Header Ads

'WASHTAKIWA SAMAKI WA MAGUFULI WANA KESI YA KUJIBU'

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa Jamhuri katika kesi ya uvuvi haramu kwenye kina kirefu cha Bahari ya Hindi upande wa Tanzania, umeiomba Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, iwaone washtakiwa wana kesi ya kujibu.


Ombi hilo liliwasilishwa jana na Wakili Mwandamizi wa Serikali Biswalo Mganga mbele ya Jaji Augustine Mwarija ambapo aliikumbusha mahakama kuwa kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya upande wa Jamhuri kuwasilisha majumuisho ya kesi hiyo, kuwaona washtakiwa wote 36 kuwa wana kesi ya kujibu.

Wakili Mganga aliomba mahakama hiyo izitupe hoja za upande wa utetezi zilizowasilishwa mwishoni mwa wiki zikiiomba mahakama hiyo iwaone washtakiwa wote hawana kesi ya kujibu kwa sababu vielelezo na ushahidi uliotolewa na mashahidi wote 13 wa Jamhuri ni thabiti utaishawishi mahakama iweze kuwaona washtakiwa wana kesi ya kujibu.

Mganga aliyetumia saa nne kuwasilisha hoja zake, alidai kuwa shahidi wa tatu, Kapteni Ernest Bubamba, kutoka Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi aliieleza mahakama kwamba siku ambayo meli ya Tawariq 1 ilikamatwa, aliyeingia melini na kuikaguzi ambapo rada ‘GPS’ ilimwonyesha kuwa meli hiyo ilikamatwa eneo la Tanzania.

Kwa mujibu wa shahidi huyo, alipomhoji nahodha wa meli hiyo ambaye ni mshtakiwa wa kwanza alikiri kuvua katika eneo hilo na kwamba walikuwa na kibali cha kufanya hivyo.

“Mheshimiwa Jaji, Bubamba katika ushahidi wake alidai kuwa alipotaka kibali hicho, mshtakiwa alimpa kibali kinachoonyesha kilitolewa na Serikali ya Zanzibar Januari 2, 2008 na kinamalizika Aprili 4 mwaka huohuo… kilitolewa kwa meli ya Tawariq 2 siyo Tawariq 1 iliyokuwa ikitumiwa na washtakiwa. Meli hiyo ni kielelezo pia,” alidai wakili Mganga.

Wakili huyo alidai kwamba shahidi huyo aliiambia mahakama kuwa wakati akiikagua meli hiyo alikuta baadhi ya samaki wakivuja damu, wengine wamehifadhiwa kwenye majokofu.

“Upande wa Jamhuri tunadiriki kusema tumeweza kuthibitisha kesi yetu kikamilifu kwani washtakiwa wanakabiliwa na kosa la kuvua bila leseni, ni kweli leseni aliyokutwa nayo mshtakiwa wa kwanza inaonyesha ilitolewa kwa meli ya Tawariq 2 na siyo Tawariq 1 na leseni hiyo ilikwisha muda wake na wewe jaji umeipokea kama kielelezo.

“Pia rada ya meli hiyo GPS ilisoma meli hiyo kati ya Januari 10 na Machi 8 mwaka 2008 meli hiyo ilikuwa ikivua katika eneo hilo, ni kwa nini samaki hao wawe wanavuja damu katika kipindi hicho walichokamatwa?” aliuliza Mganga.

Jaji Mwarija aliahirisha kesi hiyo hadi leo ambapo upande wa Jamhuri utaendelea kuwasilisha hoja zake za kuishawishi mahakama iwaone washtakiwa hao ambao hadi sasa wanasota rumande baada ya kunyimwa dhamana.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Juni 21 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.