Header Ads

WASHTAKIWA WA UNYANG'ANYI WAGOMA KWENDA KORTINI

Na Happiness Katabazi

MAHABUSU watano kati ya tisa wanaokabiliwa na kesi ya unyang’anyi wa kutumia silaha na kuiba ya milioni 233 katika duka la kubadilishia fedha za kigeni la Maxson Bureau Change jana waligoma kwenda katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam.

Watuhumiwa hao waliamua kutohudhuria kesi yao hiyo wakishinikiza kuonana na uongozi wa juu wa mahakama nchini kwa lengo la kuwaeleza matatizo yanayowakabili.

Mahabusu hao kuanzia juzi walianza mgomo wa kutokula chakula na jana kuendeleza mgomo huo kwa kukataa kwenda mahakamani kushinikiza kutekelezwa kwa takwa lao.

Waliogoma kufika mahakamani hapo ni Martin Mndesha, John Mndesha, Mashaka Pastor, Erick Mfinanga na Lucas Nyamaira watuhumiwa wote tisa wanatetewa na wakili wa kujitegemea Majura Magafu.

Mbele ya Hakimu Mkazi Frank Moshi, wakili Magafu alidai kuwa kesi hiyo ilikwenda mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa lakini wateja wake wamemweleza kuwa washtakiwa wengine watano wamegoma kwenda mahakamani kwa madai wanahitaji kuonana na uongozi wa mahakama.

Watuhumiwa waliofika mahakamani hapo jana ni Jafari Mkenda, Philip Mushi, Hussein Masoud na Rashid Eliakimu.

Magafu alidai wateja wake wanahitaji kuonana na Jaji Kiongozi Fakhi Jundu au Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kwasababu upande wa jamhuri katika kesi hiyo umekuwa ukiwatendea mambo yanayokiuka haki ikiwemo kutopeleka mashahidi mahakamani.

“Kesi hii ina miaka mitano sasa tangu ifunguliwe hapa mahakamani na bado haijamalizika na ni mashahidi wawili tu wanaoishi Arusha ndiyo wametoa ushahidi, mashahidi wengine tena wanaishi hapa hapa jijini hawaji mahakamani kutoa ushahidi wakati washtakiwa wanaendelea kusota gerezani.” Hakimu Mkazi Frank Mosha, alisema amesikia malalamiko hayo ila yeye siyo hakimu anayesikiliza kesi hiyo hivyo hawezi kutolea maamuzi maombi hayo na kwamba ataakikisha anayafikisha mkwa hakimu Katemana.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Juni 15 mwaka huu, itakapopelekwa mahakamani hapo kwaajili ya kutajwa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Juni 8 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.