkazi Mkasimongwa kwamba jamhuri imeshindwa kuwasilisha majumuisho yake kwa sababu mahakama haijawapatia mwenendo wa kesi hiyo na hakimu huyo alikubaliana na ombi hilo na kuziongezea pande zote mbili muda ambapo aliziamuru ifikapo Mei 13, mwaka huu, ziwasilishe majumusho hayo.

Mei 13, 2010:
Wakili wa utetezi Onesmo Kyauke aliwasilisha majumuisho yao upande wa utetezi, ambapo waliomba mahakama imuone mshtakiwa hana hatia kwa sababu hakuwa na mamlaka ya kuamua jambo lolote lile katika mradi wa majengo pacha.
Hata hivyo, waandishi wa habari za mahakama kwa jitihada walizozifanya kwa siku mbili mfululizo za kuhakikisha wanapata nakala ya majumuisho ya upande wa jamhuri, hazikuzaa matunda baada ya kukosa ushirikiano kutoka kwa mawakili hao wa upande wa mashtaka ambao wakati kesi hiyo inaendelea mahakamani walikuwa wakitaka ushirikiano na waandishi wa habari za mahakama.

Mei 24, 2010:
Mahakama ya Kisuti ilimtia hatiani Liyumba kwa kosa hilo na kumhukumu kwenda jela miaka miwili.

0716 774494
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Mei 25 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.