Header Ads

AG,WAZIRI WATAKA KESI YA KIKATIBA IFUTWE


Na Happiness Katabazi
MWANASHERIA Mkuu wa Serikali , waziri wa Nishati na Madini na Shirika la Umeme (TANESCO), wameiomba Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, iifukuze kesi ya Kikatiba iliyofunguliwa na wabunge watatu wa Chama cha Mapinduzi(CCM) na raia wengine wa nne dhidi yao kwa madai kuwa kesi hiyo imefunguliwa hayana mantiki ya kisheria.

Mwanasheria Mkuu,waziri wa Nishati na Madini na Tanesco ni wadaiwa katika kesi hiyo ya Kikatiba Na.5/2011 iliyofunguliwa mapema mwaka huu na Mbunge wa Jimbo la Kibakwe (CCM), George Simbachawene, Mbunge wa Karagwe (CCM), Gosbert Blandes na Mbunge wa Viti Maalumu, Angellah Kairuki chini Ibara ya 27(1) na (2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

Wengine katika orodha ya waliofungua kesi hiyo ni raia wa kawaida, Hassan Ngoma, Senkoro Izoka, Salum Kambi na Salma Shomari Mohamed, ambao wanatetewa na wakili wa kujitegemea Mpare Mpoki na Kampuni ya Uwakili ya Lukwaro, wakiliomba Jopo la Majaji watatu Jaji Njegafibili Mwaikugile, Agustine Shangwa na Projestus Lugazia kutoa amri ya kuizuia serikali isilipe fidia ya sh bilioni 94 kwa Kampuni ya Dowans Holdings SA na Dowans Tanzania Ltd.

Kesi hiyo ambayo jana ilikuja kwaajili ya kutajwa na iliarishwa hadi Julai 4 mwaka huu, Mwanasheria Mkuu wa Serikali na wenzake waliwasilisha pingamizi hilo lenye sababu sita la kutaka kesi hiyo ifutwe kwasababu maombi yaliyopo ndani ya hati hiyo ya madai hayana msingi, yameletwa mahakamani kinyume cha sheria na kwamba ubovu huo wa hati hiyo ya madai ya walalamikaji ni matumuzi mabaya ya sheria za nchi.

Kwa mujibu wa pingamizi hilo la wadaiwa ambalo Tanzania Daima inayo nakala yake walalamikaji wanaomba kesi kesi hiyo itupwe kwa gharama kwa sababu hati ya madai imekiuka taratibu na kanuni za uletaji madai ya Kikatiba kama Sheria ya Utekelezaji haki za binadamu na wajibu (Basic Rights and Duties Enforcement Act Cap 3 R.E 2000)

Sababu nyingine, wadaiwa wanaomba kesi hiyo itupwe kwasababu walalamikaji wametumia vifungu vya sheria visivyo sahihi kuwasilisha madai yao na kwamba na kwamba wadaiwa hao wameshindwa kutaja ibara zilizovunjwa na wadaiwa kwasababu kifungu cha 6 cha Sheria ya ya Utekelezaji haki za binadamu na Wajibu ambacho kinamlazimisha mlalamikaji katika kesi husika kutaja kwenye hati yake ya madai Ibara ambazo anadai mdaiwa amezivunja.

Aidha walidai hati hiyo madai ilishindishwa kumuunganisha mdaiwa mwingine muhimu ambapo hata hivyo Mwanasheria Mkuu wa serikali hakumtaja kwa jina mtu huyo.

“Kwa mapungufu hayo yaliyokuwepo kwenye hati ya madai ya walalamikaji, ndiyo maana sisi wadaiwa tumewasilisha pingamizi hilo lenye sababu sita mahakamani na tunaomba kesi hiyo itupiliwe mbali kwa gharama kwasababu hati hiyo ya madai ya Kikatiba ina udhahifu mwingi wa kisheria” alidai Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Mapema mwaka huu, wabunge wa tatu wa CCM na wananchi wa kawaida wa nne walifungua kesi ya Kikatiba mahakamani hapo chini ya Ibara ya 26(2) inasema: “Kila mtu ana haki, kwa kufuata utaratibu uliowekwa na sheria, kuchukua hatua za kisheria kuhakikisha hifadhi ya Katiba na sheria za nchi.”

Ibara ya 27(1) inasema: “Kila mtu ana wajibu wa kulinda mali asilia ya Jamhuri ya Muungano, mali ya mamlaka ya nchi na mali yote inayomilikiwa kwa pamoja na wananchi, na pia kuiheshimu mali ya mtu mwingine.”

Ibara ya 27(2) inasema: “Watu wote watatakiwa na sheria kutunza vizuri mali ya mamlaka ya nchi na ya pamoja, kupiga vita aina zote za uharibifu na ubadhirifu, na kuendesha uchumi wa taifa kwa makini kama watu ambao ndio waamuzi wa hali ya baadaye ya taifa lao.”

Walalamikaji hao kwa mujibu hati yao ya madai wanaiomba mahakama itoe amri ya kuizuia serikali isiilipe kampuni ya Dowans na endapo malipo hayo yatafanywa kwa kampuni hiyo ni wazi wadaiwa hao ambao wanaiwakilisha serikali kwa ujumla watakiwa wamevunja ibara hizo za Katiba ya nchi ambayo mahakama hiyo ina wajibu wa kuilinda ibara hizo zisivunjwe.


Simbachawene anadai kuwa tuzo iliyotolewa na ICC kwa Dowans Novemba 30 mwaka 2010, inakwenda kinyume cha Katiba ya nchi na inajaribu kufuja fedha za umma.Na tuzo hiyo ipo kinyume cha sheria kwa madai kuwa inakinzana na maazimio ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambalo kupitia mjadala juu ya ripoti ya kamati teule ya Bunge kuhusu mkataba tata wa TANESCO na Richmond, liliwahi kuweka wazi kwamba mkataba huo ulikuwa ni batili.

Aidha, alidai kuwa tuzo hiyo Dowans ikilipwa itakuwa ni kwenda kinyume cha sera za nchi na kwamba haiwezi kutekelezwa na mahakama za Tanzania.

“Kwa sababu hizo hapo juu tunaomba mahakama hii itoe amri ya kuwazuia wadaiwa wasijaribu kulipa fidia hiyo kwa Kampuni ya Dowans kwa sababu tuzo hiyo ni batili kisheria, inakinzana na maazimio ya Bunge na haiwezi kusajiliwa na mahakama za hapa nchini na inakwenda kinyume cha sera za nchi na kitendo cha kuilipa fidia kampuni hiyo basi ni wazi serikali itakuwa imevunja Katiba ya nchi”, alidai Simbachawene.

Simbachawene na wenzake wanaeleza kuwa mdaiwa wa kwanza ambaye ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), ni mshauri wa sheria wa serikali na mdaiwa wa pili ni waziri wa Wizara ya Nishati na Madini, ambaye ndiye mwenye jukumu la mdaiwa wa pili la masuala ya umeme.

Kwamba Juni 21 mwaka 2006 mdaiwa wa tatu (Tanesco) chini ya maelekezo ya mdaiwa wa pili (waziri) waliingia mkataba na Kampuni ya Richmond Develepment Company LLC ya Texas Marekani kwa makubaliano yaliyojulikana kama “Power Off Take Agreement” wa kusambaza umeme wa megawati 100.

Lakini Kampuni ya Richmond ilidanganya na haikuweza kuzalisha umeme huo kwa wakati na wakati wanaingia mkataba huo hakukuwa na mwanasheria wa Serikali ya Tanzania wala wa Marekani.

Hati hiyo ya madai inasema, kwa kitendo hicho mdaiwa wa pili ambaye ni Waziri wa Nishati na Madini alikuwa amevunja kifungu cha 38,31(1)(a) na 31(1)(b) na 31(2) ,42(a) na 59(1) vya Sheria ya Manunuzi ya Umma ya mwaka 2004.

Kwa maana hiyo utaratibu wote wa kuipatia tenda kampuni hiyo ulikuwa batili na ulikiuka vifungu hivyo vya sheria ya manunuzi ya umma.

Akiendelea kuchambua makubaliano yaliyoingiwa, alidai kuwa Kampuni ya Richmond ilipaswa kuanza kusambaza umeme ndani ya siku 150 kuanzia siku ambapo mkataba baina ya Tanesco na kampuni hiyo ulisainiwa, ambayo ni Juni 23 mwaka 2006 na muda wa kuanza kazi hiyo kwa mujibu wa makubaliano ulikuwa ni Februari 2 mwaka 2007.

Walalamikaji hao walidai tangu hapo hadi Desemba mwaka 2006 Kampuni ya Richmond ilishindwa kutekeleza kwa vitendo makubaliano hayo hali iliyosababisha mdaiwa wa tatu (Tanesco) kuandika barua kwa mdaiwa wa pili (waziri) ya kumwomba avunje mkataba huo kwa sababu Richmond imeshindwa kutimiza makubaliano waliyokubaliana na kwamba uthibitisho wa barua hiyo wanao.

Pia walidai kuwa Spika wa Bunge aliyepita, Samuel Sitta, Novemba 2007 aliunda Kamati ya Bunge kuchunguza tuhuma kuhusu mkataba huo, ambapo kamati hiyo ilibaini kampuni hiyo haikuwa na uwezo wa kuzalisha kiwango hicho cha umeme, na taratibu za upatikanaji wa tenda zilikiukwa, hivyo kusababisha aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Lowassa, mawaziri waliowahi kuongoza Wizara ya Nishati na Madini Dk. Ibrahim Msabaha na Nazir Karamagi kujiuzulu nafasi zao za uwaziri.

Januari 25 mwaka huu, Dowans iliwasilisha ombi lake la kutaka Mahakama Kuu ya Tanzania ambalo limepewa Na. 8/2011 iisajili tuzo waliyopewa na Mahakama ya ICC na siku chache baadaye Tanesco, LHCR na Timothy Kahoho wakawasilisha hati ya nia ya kupinga ombi hilo la kutaka tuzo hiyo isajiliwe. Kesi hiyo ambayo imekwisha kuanza kusikilizwa mbele ya Jaji Emilian Mushi, itakuja tena kwa ajili ya kutajwa Julai 28, mwaka huu.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Juni 22 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.