Header Ads

JK KUZINDUA KAMPENI YA AFYA UZAZI,MTOTO

Na Happiness Katabazi

RAIS Jakaya Kikwete anatarajia kuwaongoza Watanzania kuzindua kampeni ya kitaifa ya afya uzazi na mtoto katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.


Akizungumza na waandishi wa habari jana wakati wa mafunzo kuhusu namna ya kuripoti habari za afya ya uzazi na mtoto, Mkurugenzi Msaidizi wa Afya na Elimu Dk. Godfrey Kiangi alisema kampeni hiyo inafanyika kitaifa.

Alisema tayari kampeni hizo zimezinduliwa kwenye baadhi ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Masharki na kuongeza kuwa kampeni hiyo itaendelea kuzinduliwa kwa nchi nyingine barani Afrika kwa kuwa tafiti zimebaini kwamba tatizo la afya ya uzazi na mtoto ni kubwa kwa nchi zinazoendelea.

Dk.Kiangi alisema ujumbe wa kampeni hiyo ni ‘Kampeni ya kuongeza kasi ya kupunguza vifo vinavyotokana na matatizo ya uzazi na vifo vya watoto’ baada ya uzinduzi huo wizara itaendelea kufanya uzinduzi kwa ngazi ya mikoa na wilaya zote.

Kwa upande wake Meneja Mpango wa Afya ya Mtoto kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Dk. Georgina Msemo alisema siku ya uzinduzi wizara itaweka mabanda yatakayotoa huduma ya afya ya uzazi, uchangiaji damu kwa hiari na watu kupima ukimwi kwa hiari.

Aidha Dk. Msemo aliviomba vyombo vya habari kuwa mstari wa mbele kuandika habari za afya ya uzazi na mtoto ili jamii ibadilike na kuanza kuchangia katika kuboresha afya ya uzazi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Juni 3 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.