Header Ads

TANESCO IMEVUNA ILICHOPANDA DOWANS

Na Happiness Katabazi
SEPTEMBA 28 mwaka huu,Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Emilian Mushi alitoa hukumu ya kihistoria ambayo ilikata ngebe ya vizabinazabina ambao ni baadhi ya wanasiasa na wanaharakati waliokuwa wakifanya harakati za kulizuia Shirika la Ugavi wa Umeme (TANESCO), kulipa tuzo ya mabilioni ya shilingi kwa Kampuni ya kufua umeme, Dowans Tanzania.


Tuzo hiyo ya dola za Marekani milioni 65 (takriban sh bilioni 94) iliyotolewa Novemba 15, mwaka jana (2010); na Januari 25, mwaka huu, Dowans iliwasilisha ombi lake la kutaka Mahakama Kuu ya Tanzania iisajili tuzo waliyopewa na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa migogoro ya Kibiashara (ICC).

ICC iliitia hatiani TANESCO kwa kosa la kuvunja mkataba na Dowans iliyokuwa ikitetewa na wakili wa kimataifa Kennedy Fungamtama, na ikaiamuru iilipe tuzo hiyo na riba ya asilimia 7.5.

Lakini wanaharakati kadhaa na wanasiasa hapa nchini wamekuwa wakipinga uamuzi huo wa ICC mahakamani.Jaji Mushi alisema Mahakamu Kuu ya Tanzania haina mamlaka ya kutengua hukumu ya ICC.

Hatua hiyo ya wanasiasa na wanaharakati kuchelewesha malipo ya tuzo hiyo itaifanya TANESCO kulipa kiasi kikubwa zaidi kwani riba imekuwa inaongezeka. Hadi siku hukumu inatolewa na Jaji Mushi Dowans ilikuwa inastahili kulipwa na Tanesco Sh bilioni 113 badala ya sh bilioni 94 kutokana na ucheleweshwaji huo.

Jaji Mushi alianza kwa kusema maneno yafuatayo:

“Kwanza, naishukuru TANESCO na zile taasisi nne za wanaharakati waliokuwa wakiongozwa na LHRC; walijitokeza mahakamani hapa kupinga tuzo ya Dowans isisajiliwe na kutumia muda wao kuchambua kesi mbalimbali na kuandaa mapingamizi yao, ambayo hata hivyo niliyatupilia mbali.

“Pili, nafahamu fika kuwa kesi hii ya Dowans ina sayansi nyingi sana za kisiasa, hivyo napenda niwafahamishe mapema kabisa kabla ya kuendelea kuwa hukumu yangu nitakayotoa leo haijatoa nafasi kwa sayansi hizo za kisiasa, kwa sababu imezingatia misingi ya sheria na haki.”
Jaji Mushi alisema baada ya kuipitia hukumu ya ICC amebaini kuwa haina makosa ya kisheria kama anavyodai mlalamikaji, na ndani ya hukumu hiyo alikuta kiambatanisho ambacho ni mkataba kati ya TANESCO na Dowans uliosainiwa Juni 23, mwaka 2006; na kufafanua kwamba pande zote mbili katika mkataba huo zilikubaliana kwamba uamuzi wa ICC ndiyo utakuwa wa mwisho, na utazibana pande zote mbili na hautaweza kukatiwa rufaa.

Jaji huyo alisema kifungu cha 14 (f) cha mkataba huo kinasomeka hivi: “The parties waive any right to challenge or contest the validity or enforceability of this arbitration agreement or any arbitration proceeding or award brought in conformity with this section.” Kwa tafsiri nyepesi, Fungamtama alisema kifungu hicho kinasema, TANESCO na Dowans katika mkataba wao walikubaliana kwa maandishi kuweka kando haki za kupinga au kuhoji mwenendo na tuzo zitakazotolewa na baraza la usuluhishi.

Jaji akasema: “Sasa kwa mujibu wa mkataba huo ni wazi kuwa TANESCO na Dowans walikubaliana kuwa endapo utatokea mgogoro baina yao utapaswa upelekwe ICC tu na ICC itakapotoa hukumu ya mgogoro baina yao, pande hizo mbili hazitakuwa na mamlaka ya kuikatia rufaa hukumu hiyo ya ICC.

“Kwa makubaliano hayo ya pande hizo mbili ndani ya mkataba huo wa POA ambao TANESCO hadi wanakwenda kujitetea ICC hawakuwa wameuvunja huo mkataba wa POA na kupitia mkataba huo ICC pia iliutumia kutolea uamuzi wake…ni wazi kabisa mahakama hii inakubaliana na hukumu ya ICC kuwa ilikuwa ni hukumu ya haki na iliyofuata sheria na ilizingatia pia masilahi ya sera za Tanzania na kwakuwa pande hizo zilikubaliana hukumu ya ICC hawataweza kuikatia rufaa basi ndivyo hivyo hivyo mahakama hii ya Tanzania haiwezi kutoa uamuzi wa kutengua hukumu hiyo iliyotolewa na ICC.”alisema Jaji Mushi.

Alisema anakubaliana na hoja ya wakili wa Dowans, Fungamtama, kuwa kifungu cha 3 cha jedwali la 3 katika Sheria ya Usuluhishi ya Tanzania, Sura ya 15 ya mwaka 2002 ambacho kinasomeka hivi: Kwa tafsiri rahisi, kifungu hicho utaona tayari nchi imejifunga mikono na utekelezaji wa hukumu zinazotolewa na mahakama za kimataifa kwa sababu ni nchi yetu yenyewe imeridhia sheria na mikataba ya kimataifa.

Jaji Mushi alisema kitendo cha TANESCO kuwasilisha ombi mbele yake likidai kuwa Mahakama Kuu haina mamlaka ya kusajili tuzo hiyo, halina ukweli na kwamba mwanasheria aliyefahamu vema Sheria ya Usuluhishi ya Tanzania ya mwaka 2002 Sura ya 15, Mikataba ya Kimataifa na Sheria ya Makosa ya Madai ya mwaka 2002 ataona wazi kuwa Mahakama Kuu ya Tanzania imepewa mamlaka ya kusajili tuzo hapa nchini zinazotolewa na Mahakama za Kimataifa.

Jaji alisema hoja ya TANESCO kuwa mwenendo wa hukumu ya ICC ulikuwa na mapungufu ya kisheria, haikupaswa kupelekwa mbele yake kwani Tanasco walikuwa ni wadaiwa katika kesi iliyofunguliwa ICC na walipaswa kuiwasilisha hoja hiyo ICC kabla ya mahakama hiyo ya kimataifa kutoa hukumu yake na kuikumbusha TANESCO kuwa ni yenyewe iliyoingia mkataba wa POA na Dowans ambao kwa ridhaa yao waliridhia kuwa hukumu itakayotolewa na ICC haitakatiwa rufaa.

Kutokana na makubaliano ya pande hizo mbili, Jaji Mushi aliishangaa TANESCO kwa hatua yake ya kuwasilisha hoja hiyo ambayo ni wazi ilipaswa iwasilishwe kwenye mashauri ambayo yamekatiwa rufaa na kwamba shauri lilokuwa mbele yake halikuwa shauri la rufaa.

Aidha Jaji Mushi alihitimisha kwa kusema kuwa anakubali ombi la Dowans la kusajili tuzo waliyopewa na ICC isajiliwe na mahakama ya Tanzania. Pia aliiamuru TANESCO kulipa gharama zote za uendeshaji wa kesi hiyo, na Dowans ianze taratibu za kukazia hukumu ya Mahakama ya ICC.

Awali ya yote napenda kutoa pongezi zangu za dhati kwa Mahakama Kuu ya Tanzania kupitia Jaji Mushi, kwani kupitia hukumu ya kesi hiyo kudhiirisha wazi bado tuna majaji majasiri ambao hawayumbishwi na makelele ya wanasiasa wahuni ambao walikuwa wakifikiri kupitia nyadhifa zao wangeweza kuiweka mfukoni mhimili huo wa mahakama ili uweze kutoa uamuzi wanaotuka wao katika kesi hiyo ya Dowans dhidi ya Tanesco.Hongera sana Jaji Mushi.

Napenda wasomaji wa makala hii wafahamu kuwa mimi nilikuwa ni miongoni mwa waandishi wa habari wa chache hapa nchini tuliyoifuatilia kwa karibu kesi hiyo kabla haijafunguliwa, ilipofunguliwa, ilipokuwa ikiendeshwa na hadi hukumu ilipotolewa Alhamisi wiki hii.

Nakumbuka baada ya kufikishwa kwa hukumu ya ICC katika Mahakakama Kuu ya Tanzania, waandishi wa habari za mahakama tulikuwa tunapata wakati mgumu wa kupata ufafanuzi wa jinsi ya ombi hilo la kusajiliwa kwa tuzo lakini mwisho wa siku kwa busara ya uongozi wa mahakama ulitenga utaratibu uliotuwezesha sisi kuwa tunapata habari kuhusu kesi hiyo.Tunashukuru kwa hilo.

Sasa basi kwa muktadha huo hapo juu wa baadhi ya maneno yaliyopo kwenye hukumu hiyo, sote tutakubaliana na Jaji Mushi kuwa kesi hiyo ilikuwa imegubikwa na siasa zilizokuwa zikiendeshwa na baadhi ya wanasiasa manyang’au, wakorofi ambao wanafahamu fika nchi yetu inafuata sheria lakini kwa makusudi wakaamua kutumia nyadhifa zao kuamasisha umma ushiriki katika mzozo huo wa Tuzo ya Dowans isisajiliwe eti kusajiliwa kwa Dowans ni ufisadi mkubwa.

Kwa maneno machache hayo hapo juu ambayo yanapatikana kwenye hukumu ya Jaji Mushi, binafsi nampongeza Jaji Mushi kwa ujasiri wake wa kutoa hukumu hiyo ambayo nyuma ya kesi hiyo ilikuwa imegukibwa na magomvi ya siasa chafu hasa za wanasiasa wa CCM na baadhi ya taasisi za wanaharakati ambao hata nakala ya ICC na mkataba wa POA naimani hawakuzisoma kwa makini na kujua ziliandikwa nini kwani wangekuwa wamesoma, katu wasingekuwa wanabwatuka na kwenda kuipinga Tuzo ya Dowans mahakamani.

Hivyo basi utekelezwaji wa hukumu hiyo itatekelezwa kwa kuchukuliwa kodi za wananchi wa Tanzania na kisha kuilipa Dowans. Lakini chanzo cha uwendawazimu wote ni makundi yanayohasimiana ndani ya CCM ambayo yalifanikiwa kuuteka umma wa Tanzania uwange mkono katika harakati zao za kuikashfu kampuni Richmond na Dowans na kweli harakati zao zilifanikiwa kwani taifa likajikuta linaingia kwenye malumbano makali kuhusu kulipwa kwa kampuni hiyo.

Kumbe nyuma ya pazia ya wanasiasa hao wa CCM ilikuwa ni chuki zao za kibiashara na siasa ambazo pia zinadaiwa ndizo zilizoisukuma Tanesco kuyumba kitaaluma na kimaamuzi na matokeo yake ikajikuta inavunja mkataba na Dowans kwaajili ya kelele hizo za wanasiasa manyang’au.

Kwahiyo hapa hoja ya Tanesco haiwezi kulipa kiasi hicho cha fedha haina msingi wowote ,kwani kushindwa kwao kusimamia maslahi ya taifa matokeo yake ikajikuta inafanya kazi na kutoa maamuzi kwaajili ya kuwafurahisha wanasiasa manyang’au ndiko kulikosababisha leo hii fedha za walipa kodi zitumike kuilipa dowans?

Inakuwaje ni Tanesco ndiyo ilikuwa ya kwanza kuvunja mkataba halafu ikashtakiwa na hukumu ilivyotolewa ndiyo ikurupuke kutoa maneno matamu ya kuhadaa umma kuwa kulipwa kwa fedha hizo kutaifanya Tanesco ifilisike?Tuiulize Tanesco wakati ikitenda kosa hilo la kuvunja ule mkataba kwa mashiniko ya kisiasa mwisho wa siku ilitegemea Dowans iwafanye nini kama siyo kuwashtaki?

Ieleweke wazi Tanzania ni nchi inayoendeshwa kwa misingi ya sheria na kila siku Jaji Mkuu Mstaafu Agustino Ramadhani amekuwa akisema haki ni gharama.Kwahiyo katika hili Tanzania hatuna budi kugharimika kwa kuilipa Dowans kiasi hicho mabilioni ya shilingi.

Na nipende kutoa taadhari kwa Tanesco ule mkataba waliousaini wa POA na Dowans na kitendo chao cha kuvunja mkataba na Dowans kabla ya muda, kuendesha mambo hayo kwa matakwa ya kelele za wanasiasa manyang’au ndiko kuliko tukifisha leo hii.

Lakini Tanesco wanawafanya Watanzania wote ni mazuzu wasioshindwa kung’amua kuwa matendo hayo waliyoyatenda hapo na hatua yake ya kuwakodi mawakili wa kujitegemea toka kampuni ya FK Chamber, Rex Attoney kulitetea shirika katika Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro(ICC), Mahakama Kuu ya Tanzania, kunaendelea kuteketeza fedha za walipa kodi kwa kisingizo cha kutoa fedha za umma kuwalipa mawakili hao wa kujitegemea wakati mawakili wa serikali tena wazuri tu wapo.

Kwa sisi tunaowafahamu hulka na tabia za mawakili wengi wa kujitegemea ,cha kwanza wanapenda fedha toka kwa mteja wao na uwa wanatabia za kama za matapeli za kuwahada wateja wao kuwa nilazima watashinda kesi inayomkabili mteja wake huku akijua wazi na akikaa pembeni ya watu wa mbali na mteja huyo anasema kesi inayomkabili mteja wake ni ngumu na watashindwa ila anachokifanya ni kuchukua fedha na kumfariji mteja wake kuwa atashinda.

Kwa hiyo Idara ya Usalama wa Taifa(TISS), iamke usingizi na kuwatumia hata wanasheria wake kuzisoma hizo nakala za hukumu za ICC na mahakama kuu ya Tanzania na ule mkataba wa POA na pia iwachunguze hao mawakili wakujitegemea waliopewa tenda ya kuitetea Tanesco tangu ICC, Mahakama Kuu na aliyewapa tenda hiyo, wanatumia taaluma zao kikweli kweli au wapo hapo kwaajili ya kutafuna tu fedha za walipa kodi na kuwaada wananchi huku wakijua moyoni kesi hiyo hatutaweza kushinda?

TISS ikishabaini ukweli pia ikachunguze katika ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ni kweli kabisa hatukuwa na wanasheria wa serikali ambao nao wangepewa fursa ya kuendesha kesi hiyo tangu ICC na Mahakama Kuu? Na endapo itabaini ni ngumu Tanesco kushinda rufaa katika Mahakama ya Rufaa, ni vyema iikataze Tanesco kukata rufaa mahakama ya rufaa kwani fedha zetu zitaendelea kutafunwa bure na mawakili na gharama za liba ya kuilipa Dowans zitakuwa zimeongezeka maradaufu.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali Jaji Fredrick Werema, Waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja hakuwa wapumbavu walivyojitokeza adharani siku za nyuma kusema ni lazima Dowans ilipwe licha baadhi ya wanasiasa na waandishi wa habari ambao ni mambumbu wa sheria waliwakejeli.

Werema na Ngeleja na wengineo walikuwa wakijua wanachokisema kwasababu ni wanasheria wazuri waliobobea katika fani hiyo.Na walichokisema ndicho kilichokuja kuamuliwa na mahakama kuwa tuzo ya Dowans isajiliwe.

Na cha kustajaabisha kabisa Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samwel Sitta na aliyekuwa Spika na kundi lake ambalo ndilo lilikuwa mstari wa mbele kutoa kauli za kuamasisha umma tuamini kuwa kampuni ya Richmond, Dowans ni kampuni za mafisadi na mikataba iliyoingiwa na Tanesco ivunjwe na leo hii wamekaa kimya utafikiri hawaishi Tanzania.Zile taasisi za wanaharakati ambazo ziliandaa maandamano ya kupinga Dowans isilipwe nazo leo hii baada ya hukumu kutolewa, hawasikikiti tena utafikiri wameaga dunia.

Hakuna ubishi yale malumbano ya visasi na kusingiziana kuhusu kampuni ya Richmond,Dowans na baina ya baadhi ya viongozi wa kisiasa hususasi wale wa CCM kuhusu mikataba ya makampuni hayo, kama serikali yetu isingekuwa imara, ni wazi leo hii taifa hili lingekuwa limeingizwa mtoni na malumbano hayo ambayo yalikuwa yanachagizwa kwa kiasi kikubwa na sisi vyombo vya habari bila kujua kilichopo nyuma ya ajenda hiyo ya malumbano.

Ieleweke wezi kuwa Tanzania itabaki kuwa nchi yetu na hao wanasiasa manyang’au ambao wamekuwa wakitumia ushawishi wao wa kisiasa kuutumia umma usifahamu kilichopo nyuma ya pazia ya ajenda chafu zao , watapita na kusaulika.

Hivyo nitoe rai kwa viongozi wetu wa siasa, taasisi za wanaharakati, vyombo vya habari na wananchi kuwa hukumu ile ya ICC na ile ya Mahakama Kuu ya Tanzania iwe funzo kwetu kuanzia sasa tukatae kugeuzwa makasuku wa ajenda chafu za wanasiasa hasa wa CCM na wale vyama vya upinzani kwani tukikubali kuwa makasuku wa ajenda za manyang’au mwisho wa siku tukubali matokeo kama haya ya kutakiwa na mahakama kuilipa fidia Dowans ya zaidi ya dola za kimarekani bilioni 111. Na tutakapotakiwa na mahakama kufanya hivyo tusikasilike, tufurahi kwani tuliyataka wenyewe.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika
0716 774494
Chanzo:Gaazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Oktoba 2 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.