Header Ads

AKIBA BENKI KORTINI KWA UPOTEVU WA FEDHA ZA MTEJA WAKE



Na Happiness Katabazi

MKURUGENZI wa Kampuni ya Principal Company Limited, Godfrey Mosha ameieleleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam jinsi  Benki ya Akiba Commercial  Tawi la Ubungo ilivyoidhinisha malipo ya fedha  kwa mtu mwingine kutoka katika akaunti yake ndani ya benki hiyo, bila yeye kuwa na taarifa wala kuridhia.

Katika kesi hiyo ya madai ya uzembe iliyofunguliwa na Mosha dhidi ya Benki ya Akiba, inayosikilizwa na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Warialwande Lema, Mosha anaomba Benki hiyo imlipe  Sh.milioni 46.8 , zilizolipwa kwa mtu asiyemfahamu kwa kutumia hundi nne tofauti na kwa tarehe tofautitofauti ambazo alidai hundi hizo zimeghushiwa.

Akiongozwa na wakili wake Michael Ngaro kutoa ushahidi wake mbele ya Hakimu Lema, Mosha ambaye ni mlalamikaji katika kesi hiyo, alidai kuwa aligundua  hamisho hilo la kiasi hicho cha fedha katika akaunti ya kampuni yake Na. 0400438671, Novemba 15, 2011, alipochukua taarifa ya kibenki (Bank Statement).

Mosha alidai kuwa  baada ya kubaini hamisho hilo , alikwenda makao makuu ya benki hiyo ambako alimuona Meneja wa Fedha, Vicent Antony na kumwalifu kuhusu  tukio hilo wakati yeye hajawahi kuidhinisha hamisho hilo.

“Vicent aliniambia kuwa siyo transfer (hamisho) bali ni malipo yaliyofanyika kwa kutumia cheque. Aliniambia namba za hundi hizo na ikaonekana kuwa zililipwa kwa Rafael John Mkwabi, mwenye namba ya akaunti 11000787541.”, alidai Mosha na kuongeza:

“Binafsi huyo John  sijawahi kumwandikia hundi wakati wowote ule , wala sijawahi kufanya naye biashara, sijawahi kukutanana naye, wala simfahamu kabisa.”

Mosha alidai kuwa hundi hizo zilikuwa zimesainiwa na Vicent na Meneja Mkuu, Salehe Ramadhani, huku akidai kuwa saini inayoonekana katika hundi hizo si yake.

Alizitaja hundi hizo kuwa ni hundi namba 083722, ya Sh11.6 milioni iliyolipwa Novemba 11, 2011 na  hundi namba 083723, ya Sh 9 milioni, pia iliyolipwa tarehe hiyo.Hundi nyingine  ina namba   083724 , ya Sh milioni 14.4  iliyolipwa Desemba 2011, na hundi namba 083725, ya Sh.milioni 11.8  iliyolipwa Desemba 3, 2011.

Mosha kupitia wakili wake Ngaro alizitoa hundi hizo na nyaraka nyingine mbalimbali   na kuomba zipokelewe kama vielelezo.Na baada ya kumaliza kutoa ushahidi wake, wakili , Ngalo alifunga ushahidi na hakimu Lema aliarisha kesi hiyo hadi Julai 8 mwaka huu, iyakapokuja kwaajili ya mdaiwa ambaye ni benki ya Akiba inayotetewa na wakili wa kujitegemea Karoli Tarimo  waanze kujitetea.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatatu, Juni 24 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.