Header Ads

WALIONDAMANA DAR WAPATA DHAMANA

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imewapa dhamana wafuasi watatu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wakiwemo wanafunzi wa vyuo vikuu wanaokabiliwa na kesi ya kufanya maandamano bila kibali.

Wafuasi hao ni Julian Daniel (24) mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), General Kaduma (25) ambaye ni Mwanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) na Joseph Mseti (50) ambaye ni mkulima.

Watuhumiwa hao wanatetewa na wakili wa kujitegemea Mabere Marando wakati upande wa jamhuri uliwakilishwa na mwanasheria wa serikali Elizabert Kaganda.

Hakimu Mkazi Sundi Fimbo alisema ameamua kuwapatia dhamana washtakiwa hao ambao walifikishwa kwa mara ya kwanza juzi baada ya kutimiza masharti ya dhamana ambayo yaliwataka kila mshtakiwa kuwa na wadhamini wawili watakaosaini bondi ya sh milioni nne.

Hakimu Fimbo aliahirisha kesi hiyo hadi Juni 21 mwaka huu, itakapopelekwa kwa kwaajili washtakiwa kusomewa maelezo ya awali.

Washtakiwa hao walikamatwa Juni 5, mwaka huu jijini Dar es salaam walipokuwa wakiandamana bila kibali kushinikiza kuachiwa huru kwa Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe aliyekuwa akishikiliwa na polisi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Juni 8 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.