Header Ads

HAKIMU KORTINI KWA RUSHWA DAR

Na Happiness Katabazi

HAKIMU wa Mahakama ya Mwanzo Ukonga jijini Dar es Salaam, Ndevera Kihangu na wenzake wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na makosa ya kushawishi na kupokea rushwa ya sh 100,000.


Mbali na Hakimu Kihangu, washitakiwa wengine ni karani wa hakimu huyo, Eveline Mowo na mhasibu wa mahakama hiyo, Victoria Mtasiwa.

Wakili wa Serikali, Salha Abdallah, mbele ya Hakimu Mkazi, Ritha Tarimo, alidai washitakiwa wanakabiliwa na makosa matatu ya kushawishi na kuomba rushwa ya kiasi hicho cha fedha.

Alidai kosa la kwanza ambalo linamkabili mshitakiwa wa kwanza na wa pili ni kuwa Aprili 24 mwaka huu, katika Mahakama ya Mwanzo Ukonga washitakiwa hao walimshawishi Joyce Msaki awapatie kiasi hicho cha fedha ili wampatie dhamana katika kesi inayomkabili iliyopo katika mahakama hiyo.

Wakili Abdallah alidai kuwa kosa la pili ni la kupokea rushwa ya sh 40,000, ambalo linamkabili mshitakiwa wa kwanza na wa pili. Siku hiyo walipokea kiasi hicho cha fedha kama kianzio cha kumpatia dhamana.

Alidai kosa la tatu ambalo linawakabili washitakiwa wote ni kuwa Mei 27 mwaka huu katika mahakama hiyo, washitakiwa hao walipokea tena sh 60,000 kutoka kwa Msaki.

Washitakiwa wote walikana mashitaka na washitakiwa wawili ambao ni Hakimu Kihengu na Mhasibu Victoria walipata dhamana baada ya kutimiza masharti huku mshitakiwa Mowo alipelekwa mahabusu kwa kushindwa kutimiza masharti na kesi hiyo imeharishwa hadi Juni 22, mwaka huu.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Juni 9 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.