Header Ads

MKENYA WA DK.ULIMBOKA JELA MIEZI SITA




Na Happiness Katabazi
HATIMAYE Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imemhukumu kwenda jela miezi sita au kulipa faini ya Sh.1,000 ,raia wa Kenya, Joshua Mulundi ambaye alikuwa akikabiliwa na kosa moja la kutoa taarifa za uongo kwa ofisa wa polisi katika Kituo cha Polisi Oystebay  ambapo alimweleza ofisa huyo wa polisi yeye na wenzake ambao waliokodiwa kwenda kumteka na kumjeruhi Dk.Steven Ulimboka.

Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Alocye Katemana  alisema kesi hiyo ilikuja jana kwa ajili ya upande wa jamhuri kumsomea maelezo ya awali mshitakiwa huyo  ambapo Wakili Mwandamizi wa Serikali Tumaini Kweka alimsomea maelezo ya awali mshitakiwa  na baada ya kumaliza kusomea maelezo hayo , mshitakiwa huyo alikiri kutenda kosa hilo la kutoa taarifa za uongo polisi kinyume na  kifungu cha 122 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002.

Kabla ya Hakimu Katemana kutoa adhabu yake aliutaka upande wa jamhuri uzungumze lolote kama wanalo, ambapo wakili Kweka alidai kuwa anaiomba mahakama itoe adhabu inayostahili kwasababu kwa mazingira ya kesi hiyo , hali iliyojengeka katika jamii kuhusu sakata la kutekwa na kuteswa kwa Dk.Ulimboka ni tetete na kwamba ni kwamba si vyema kwa mtu mzima kama mshitakiwa kwenda kutoa taarifa za uongo polisi ambazo zilipelekea jamii kuwa na hisia tofauti kuhusu utekwaji wa Dk.Ulimbo na kuomba mahakama itoe adhabu kali.

Aidha kwa upande wake Mulundi alieleza kuwa yeye ni raia wa Kenya na kwamba lengo na madhumuni ya kuja Tanzania, ni kuja kufanyabiashara ya kuuza nguo. Juni  27 mwaka jana akiwa Arusha, alitekwa na mtu asiyemfahamu na wakati ametekwa huyo mtu alimwamuru afanye kila jambo atakalomtaka alifanye na kwamba yeye alikubali kufanya yote aliyokuwa akiamriwa na mtu huyo ambaye alikuwa akimpa maelekezo huku akiwa ameshika silaha.

“Mheshimiwa hakimu  kwa kuwa nilikuwa naogopa vitisho hivyo  nilifanya kama alivyokuwa akinielekeza na baadae mtu huyo aliyekuwa ameniteka akanipeleka hadi Tanga, sehemu ambayo sikuwa nimewahi kufika na kwamba mtu huyo akanieleza kuwa yeye ni mkristo na kwamba ananituma kwa mkristo mwenzie  na akanipa taarifa hizo nizipeleke kwa mkristo mwenzake  na taarifa hizo ndizo zilizosomwa hapa mahakamani na mwendesha mashitaka wakati akinisomea maelezo ya awali.

“Nilienda hadi katika kanisa la Ufufuo na Uzima lililopo Kawe Tanganyika Parkers  na kumkuta mchungaji Joseph Marwa Kiliba ambaye yule mtekaji aliniambia nimfikishie taarifa hizo na nilimfikishia kwani nilikuwa naogopa vitisho vile kwani yule mtekaji aliniambia endapo sitafikisha zile taarifa za ungamo langu niloungama polisi na kwa mlinzi wa amani atapewa taaarifa kwani huyo mchungaji ni mtu wao pia . Nikampatia taarifa zile kama nilivyoelekezwa baada ya hapo nikajikuta nakamatwa na pelekwa kituo cha polisi Oystebay kishwa kwa mlinzi wa amani katika Mahakama ya Mwanzo Kawe ambapo nilitoa taarifa hizo ambazo mwisho wa siku zilisababisha nifunguliwe kesi hii ya kutoa taarifa za uongo”alidai Mulundi.

Mapema jana asubuhi wakili Kweka akimsomea maelezo ya awali mshitakiwa huyo, alidai kuwa mshitakiwa ni Raia wa Kenya na kwamba alifika katika kanisa na Ufufuo na Uzima Kawe , mbele ya mchungaji  Kiliba  na kuungama na kusema kuwa yeye na wenzake ambao hawapo mahakamani ndiyo waliousika kumteka na kumtesa Dk.Ulimboka na kisha kwenda kumtupa katika Msitu wa Magwepande Dar es Salaam.

Baada ya kumaliza kuungama mbele ya mchungaji huyo, Mulundu alijikuta akikamatwa na wanausalama na kupelekwa kituo cha polisi Oystebay  mbele ya Sajenti  Nyagea  ambapo mshitakiwa huyo mbele ya askari huyo alisema kuwa yeye ndiye aliyeusika kumteka na kumtesa Dk.Ulimboka na baada ya hapo askari polisi huyo alimpeleka Mulindi kwa mlinzi wa amani katika mahakama ya mwanzo Kawe na mshitakiwa huyo alikiri kutenda kosa hilo.

Akitoa adhabu yake baada ya kusikiliza maombi ya pande zote mbili Hakimu Katema alisema kwakuwa mshitakiwa amekiri kosa kabla hata mashahidi wa jamhuri hawajaletwa kuja kutoa ushahidi wa kesi hiyo, mahakama yake inamhukumu kwenda jela miezi sita au kulipa faini ya Sh.1,000. Hata hivyo Mwandishi wa habari wa Redio Times, Chipangula  Nandule   aliyekuwepo mahakamani hapo alijitolea kumlipia faini hiyo ya Sh.1,000 na sekunde chache baadaye askari polisi walimkamata Mulundi na askari hao kwa masharti ya kutotajwa majina yao gazeti kwa maelezo kuwa wao siyo wasemaji wa jeshi, walisema kuwa Mulundi ni raia wa Kenya, hivyo wanamshikilia ili waweze kuandaa taratibu za kumrejesha nchini kwao Kenya.

Agosti 6 mwaka huu, Mkurugenzi  wa Mashitaka nchini(DPP), Dk.Eliezer Feleshi  alimfutia kesi ya kujaribu kumuua na kuteka Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari nchini Steven Ulimboka, raia wa Kenya Joshua Mulundi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, baada ya kuona hana haja kuendelea kumshitaki kwa makosa hayo ambayo yalikuwa hayana dhamana na kisha siku hiyo akamfungulia kesi mpya ya kutoa taarifa za uongo Polisi.


Wakili Kweka mbele ya Hakimu Katema alimsomea shitaka hilo mshitakiwa ambapo Julai 3 mwaka jana, katika Kituo cha Polisi Oystebay mshitakiwa huyo alitoa taarifa za uongo kwa ofisa wa polisi ambapo alimweleza ofisa huyo wa polisi yeye na wenzake ambao waliokodiwa kwenda kumteka na kumjeruhi Dk.Ulimboka jana ambalo si kweli kosa ambali ni kinyume na kifungu cha 122 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 na kuongeza kuwa upelelezi wa kesi hiyo mpya umekamilika.

Wakili Kweka alidai licha kosa hilo lina dhamana kwa mujibu wa sheria lakini upande wa jamhuri unaomba asipewe dhamana kwaajili ya usalama wake,kesi hiyo ina maslahi kwa taifa hoja ambayo ilimlazimu hakimu Katemana aairishe kesi hiyo kwa muda na kisha kuutaka upande wa jamhuri uende ukalete kwa maandishi hati ya kumfungia dhamana mshitakiwa huo.

Julai 13 mwaka 2012, Mulundi (21), alifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza akikabiliwa na makosa mawili, kosa la kwanza ni la kutaka kuua Dk.Ulimboka na kosa la pili ni la kumteka,ambapo makosa hay ohayo kwa mujibu wa sheria hayana dhamana na yanasikilizwa na Mahakama Kuu peke yake na kwamba mahakama ya Kisutu ilikuwa haina mamkala ya kusikiliza kesi hiyo hiyo na hivyo kusababisha kukaa gerezani tangu siku hiyo.

Wakili wa serikali, Ladslaus Komanya, mbele ya Hakimu Agnes Mchome, alidai kuwa Mulundi ambaye mkazi yake ni Murang’a nchini Kenya, anadaiwa kuwa  Juni 26 mwaka jana, akiwa eneo la Leaders Club alimteka Dk. Ulimboka.
Katika shtaka la pili, Komanya alidai kuwa Juni 26 mwaka huu, akiwa katika eneo la Msitu wa Mwabepande Tegeta, Dar es Salaam, kinyume cha sheria, mshtakiwa huyo alijaribu kumsababishia kifo Dk. Ulimboka.

Hakimu Mchome alisema mshtakiwa hatakiwi kujibu chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza shauri hilo, kwani Mahakama Kuu ndiyo yenye mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo.

Juni 27 mwaka 2012, Dk. Ulimboka aliokotwa na msamalia mwema katika msitu huo wa Mwagwepande akiwa amejeruhiwa vibaya na kisha akafikishwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili akiwa na maumivu makali na kuanza kutibiwa na kisha kupelekwa afrika Kusini kwaajili ya matibabu zaidi na kisha kurejeshwa nchini akiwa amepona.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Oktoba Mosi mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.