Header Ads

KWANINI TUANDALIWE KUHONGA NA KUHONGWA?

Na Happiness Katabazi

SHERIA ya gharama za uchaguzi ya mwaka 2010 iliyosainiwa na Rais Jakaya Kikwete hivi karibuni si suluhisho la rushwa katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba na chaguzi za miaka mingine ijayo.


Kwanza sheria hiyo imekuja ghafla na kushtukiza. Leo hii ni Aprili ikiwa ni miezi takriban sita kabla taifa halijaingia katika uchaguzi.

Wanachama wa CCM wanaotaka urais, ubunge na udiwani walishaanza kampeni miaka mitatu iliyopita, sheria hii inasaidia nini kudhibiti mamilioni ya fedha yaliyokwishatumika katika kipindi hicho?

Sheria hiyo inataka fedha zipitie kwenye chama cha siasa husika lakini ni ukweli usiopingika kuwa fedha nyingi zimeshapitia au zinapitia katika mikono ya watu binafsi kwa ajili ya kampeni, hizi zitadhibitiwa vipi?

Tatu; sheria hiyo ya gharama za uchaguzi inatamka kiasi cha fedha atakachotumia mgombe urais, ubunge na diwani, vyanzo halali vya fedha hizo viko wapi? Mbona sheria hiyo haitambui wawezaje kupata hizo fedha kutokana na vyanzo halali?

Inataka mgombea udiwani atumie kiasi cha fedha kisichozidi milioni saba lakini haiangalii uwezo wa vyama husika ambavyo kila kukicha vimekuwa vikigalagala kwa njaa isipokuwa CCM.

Vyama visivyokuwa na uwezo vitawezaje kuwapa wagombea ubunge kiasi kisichozidi milioni 50 ili kuwania ubunge? Hapa si tunaendelea kuwaneemesha wabunge wanaolipwa kiinua mgongo kila unapokaribia uchaguzi?

Bila shaka wenye kunufaika zaidi ni wana CCM ambao wana wabunge wengi pamoja na vitega uchumi mbalimbali vilivyojengwa kwa nguvu ya wananchi lakini sasa vinatumika kwa manufaa ya chama.

Kwa mujibu wa sheria hiyo mgombea urais anatakiwa asitumie zaidi ya sh bilioni tano, hapa ni lazima tuweke mazingira mazuri ya kujua usafi na uhalali wa fedha zinazotolewa na mgombea au chama chake ili kufanikisha azma waliyojiwekea.

Je, rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania analipwa kiasi gani? Anao uwezo wa kudunduliza fedha zitakazomsaidia katika kampeni hizo au chama chake kitakuwa tayari kutoa fedha zote hizo?

Ikiwa mgombea hana uwezo au marafiki wa kumchangia fedha za kampeni, je, chama chake kina vyanzo halali vya fedha?

Chama tawala kimekuwa kikihusishwa mara kwa na ukwapuaji wa fedha kwenye mashirika ya umma au zile wanazopewa na wafanyabiashara ambao inadaiwa kuwa hupatiwa misamaha ya kodi kwa biashara wanazozifanya.

Kwa hali ilivyo si kila chama kina mwanya wa kutoa misamaha ya kodi kwa wafanyabaishara au kukatiwa ‘mishiko’ na baadhi ya wawekezaji wanaopora rasilimali za nchi ambao wamekuwa wakipewa kipaumbele kikubwa zaidi kuliko wazawa.

Kumbe hili la chama kuwa chanzo cha fedha za uchaguzi ni mwanya wa rushwa na ufisadi uliovishwa joho la kisheria. Serikali haijakubali kwamba itachangia kwa vyovyote vile gharama za uchaguzi .Hilo ndilo tulilolitazamia liwe lengo kuu la sheria hii.

Kila mgombea akigharamia kwa kiwango fulani na kodi ya wananchi ni halali kumbana asizidishe kiwango fulani kilichowekwa na sheria ya gharama za uchaguzi anapochangisha fedha.

Lengo la sheria kama hii ni kupambana na fedha chafu kuingizwa kwenye mfumo wa uchaguzi wa nchi yetu, jingine ni kuzuia matumuzi mabaya ya kifisadi, kuhonga wapiga kura jambo ambalo litapelekea kuwa na serikali iliyoletwa madarakani kwa rushwa.

Kwa kuwa hayo yote hayakuzingatiwa na sheria, tunaona sasa wagombea wengi wa CCM hususan wa Jimbo la Ubungo ambako mimi ni mkazi wake tunawashuhudia kwa miaka miaka mitatu sasa makada wa chama hicho wakiendelea kuvinjari mitaani na maburungutu ya fedha ambayo hatuyajui wameyapata wapi.

Na mbaya zaidi wala hatuoni Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ikiwashughulikia. Kwa hiyo tuna haki ya kuamini kwamba sheria hii ni danganya toto na kuwa uchaguzi mkuu wa mwaka huu utakuwa mchafu, wenye rushwa ya kupindukia kupita uchaguzi wowote uliokwishafanyika hapa nchini. Nawatakia Pasaka Njema.

Mungu Ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Aprili 4 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.