Header Ads

KESI YA MPENDAZOE YAONDOLEWA KORTINI

Na Happiness Katabazi
MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imetoa amri ya kuondolewa kwa hati ya madai ya kesi ya kupinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 wa Jimbo la Segerea iliyokuwa imefunguliwa na aliyekuwa mgombea ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya (CHADEMA), Fred Mpendazoe dhidi ya mbunge wa sasa (CCM), Dk.Makongoro Mahanga na wenzake mahakamani hapo baada ya kubaini hati hiyo ina mapungufu yanayosababisha wadaiwa kushindwa kuaandaa utetezi wao.


Mbali na Mahanga ambaye ni Naibu Waziri wa Kazi na Ajira wengine ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Segerea ambapo mdaiwa wa kwanza na wa pili wanatetewa na mawakili wa serikali David Kakwaya na Patience Ntwina na Mahanga anatetewa na wakili wa kujitegemea Jerome Msemwa.

Uamuzi huo ulitolewa jana mchana na Jaji Profesa Ibrahim Juma ambapo alisema kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya yeye kutolea uamuzi mapingamizi matatu yaliyowasilishwa mbele yake na upande wa utetezi Mei 25 mwaka huu, ambayo yaliomba mahakama hii itoe amri ya ama ya kuifuta kesi hii au kuamuru hati ya madai ifanyiwe marekebisho kwasababu baadhi ya aya zilizopo ndani ya hati hiyo zina mapungufu yanayonyima haki wadaiwa kuandaa utetezi wao.

Jaji Profesa Juma alisema amefikia uamuzi wa kukubaliana na mawakili wa serikali wa kwasababu mapingamizi yao ya msingi wa kisheria kwani baadhi ya baadhi ya Aya katika hati hiyo ya madai inasomeka kuwa wasimamizi wa uchaguzi katika vituo vinne vya kupigia kura toka Kata ya Buguruni, vituo viwili toka Kata ya Tabata, Vituo vinne toka Kata ya Kipawa walikubali matokeo bila ya kura zote zilizopigwa kuhesabiwa.

“Kwa kuwa hati hiyo ya madai katika aya yake ya 7:4 mlalamikaji ameishia kutaja idadi hiyo ya vituo toka katika Kata hizo za Buguruni, Tabata na Kipawa na akashindwa kutaja majina yenyewe ya vituo hivyo, jumla ya idadi za kura zilizopigwa na jumla ya idadi ya kura zilizopigwa kwa kila mgombea …mahakama hii inakubaliana na hoja za upande wa utetezi kuwa kwa mdaiwa huyo kushindwa kuweka wazi majina ya vituo na idadi ya kura kutasababisha upande wa utetezi kukosa haki ya kuandaa utetezi wao katika kesi hiyo.

“Kuhusu aya 7:5 katika hati hiyo Mpendazoe anadai kuwa majina yote ya Wasimamizi wa vituo vya kupigia kura toka Kiwalani,Vingunguti na baadhi toka Buguruni,Tabata na Kipawa kuwa walijumlisha matokeo katika fomu Na.21B ambazo siyo fomu rasmi za Tume ya Uchaguzi….pia mahakama hii inakubaliana na upande wa utetezi kuwa aya hiyo pia ina mapungufu na mahakama hii inaamuru hati ya madai iondolewe mahakamani ili ikafanyiwe marekebisho”alisema Jaji Juma.

Akiendelea kuchambua mapungufu hayo yaliyokuwemo kwenye hati hiyo huku akitumia baadhi ya mifano mbalimbali ya kesi, Jaji Juma alisema pia anakubaliana na hoja ya utetezi kuwa aya ya 7:6 ya hati hiyo ya madai ambayo mlalamikaji anadai kuwa jumla ya majina ya vituo 53 vya kupigia kura matokeo yake hayakujumlishwa na kusema kuwa haya hiyo pia ina mapungufu kwasababu mlalamikaji alipaswa ataje majina ya

Aidha alisema pia anakubaliana na upande wa utetezi kuwa Aya ya 7.7 nayo ilikuwa na mapungufu kwasababu mlalamikaji ameshindwa kutaja majina ya maofisa wa vituo vya kupigia kura katika vituo vya Kiwalani, Vingunguti na baadhi ya maeneo ya Buguruni,Tabata na Kipawa ambayo Mpendazoe anadai kuwa maofisa hao walishindwa kuwasilisha matokeo ya kura zilizopigwa kama walivyotakiwa Oktoba 30 mwaka 2010 na matokeo yake maofisa hao waliwasilisha matokeo hayo Novemba 1, mwaka 2010.

‘Kwa mchanganuo hapo juu mahakama hii inakubaliana na mapingamizi ya upande wa utetezi kuwa baadhi ya aya za hati ya madai zina mapungufu ambayo yanasababisha wadaiwa kushindwa kuandaa utetezi wao na kwa sababu hiyo mahakama hii itatoa amri ya kuondolewa kwa hati ya madai ya kesi hii iende ikafanyiwe marekebisho na mdaiwa na kisha irejeshwe mahakamani hapa ndani ya siku 14 kuanzia leo na kesi hii itakuja kwaajili ya kutajwa Juni 22 mwaka huu”alisema Jaji Profesa Ibrahim Juma.

Hata hivyo Jaji huyo alitupilia mbali ombi la Dk.Mahanga lililotaka kesi hiyo ifutwe kwasababu mdaiwa aliifungua kwa mbele ya Jaji badaya Msajili wa mahakama hiyo kwa maelezo huo amelikataa ombi hilo kwasababu halina ukweli wowote kwani mlalamikaji alifungua kesi hiyo kwa kufuata misingi yote ya sheria.

Chanzo:Gazeti la Tanzania la Jumanne, Juni 7 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.