Header Ads

HUKUMU KESI YA ARCADO NTAGAZWA OKTOBA 17, 2013




 
Na Happiness Katabazi
 
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imesema Oktoba 17 mwaka huu, ndiyo siku itakayotoa hukumu ya kesi ya kujipaia kofia ,fulana zenye jumla ya thamani ya Sh.milioni 74.9 kwa njia ya udanganyifu inayomkabili Waziri wa  zamani Arcado Ntagazwa na wenzake.
 
Hayo yamesemwa na Hakimu Mkazi Gene Dudu muda mfupi baada ya wakili wa utetezi Alex Mushumbusi kuiambia mahakama upande wa utetezi umefungua utetezi baada ya washitakiwa wote kumaliza kujitetea.
 
Hakimu Dudu alisema baada ya washitakiwa wote kumaliza kujitetea anautaka upande wa jamhuri na utetezi kuwasilisha kwa maandishi majumuisho yao ya mwisho ya kuiomba mahakama iwane washitakiwa wana hatia au la Oktoba 3 mwaka huu, na kwamba hukumu ya kesi hiyo ataitoa oktoba 17 mwaka huu.
 
Mbali na Ntagazwa , washitakiwa wengine ni mtoto wa Ntagazwa, Dk. Webhale Ntagazwa na mshitakiwa wa kwanza Senetor Mirelya (60) alishamaliza kutoa utetezi wake.
 
Aprili 23 mwaka 2012, ilidaiwa mahakamani hapo na Wakili wa Serikali Ladslaus Komanya  kuwa Oktoba 22 mwaka 2009 huko Msasani Mikoroshini washtakiwa hao kwania ovu walijipatia fulana 5000 na kofia 5000 zenye jumla ya thamani ya Shilingi milioni 74.9 toka kwa Noel Sevele kwa makubaliano kuwa wangemlipa Sevele kiasi hicho cha fedha katika kipindi cha mwezi mmoja tangu walipochukua vifaa hivyo lakini hata hivyo walishindwa kumlipa na washtakiwa walikana shtaka na kwamba upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika. 
 
Ntagazwa ambaye kwa sasa ni Kada wa Chadema , kabla ya kujiunga na chama hicho miaka minne iliyopita, akitokea chama cha Mapinduzi (CCM).Akiwa mwanachama wa CCM, aliwahi kuteuliwa na rais wa Serikali ya awamu ya pili na ya tatu, Ally Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa kushika nyadhifa za uwaziri katika wizara mbalimbali hadi ilipofika mwanzoni mwa mwaka 2006, Rais Jakaya Kikwete alipounda baraza lake jipya la mawaziri na kuamuacha nje ya baraza hilo. 
 
Ntagazwa ambaye aliwahi kuwa mbunge wa muda mrefu wa Jimbo la Mhambwe kwa tiketi ya CCM, hadi sasa nakumbukwa kwa msemo wake mmoja maarufu aliowahi kuutoa bungeni akiwa Waziri Nchi ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Mazingira alisema ‘Ipo siku wajukuu zetu watafukua makaburi yetu wachunguze ubongo wetu kama tulikuwa na akili timamu’. Ntagazwa alitoa msemo huo kutokana na kutoridhishwa na baadhi ya maamuzi yaliyokuwa yakifanywa na baadhi ya watendaji waliopewa dhamana.
 
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Septemba 25 mwaka 2013. 

No comments:

Powered by Blogger.