Header Ads

WASHTAKIWA SAMAKI WA MAFUGULI HAWANA HATIA-MAWAKILI

Na Happiness Katabazi
UPANDE wa utetezi katika kesi ya uvuvi haramu katika kina kirefu cha Bahari ya Hindi maarufu kama kesi ya ‘Samaki wa Magufuri’inayowakabili raia 36 wa kigeni, umeiomba Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, uwaone washtakiwa wote hawana kesi ya kujibu kwasababu upande wa Jamhuri umeshindwa kuthibitisha kesi yao.

Maombi hayo yalitolewa Juni 16-17 mwaka huu na mawakili wa washtakiwa Ibrahim Bendera na John Mapinduzi mbele ya Jaji Agustine Mwarija wakati kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya upande wa utetezi kuwasilisha majumuisho ya kesi hiyo yanayowaona washtakiwa hao hawana kesi yakujibu kwa njia ya mdomo ambapo upande wa jamhuri nao utawasilisha majumuisho yao Juni 20 mwaka huu.

Wakili Bendera alianza kwa kuikumbusha mahakama kuwa Sheria mama ya Uvuvi katika kina kirefu(The Deep Sea Fishing Authority) Act Cap 388 ilitakiwa ianze kazi kwa tango la Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi wakati huyo alikuwa John Magufuri ambalo waziri huyo alilitangaza kwenye gazeti la serikali Na.138 , Agosti 15 mwaka 2009 na akaisaini tangazo hilo Julai 21 mwaka 2009 na waziri huyo ndani ya tangazo hilo akasema sheria hiyo mama itaanza kufanyakazi Julai 1 mwaka 2008.

Bendera alidai kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Tanzania ya Kutafsiri Sheria (Interpretation of Laws Act Cap 1) kifungu cha 17 kinatoa mamlaka kwa waziri yoyote katika tangazo lake la kutaka sheria mama anayoitunga ianze kazi kabla ya tarehe aliyoisaini tofauti na sheria ndogo ndogo ambazo zinaweza kuanza kutumika kabla ya waziri kusaini sheria hiyo.

“Kwa maelezo hayo hai niliyoyatoa hapo juu kwamba sheria hiyo iliyotumika kuwafungulia mashtaka washtakiwa ilitungwa kabla ya washtakiwa kukamatwa na kwa maana hiyo wakati washtakiwa hao wanakamatwa Machi 7 mwaka 2009 Tanzania ilikuwa haina sheria hiyo.Waziri Magufuri alisaini tangazo Julai 21 mwaka 2009 na kusema sheria hiyo itaanza kufanyakazi Julai 1 mwaka 2008….kwa hiyo mheshimiwa Jaji sisi tunasema waziri alikosea kufanya hayo aliyoyafanya kwani duniani kote siku sheria inapo saini ndiyo siku hiyo inapoanza kufanyakazi sasa huyu waziri kasaini sheria hiyo mwaka 2009 halafu tena kwa maandishi anasema sheria hiyo itaanza kutumika kuanzia mwaka 2008”alidai wakili Bendera.

Aidha alidai kifungu cha 3 cha Sheria ya Uvuvi katika kina kirefu, inasema mtu mwenye mamlaka ya mwisho kwenye shughuli zote za meli ya uvuvi ni keptaini lakini cha kushanga upande wa Jamhuri umewakamata na kuwafungulia kesi hata wapishi na wafagizi wa meli ya Tawariq 1 ambao ni miongoni wa washtakiwa katika kesi hiyo.

Aliendelea kudai kuwa sababu nyingine ya kutaka mahakama hii iwaone hawana kesi ya kujibu ni kwamba mashahidi wote 13 wa upande wa Jamhuri walieleza mahakama kuwa meli hiyo haikuwa na usajili, bendera ya taifa lililotokea,ambapo alidai kuwa mashtaka yanayowakabili washtakiwa hao ni uvuvi kwenye kina kirefu cha bahari ya hindi hila leseni na kuchafua mazingira katika eneo hilo na kwamba jamhuri hawakuwashtaki washtakiwa hao kwamba walikuwa wakiendesha meli hiyo ikiwa haina bendera wala kuwa na usajili na kwamba washtakiwa ambao ni wapishi na wafagizi hawawezi kufahamu hati ya usajili ipo wapi na wala meli hiyo kama ina bendera.

Aidha aliendelea kuchambua kuwa Sheria ya Kimataifa ya Mambo ya Bahari ,inaitaka nchi yoyote inayotoa kutoa uhuru kwa vyombo vinavyopita baharini kama meli kupata haki stahili na pindi nchi moja inapobadili au kutungusha sheria kuhusu mambo ya bahari nchi hiyo italazimika kutoa taarifa na kuisambaza sheria hiyo kwa nchi wanachama ili waielewe sheria hiyo inasemaje na kuongeza kuwa kwa muktadha huo hadi washtakiwa hao wanakamatwa serikali ya Tanzania haikuwa imesambaza sheria hiyo kwa nchi wanachama.

Hata hivyo alidai kwa mujibu wa vielelezo na mashahidi wote 13 wa Jamhuri waliotoa ushahidi, hakuna shahidi hata mmoja aliyetoa ushahidi unaothibitisha kuwa aliwaona washtakiwa hao na meli ya Tawariq 1 walikuwa wakivua samaki na kuaribu mazingira katika kina kirefu cha Bahari ya Hindi katika Ukanda wa Tanzania na kuongeza kuwa anaomba mahakama hiyo iwaaone washtakiwa wote hawana kesi ya kujibu na hivyo iwaachilie huru.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatatu, Juni 20 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.