Header Ads

DIWANI CCM JELA MIAKA 10 KWA RUSHWA

Na Happiness Katabazi, Tunduru

MAHAKAMA ya Wilaya ya Tunduru, imemhukumu kifungo cha mika 10 jela na faini ya sh milioni 6.7 Diwani wa Viti Maalum (CCM) Kata ya Mlingoti, Atindanga Mohammed kwa makosa 11 ya rushwa.


Hukumu hiyo ya aina yake ilitolewa jana na Hakimu Shemuli Cyprian baada ya mahakama hiyo kuridhishwa na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka ambapo diwani huyo aligawa vitenge na kanga kwenye Uchaguzi Mkuu mwaka 2010.

Katika kesi hiyo upande wa mashtaka uliwakilishwa na wakili wa serikali kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Christa Kadekenga.

Hakimu Cyprian alisema mshtakiwa huyo alikuwa akikabiliwa na makosa 15 ya kushawishi na kutoa rushwa kwa wapiga kura 15 ili wampigie kura za ndiyo ashinde udiwani huo ambapo alitoa doti 12 za kanga na doti tatu za vitenge kwa wapiga kura hao.

“Mahakama hii imeridhika na ushahidi na vielelezo vilivyotolewa na upande wa Jamhuri…inakutia hatiani kwa makosa 11 na kukufutia makosa mengine manne kwa sababu upande wa Jamhuri katika kesi hii umeshindwa kuthibitisha makosa hayo,” alisema hakimu Cyprian.

Baada ya hukumu hiyo diwani Atindanga, aliangua kilio ndani ya mahakama kisha kupakizwa kwenye karandika kwa ajili ya kupelekwa gerezani kuanza kutumikia kifungo hicho.

Katika uchaguzi wa Rais, wabunge na madiwani uliofanyika nchini kote mwaka jana, madai ya kuwepo kwa rushwa yalitawala licha ya Rais Jakaya Kikwete kutia saini Sheria ya Matumizi ya Fedha za Uchaguzi.

Hata hivyo ushindi wa baadhi ya madiwani na wabunge umepingwa mahakamani, mengi ni madai ya rushwa kwenye uchaguzi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Juni 21 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.