Header Ads

SERIKALI YASHINDA KESI TANO MAUJI YA ALBINO


Na Happiness Katabazi

MKURUGENZI wa Mashtaka nchini (DPP),Eliezer Feleshi ameeleza kuwa hadi sasa ofisi yake imeshinda jumla ya kesi tano za mauji ya watu wenye ulemavu wa ngozi(Albino) walizokuwa wamezifungua katika Kanda mbalimbali za Mahakama Kuu hapa nchini na Mahakama Kuu nchini.


Sambamba na kushinda kesi hizo tano za mauji ya albino, pia imeweza kushinda kesi moja ya biashara haramu ya kusafirisha binadamu ( Human Traffick and Abduction) iliyomhusisha Robison Mukwena ambaye ni mlemavu wa ngozi.

Akizungumza na Tanzania Daima katika mahojiano maalum ofisini kwake jijini Dar es Salaam, Feleshi alianza kwa kutoa takwimu ambapo alisema kuanzia mwaka 2007 hadi Januari 2011 jumla ya matukio 54 yanayowahusu watu wenye ulemavu wa ngozi yaliripotiwa kwa Jeshi la Polisi kote nchini nzima na jumla ya matukio manne ndiyo yaliyotokea mwaka 2010 katika wilaya za Kibondo,Kahama,Mwanza na Morogoro.

Feleshi alisema hadi sa jumla ya kesi tano za mauji ya Albino zimeshasikilizwa na kutolewa hukumu na Mahakama Kuu Kanda mbalimbali. Alizitaja kesi hizo za mauji ni kesi ya jinai Na.24/2009 ya Jamhuri dhidi ya Masumbuko Matata ‘Matata’ na wenzake wawili.Ambapo washtakiwa wote walitiwa hatiani na mahakama kwa kosa la mauji na washtakiwa hao wakakata rufaa katika Mahakama ya Rufaa lakini mahakama hiyo ya rufaa iliitupilia mbali rufaa hiyo.

Mkurugenzi huyo wa Mashtaka aliitaja kesi ambayo ni Na.26/2009 Jamhuri dhidi ya Joseph Lugata ambapo mahakama ilimtia hatiani mshtakiwa huyo na mshtakiwa huyo alikata rufaa mahakama ya rufaa na mahakama ya rufaa hadi sasa bado haijatoa hukumu ya rufaa hiyo.

Akiizungumzia kesi tatu ambayo Jamhuri ilishinda ni kesi Na.25/2009 iliyokuwa ikimkabili Mboje Mawe na wenzake watatu ambao walitiwa hatiani na Mahakama Kuu kwa kosa la mauji na wamekata rufaa mahakama ya Rufaa na hadi sasa mahakama hiyo ya juu kabisa nchini bado haijaanza kusikiliza rufaa hiyo.

Feleshi alisema kesi ya nne waliyoshinda ni kesi Na.42/2009 iliyokuwa ikimkabili Kazimili Mashauri na mwenzake ambapo Mashauri alitiwa hatiani na mwenzake akaachiliwa huru na aliyetiwa hatiani alikata rufaa Mahakama ya Rufaa na rufaa yake bado haijaanza kusikilizwa.

Aidha kesi ya tano ni kesi Na.672/2010 iliyofunguliwa na Jamhuri dhidi Nathan Mutei Mwasha iliyofunguliwa na kusikilizwa na Mahakama ya Wilaya ya Nyagamana mkoani Mwanza na mshtakiwa alitiwa hatiani kwa kosa la biashara haramu ya kusafirisha binadamu (Human Traffick and Abduction) iliyomhusisha Robison Mukwena ambaye ni mlemavu wa ngozi kutoka Kenya aliyesafirishwa kwa lengo la kuuzwa ambapo Feleshi alisema kesi hiyo ilisikilizwa ndani ya 20 na mahakama na kisha kutolewa hukumu.

Hata hivyo alisema kesi moja ya mauaji ya albino Na.22/2009 iliyofunguliwa na Jamhuri dhidi ya Mwigulu Madata na wenzake imeishaanza kusikilizwa na katika Mahakama Kuu Kanda ya Tabora. Na kuongeza kuwa bado kesi nyingine za mauji ya aina hiyo zinaendelea kusikilizwa na mahakama.

“Ushindi wa kesi hizo ambazo zilifunguliwa mahakamani na ofisi yangu na kuendeshwa timu ya waendesha mashtaka wangu ambao wamebobea kwenye tasnia ya kuendesha mashtka nadiriki kusema kuwa umechangia kwa kiasi kikubwa mauji ya albino kupungua kwani kabla ya watuhumiwa kukamatwa na kufikishwa mahakamani walifikiri serikali imelala lakini baada ya baadhi ya watuhumiwa kutiwa hatiani na makosa hayo ya mauji vitendo hivyo vya kikatili ambavyo vilikuwa vinailetea sifa mbaya nchini yetu kwenye uso wa dunia”alisema Feleshi.

Akizungumzia ushindi mwingine ambao ofisi yake imeupata Mei 23 mwaka huu, katika kesi ya jinai Na.1161/2008 Jamhuri dhidi ya Mweka Hazina wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Mkoani Kigoma, Rajabu Maranda na Binadamu yake Farijala Hussein ambao walikuwa wakikabiliwa na kesi ya wizi wa Sh bilioni 1.8 katika Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki Kuu ya Tanzania, ambapo Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilihukumu kwenda jela miaka mitano jela alisema , siri ya ushindi huo ni jeshi la polisi liliipatia ofisi yake ushahidi mathubutu na waendesha mashtaka wake walitumia vyema taaluma yao kisheria na ushahidi huo katika kuendesha kesi hiyo na mwisho wa siku upande wa Jamhuri ukaibuka mshindi.

Aidha alisema ofisi yake inafanyakazi kwa misingi ya taaluma ya sheria na ushahidi uliokusanywa na vyombo vya upelelezi na kamwe hatakubali ofisi yake ifungue kesi mahakamani kwaajili maneno yanayosemwa barabarani ambayo hayana msingi wowote wa kisheria na wala hayana ushahidi mathubutu ambao hauwezi kuishawishi ofisi yake kufungua kesi yoyote dhidi ya mtu yoyote mahakamani na kuongeza kuwa ofisi yake kote mikoani imejipanga kikamilifu kuakikisha inaendelea kufanya kazi zake kwa misingi ya kisheria.

Itakumbukwa kuwa miaka mitatu nyuma wimbi la mauji ya watu wenye ulemavu wa ngozi lilishamiri hapa nchini hali iliyosababisha albino kuishi kwa hofu na serikali kutangaza vita dhidi ya watu wote wanajiusisha na mauji hayo kwa ambayo yaliusishwa na imani za kishirikina na mwisho wa siku Jaji Mkuu Mstaafu Agustino Ramadhani alitenga bajeti ya fedha kwaajili ya kuzishughulikia kesi za mauji hayo ambazo ziliendeshwa na kutolewa maamuzi haraka zaidi lengo likiwa ni jitihada za serikali za kutokomeza mauji hayo ambayo yalikuwa yanaipa sifa mbaya Tanzania.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatatu, Juni 6 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.