Header Ads

KAMPENI AFYA YA UZAZI WA MAMA,MTOTO IWE ENDELEVU


Na Happiness Katabazi

JANA Tanzania ilizindua Kampeni ya kitaifa la Afya ya uzazi wa mama na mtoto katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam na kudhuriwa na mamia ya watu.

Kampeni hiyo ambayo ni ya kwanza kuzinduliwa hapa nchini chini na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk.Haji Mponda tayari imeshazinduliwa katika baadhi ya nchi za Jumuiya ya Afrika Masharki.Na kuzinduliwa kwa kampeni hizo ni utekelezaji wa azimio la nchi wanachama wa umoja wa Afrika ambao waliazimia kila nchi mwanachama wa umoja huo kuakikisha inaongeza kasi ya kupunguza kasi ya vifo vya uzazi na watoto.

Kauli mbiu ya uzinduzi huo ni “Kuongeza kasi ya kupunguza vifo vinavyotokana na matatizo ya uzazi na vifo vya watoto”:Kampeni hiyo ambayo imefadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya Watu(UNFPA).

Fukuto la Jamii kwanza linaanza kwa kutoa pongezi kwa uongozi wa nchi hii kuzindua kampeni hiyo kwani hakuna ubishi ni ukweli ulio wazi vifo vinavyotokana na matatizo ya uzazi na vile vya watoto wadogo chini ya miaka miatano vinatokea sana hapa nchini.

Na ukitaka kuthibitisha matukio hayo ni kupitia takwimu mbalimbali za kitaifa na ukilazwa katika wodi ya wazazi au wodi ya watoto, vifo vya aina hiyo utokeo.

Kwakuwa mwandishi wa safu hii ni mama wa mtoto wa mmoja aitwaye Queen Kissa Mwaijande ‘Malkia’ ambaye kesho Juni 8 anatimiza umri wa miaka mitatu,ni shuhuda wa vifo vya aina hiyo kwani kama mtoto wa kike mwaka 2008 nilibeba ujauzito na likuwa nikiudhulia kwenye kliniki ya wajawazikama mama niliwahi kubeba ujauzito na nilipokuwa nikiudhuria kliniki ya Mwenge inayomilikiwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi (JWTZ) na kisha kwenda kujifungulia katika Hospitali Kuu ya Jeshi Lugalo kikosi cha 521 kinachoongozwa na Meja Jenerali, Salim Salim.

Na katika kuudhulia kliniki hapo ambapo wanawake wajawazito upata fursa ya kufundishwa jinsi ya kuweza kuulea ujauzito kwa kufuata kanuni ya kitabibu na kuchukua taadhali mapema pindi tunapojigundua tuna dalili mbaya kuwahi hospitalini.

Na ikumbukwe tayari taifa letu lina sera inayotamka bayana kuwa mtoto mwenye umri wa chini ya miaka mitano anapaswa kutibiwa bure.

Na baada ya kujifungua mwanangu Queen salama, niliendelea kumlea vizuri kwa kuzingatia maelekezo ya madaktari na manesi wa Hospitali ya Lugalo.Lakini Juni mwaka jana, mwanangu Queen alilazwa hospitalini hapo kwa takribani wiki tatu akisumbuliwa na ugonjwa Rimonia.Kwa kweli nilichanganyikiwa sana lakini kwa nguvu za mungu na jitihada za madaktari wa Lugalo ziliweza kumwokoa uhai wake.

Kwa kipindi hicho cha wiki mbili nilicholazwa pale katika Wodi ya Watoto Hospitali ya Jeshi Lugalo, niliweza kushuhudia watoto wadogo waliokuwa wakiumwa sana majumbani kwao wakifikishwa hospitalini hapo hata usiku wa manane wakiwa wamecheleweshwa kuletwa hospitali hapo kupatiwa matibabu wakifika moja kwa moja wodini na kabla ya kuanza kupatiwa matibabu walikuwa wakikata roho kabla ya kuanza kupatiwa matibabu.

Na wengine watoto wadogo ambapo walikuwa wakiletwa wodi hapo wakiwa katika hali mbaya ambapo baadhi ya madaktari na manesi walipokuwa wakiowaona tu watoto hao, manesi na madaktari hao walikuwa wakiwaeleza wazazi watoto hao kuwa hospitali hiyo haina uwezo wa kuwatibia na badala yake walikuwa wakiwapatia msaada wa nesi mmoja na gari la kubebea wagonjwa(Ambulance) ili wawakimbize kwenye Hospitali ya Rufaa ya Muhimbili kwa matibabu.

Pia kuna baadhi ya wanawake wajawazito ambao hadi wanaujauzito wenye umri wa miezi saba wanakwepa kwenda kuanza kliniki kwa kisingizio eti cha hofu ya kutakiwa kupimwa ukimwi.Wakati huo huo wataalamu wa afya wanashauri mama mwenye ujauzito anapaswa aanze kwenda kliniki tangu mimba ikiwa na umri wa kuanzia miezi minne.

Aidha pia kumekuwepo na tuhuma zinazoelekezwa moja kwa moja kwa baadhi ya wakunga katika baadhi ya hospitali za serikali kuwa wamekuwa wakichangia wajawazito kupoteza maisha yao kwaajili ya uzembe au kudai rushwa.

Lakini kuna wakina mama ambao watoto wao kweli walikuwa wakiumwa sana lakini waliwawahisha kuwafikisha hospitalini hapo na waliweza kupokelewa na kupatiwa matibabu ama wengine ulazwa au wengine utibiwa na kurudi majumbani kwao.

Kama ilivyohada ya manesi na madaktari kila siku nasema kazi yao ni wito,pindi wanapobaini wazazi wamewachelewesha watoto kuwaleta hospitali hawasiti kuwasema waziwazi na kuwataka waachache na tabia hiyo kwani wao wanaamini vifo vingi vinavyotokana na uzazi na watoto wadogo huweza kudhuirika kama kila mmoja wetu atafuata ushauri unatolewa wahudumu ya sekta ya afya.

Kwahiyo basi utaona basi licha ya serikali yetu kuwa na sera hiyo inayoruhusu watoto wote chini ya miaka mitano kutibiwa bure lakini kuna watoto wa umri huo wanaugulia majumbani na wazazi wao wapuuzia kuwapeleka hospitalini hadi mwisho wa siku watoto hao wasiyo na hatia wanajikuta wakikatishwa uhai wao kwaajili ya uzembe wa wazazi.Sisi kama wazazi tuache hii tabia.

Kwani miongoni mwa vigezo vinachokulia kuipima nchi fulani ni maskini, ni pamoja na vifo vingi ikiwemo vifo vya watoto.Kwahiyo kama taifa letu limeridhia kuzindua kampeni dhidi ya afya ya uzazi na mtoto ni wazi sasa kuanzia sasa tukaongeza kasi kwa pamoja kuakikisha kutokomeza vifo vya aina hiyo ambavyo kwa mujibu wa wanataaluma ya afya wanasema vifo hivyo vinaepukika.

Fukuto la Jamii linatoa dira ya kuona jinsi gani ya kampeni hiyo inaweza kufanikiwa na mwisho wa siku taifa letu likajikuta likudhiti vifo hivyo kwa kiwango cha juu. Mosi; ni kupitia vyombo vya habari ambapo kama wahusika wa kampeni toka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ambao miongoni mwao ni Mkurugenzi Msaidizi Afya na Elimum Dk.Godfrey Kiangi, Meneja Programu ya Afya ya Mtoto Dk.Georgina Msemo na Dk.E.Mapella na wafadhili wa kampeni hiyo UNFP kuakikisha wanashirikiana kitaaluma kupitia vyombo vya habari naamini mwisho wa siku jamii itafahamu umuhimu wa kampeni hiyo.

Na sisi vyombo vya habari kama wanazalendo wa taifa hili na ambao tunapenda kuona taifa letu likiondokana na tatizo hilo mbalo linakatisha uhai wa mama na mtoto ni jukumu letu sasa kuakikisha tunazipa umuhimu pia habari na makala zinazoelimisha kuhusu afya ya uzazi wa mama na mtoto ili jamii ibadilike na kuona haja ya kukabiliana na tatizo hilo.

Kama sisi vyombo vya habari tutabadilika kwa dhati na kuanza kuona haja ya kuzipa uzito na umuhimu habari zinazohusu jamii yetu moja kwa moja kama tunazipaka umuhimu kila kukicha habari za kisiasa na burudani, ni wazi kabisa mashirika mbalimbali na wananchi wenye fedha watajitokeza kutoa michango yao ya hali na mali itakayowezesha majengo ya wodi za watoto wa changa wa chini ya umri wa miezi mitatu katika hospitali nyingi za wilaya na mikoa.

Kwani hali ilivyo hivi sasa karibu hospitali nyingi ziwe za serikali na zile binafsi hazina wodi maalum ya kuwalaza watoto wa changa wenye umri wa miezi mitatu kushuka chini.Na matokeo yake watoto hao wachanga hao ta waliozaliwa siku nne zilizozipita wakiugua na kufikia hatua ya kulazwa ,ulazwa katika wodi ya watoto wenye umri wa chini ya miaka 10 kushuka chini.

Sote tunafahamu kuwa watoto wachanga ni wepesi sana kushambuliwa na magonjwa yoyote sasa inapotokea mtoto mchanga analazwa kwenye wodi ya watoto wenye maradhi mengine ambayo hatutarajii mtoto huyo mchanga ayapate kwa umri wake huo, ujikuta anaweza kuambukizwa magonjwa hayo haraka iwezekanavyo.

Hivyo basi sisi vyombo vya habari hasa wahariri katika vyumba vyetu vya habari kuakikisha vinatoa kipaumbele kwa habari za aina hiyo za kuwaelimisha umma kuhusu kampeni hiyo ili mwisho wa siku nchi yetu iweze kuondokana na tatizo hilo.Nanina imani kabisa kama habari kuhusu kampeni hii zitapewa umuhimu, pia wanasiasa wetu nao wataona haja ya kuanza kulipigia chapua tatizo hilo ili mwisho wa siku serikali iongeze bajeti katika kukabiliana na janga hili.

Hakuna ubishi kwamba wanasiasa wetu tena kuanzia ngazi ya taifa hadi wilayani wamekuwa vinara sana wakuongoza harambee za kuchangia matamasha ya Injili,harambee za kuchangia kampeni za vyama vyao,ujenzi wa mashule na mambo mengine lakini siwaoni wanasiasa hasa wanasiasa wanawake wakielekeza nguvu zaidi katika kukabiliana na tatizo hilo na hivyo basi wakati umefika kwa wanasiasa kuelekeza nguvu katika afya ya uzazi wa mama na mtoto.

Ikumbukwe sote tulikuwa watoto tukalelewa vizuri na kwa umakini wa hali ya juu na ndiyo maana leo hii tumekuwa wakubwa tunaweza kujitegemea na kujieleza mbele ya madaktari kwamba tunaumwa nini.Sasa inakuwaje baadhi ya wazazi wanasahau wazazi wao waliwaangalia vyema walipokuwa watoto wadogo na kushindwa kuwafikishwa kwa wakati hospitalini watoto wao wadogo wanapougua?

Sisi watu wazima wa leo ifike mahali tujiulize kuwa Je tusingeangalia vyema na kufikishwa mahospitalini kupata tiba kwa wakati, tungefika hapa tulipo? Kwa hiyo tulitendewa haki na kuangaliwa vizuri na walezi na wazizi wetu hadi leo tumefikia hapa tulipofikia, inakuwaje miongoni mwetu tushindwe kuwatendea haki watoto wetu kwa kuwapeleka mahospitalini kwa wakati?

Nyie manesi ambao mnalalamikiwa kukiuka miiko yenu ya taaluma hadi wakati mwingine mnasababisha vifo vya wajawazito, Je na nyie kipindi kile mama zenu wakati wamebeba ujauzito wenu tumboni wangefika hospitalini na wauguzi waliokuwa wakiwahudumia wangekiuka miiko ya taaluma yao kwaajili ya kudai rushwa,mngekuwepo duniani nyie kama si nyie na mama zenu mngekuwa mmekufa na uzazi?

Ikumbukwe kuwa Ibara ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, inatamka bayana kuwa. “Kila mtu anayo Haki ya Kuishi na kupata kutoka katika jamii hifadhi ya maisha yake, kwa mujibu wa sheria.”.

Kwa hiyo kimsingi tukubaliane haki ya kuishi imetamkwa kwenye Katiba yetu na hivyo ni wajibu wa kila mmoja wetu kwa nafasi yake kuakikisha anailinda haki hiyo bila kuivunja.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Juni 7 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.