Header Ads

MHINZI WA TEFFA KORTINI KWA KUISHI NCHINI BILA KIBALI


Na Happiness Katabazi

Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu  wilaya ya Temeke (TEFA), Peter Steven Mhinzi (64),jana alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, akikabiliwa na mashitaka ya kuishi nchini, kinyume na sheria.

Mbele ya Hakimu Devotha Kisoka, Mwendesha Mashtaka wa Uhamiaji, Patrick Ngayomela alidai kuwa Mhinzi anakabiliwa na kosa la   kuishi nchini kinyume na kifungu cha 31 (1) na (2) cha sheria ya Uhamiaji, na kuwa   Julai 14, mwaka 2010 katika ofisi ya uhamiaji Temeke , Mhinzi akiwa raia wa Burundi  alipatikana akiishi nchini bila ya kuwa na kibali cha kuishi nchini.

Wakili  Ngayomela alidai kuwa  upelelezi wa kesi bado haujakamilika ,na kwamba  hawana pingamizi na dhamana na akaomba  mahakama ipange tarehe ya kutajwa kwa kesi hiyo ili kuangalia kama upelelezi wa shauri hilo kama umekamilika. 

Wakili wa Muyinzi, Mtiginjola aliiomba  mahakama kumpa dhamana mteja wake, Hakimu Devotha Kisoka alimuachia huru Mhinzi baada ya kukamilisha masharti ya dhamana ya kuwa na wadhamini wawili wanaominika ambao kila mmoja wao pamoja nay eye mwenyewe walisaini bondi ya Sh 5 milioni.

Hata hivyo, baada ya zoezi hilo kukamilika, Wakili Mtiginjola aliiomba mahakama kuifuta kesi hiyo  kwa madai kuwa ilipelekwa mahakamani hapo na upande wa mashtaka kinyume na sheria.
Alidai kuwa mtuhumiwa huyo aliwahi kuandikiwa barua na Mkurugenzi wa Idara ya Uhamiaji wa Mkoa wa Dar es Salaam, akimtuhumu  kuwa yeye siyo raia  wa Tanzania na kumuamuru aondoke nchini  ama aombe kibali cha kuwepo hapa nchini.

Mtiginjola  alidai kuwa baada ya kutolewa kwa tuhuma hizo, Mhinzi alifungua  maombi maalum Oktoba 7 mwaka 2011 katika Mahakama Kuu ya Tanzania akidai kuwa ametuhumiwa pasipo kupewa nafasi  ya kusikilizwa.

Aliongeza kudai kuwa, Mahakama Kuu ilikubaliana na maombi ya Mhinzi  Oktoba 20, 2011 na kuamuru kuwa asifanyiwe bughudha yoyote hadi maombi yake ya msingi yatakaposikilizwa. Alisisitiza kuwa uamuzi huo ulikuwa na maana kuwa chochote kisifanyike dhidi ya mshtakiwa  hadi hapo maombi ya msingi yatakaposikilizwa baina ya pande mbili.

“Mheshimiwa hakimu tumeshtushwa   kwa kufunguliwa kwa shauri hili jipya linalodai mteja wangu anaishi nchini kinyume na sheria wakati tayari kuna amri ya Mahakama Kuu inayozuia Mhinzi asibughudhiwe hadi maombi ya msingi yatakaposilizwa, chochote kitakachoendelea kitakuwa ni dharau  dhidi ya uamuzi huo uliotolewa na Jaji Frederick Mgaya ambao hadi sasa bado haujatenguliwa.”Alidai wakili Mtiginjola.

Alidai kuwa ilikuwa ni tegemeo la Muhinzi  kuona upande wa Jamhuri ukijibu maombi yake ili iweze kuonekana kuwa alipata haki ya kusikilizwa ama la na ndipo afunguliwe shtaka hili lakini hilo halikufanyika.
Hivyo kuendelea kusikilizwa kwa shauri hili ni kama Mahakama  ya Hakimu Mkazi Kisutu na Mahakama Kuu zinapimana nguvu  na  kuomba ifutwe.

Kwa upande wa wakili Ngayomela, aliiomba  shauri hilo liendelee kusikilizwa katika mahakama ya Kisutu kama jinsi lilivyosajiliwa na kwamba muda uliowekwa na mahakama Kuu wa kutaka mshtakiwa huyo asibughudhiwe  umekwisha pita. Hata hivyo kwa upande wake Hakimu Kisoka  alisema atatoa uamuzi juu ya hoja hizo Juni 14, mwaka huu,.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Mei 30 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.