Header Ads

HAKIMU AKWAMISHA KESI YA LIYUMBA

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa Jamhuri katika kesi ya kukutwa na simu gerezani inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba jana ulishindwa kumsomea maelezo ya awali mshtakiwa huyo kwa sababu hakimu mkazi Stewart Sanga anayesikiliza kesi yake kutokuwepo mahakamani hapo.


Wakili wa Serikali Elizabeth Kaganda alimweleza Hakimu Mkazi Aloyce Katemana kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya wao kumsomea maelezo ya awali mshtakiwa huyo na mawakili wa utetezi kuwasilisha hoja za pingamizi lao lakini akaomba kesi hiyo iairishwe kwasababu hakimu anayesikiliza kesi hiyo hajafika mahakamani hapo.

Hoja hiyo ilikubaliwa na mawakili wa utetezi Hudson Ndusyepo, Onesmo Kyauke na Majura Magafu pamoja na Hakimu Katemana ambaye aliairisha kesi hiyo hadi Desemba mbili mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya Jamhuri kumsomea maelezo ya awali.

Awali Septemba 8 mwaka huu, Liyumba alifikishwa mahakamani hapo akikabiliwa na kesi hiyo mpya ya kukutwa na simu akiwa katika gereza la Ukonga wakati akitumikia adhabu ya kifungo cha miaka miwili jela baada ya Mei 25 mwaka jana, mahakama hiyo kumtia hatiani kwa kosa la matumuzi mabaya ya ofisi ya umma.Septemba 23 mwaka huu, alitoka gerezani baada ya kumaliza kutimikia kifungo hicho.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Oktoba 29 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.