Header Ads

MENEJA BOA BANK ATETEA FEDHA ZA EPA

Na Happiness Katabazi

MENEJA Mkuu Msaidizi anayeshughulika na wateja wadogo wa Benki ya Afrika (BOA), Jerome Kimario (39), ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kuwa ingizo la shillingi bilioni sita toka Benki Kuu kwenda akaunti ya Kampuni ya Kennely Ltd inayomilikiwa na Jonhson na ndugu yake Mwesigwa Lukaza halikuwa na kasoro yoyote.


Kimaro ambaye ni shahidi wa kwanza wa upande wa Jamhuri katika kesi ya wizi wa sh bilioni 6, katika akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), inayowakabili washtakiwa hao wanaotetewa na mawakili wa kujitegemea Richard Rweyongeza na Alex Mgongolwa alitoa maelezo hayo jana wakati akihojiwa na wakili wa utetezi Alex Mgongolwa mbele ya jopo la mahakimu wakazi, Prophil Lyimo, Edson Mkasimongwa na Salome Mwandu, ambapo jana kesi hiyo ilianza kusikilizwa rasmi.

Kimario alidai washtakiwa hao ambao waliwasilisha nyaraka sahihi mwaka 2004, wakiomba kufungua akaunti ya kampuni hiyo kwa kianzio cha shilingi milioni 15, ambapo BOA, haikuwa na shaka kuhusiana na akaunti hiyo kutokana na kwamba kampuni ni mteja wa kuaminika.

“Kennely Ltd inamilikiwa na Johnson na Mwesigwa ni wateja wazuri wa benki yetu kwani walifuata taratibu zote za ufunguaji akaunti ambapo waliweka kianzio cha sh milioni 15, na Desemba 7, 2005, BoT iliingizia akaunti ya kampuni hiyo dola za Kimarekani milioni 6 na kwa kweli benki yetu ililipokea vyema ingizo hilo na kulifanyia kazi kitaalamu kwani tulibaini halikuwa na kasoro zozote,” alieleza Kimario.

Awali akiongozwa kutoa ushahidi wake na Wakili wa Serikali Timon Vitalis aliithibitishia mahakama kuwa ni kweli mshtakiwa wa kwanza (Johnson), ndiye aliyefungua akaunti hiyo kwa kuwasilisha nyaraka halali, na kudai mshtakiwa wa pili hakuhusika katika ufunguaji wala uchukuaji wa fedha katika akaunti hiyo.

Kiongozi wa Jopo la Mahakimu Wakazi, Profil Lyimo, aliahirisha usikilizaji wa kesi hiyo hadi leo na kuamuru upande wa serikali umlete shahidi wa pili.

Wakati huo huo mfanyakazi wa Benki ya International Commercial, Dorine Chonjo, anayetetewa na wakili wa kujitegemea, Furgence Massawe, alifikishwa mbele ya Hakimu Mkazi Stewart Sanga, akikabiliwa na mashtaka matatu ya kula njama, kughushi na wizi wa sh bilioni moja kwa njia ya mtandao, mali ya benki hiyo.

Wakili wa Serikali Tofil Mtakyawa alidai makosa hayo yalitendeka Desemba 21 mwaka jana. Mshtakiwa alikana mashtaka yote.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Aprili 21 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.