Header Ads

HAKIMU ADAIWA KUKOSEA KUTOA DHAMANA

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa Jamhuri jana umeiambia Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kuwa unakubaliana na hoja za mawakili wa utetezi katika kesi ya matumuzi mabaya ya ofisi ya umma inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Benki Kuu, Simon Jengo, na wenzake kwamba Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Agnes Mchome, alikosea kisheria kutoa masharti ya dhamana kwa washitakiwa hao.


Mbali na Jengo, washitakiwa wengine ni aliyekuwa Naibu Mkurugenzi wa Fedha za Nje, Kisima Mkango na Mkurugenzi wa Huduma za Benki Kuu, Ally Bakari, ambao wanatetewa na mawakili Mabere Marando na Richard Rweyongeza.

Wakili Mwandamizi wa Serikali, Timon Vitalis, aliyekuwa akisaidiana na Ephrey Sedekia, mbele ya Jaji Emilian Mushi, aliiambia mahakama kuwa upande wa jamhuri unakubaliana na ombi lilowasilishwa mbele yake na mawakili wa utetezi la kutaka mahakama hiyo ipitie upya masharti ya dhamana yaliyotolewa Mei 7 mwaka huu, na mahakama ya wilaya ya Ilala.

“Upande wa Jamhuri tunaunga mkono hoja za mawakili wa utetezi kwamba Mahakama ya Wilaya ya Ilala, ilikosea kutoa masharti ya dhamana kwa washitakiwa hao kwa matakwa ya kifungu hicho, kisheria na kwa mujibu wa kesi inayowakabili washitakiwa, Hakimu Mchome alipaswa atoe masharti ya dhamana kwa mujibu wa kifungu cha 148(6) cha Sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, ambacho kinatamka mshitakiwa wa kesi kama hii ili apate dhamana asalimishe hati ya kusafiria mahakamani, asitoke nje ya mji anaoishi hadi aombe kibali,” alisema wakili Timon Vitalis.

Awali wakili Marando na Rweyongeza walimweleza Jaji huyo wao hawakubaliani masharti ya dhamana ya Mahakama ya Ilala na ndiyo maana wakawasilisha ombi hilo Mahakama Kuu,walidai kuwa kwa mujibu wa hati ya mashtaka inaonyesha kosa linalowakabili washtakiwa la matumuzi mabaya na siyo shtaka la wizi wala kusababisha hasara.

“Sisi tunasema hakimu Mchome hakuisoma vizuri hati ya mashtaka na ndiyo maana akatoa masharti ya dhamana kwa wateja wetu kinyume cha sheria ..kwani hata hiyo hati ya mashtaka imejieleza wazi kabisa kwa kutaja idadi ya noti zilizochapwa na siyo thamani ya noti hizo “alidai Wakili wa utetezi Mabere Marando

Kwa upande wake, Jaji Mushi alisema amesikiliza hoja za pande zote mbili na akazitaka zifike mahakamani hapo Juni 11 mwaka huu, kwa kuwa siku hiyo ndiyo atatoa uamuzi wa ombi hilo na kuamuru washitakiwa warudi rumande.

Mei 7 mwaka huu,Mahakama ya Wilaya ya Ilala iliwafutia kesi kesi ya uhujumu uchumi na kuisababishia serikali hasara ya Sh bilioni 500.Licha ya kuwafutia mashtaka wagurungezi hao walijikuta wakikamatwa tena baada ya kutuhumiwa mashtaka matatu ya matumuzi mabaya ya ofisi ya umma.

Wakili Sedekia, alidai mahakamani hapo kuwa washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka matatu, ambapo kosa la kwanza walilifanya 2004, kwa kuchapisha noti zenye thamani ya sh milioni 500.
Wakili Sedekia, alidai shtaka la pili linafanana na la kwanza ambapo wanadaiwa kutumia nyaraka hizo kumdanganya mwajiri wao ili aweze kuongeza gharama za uchapishaji wa noti zenye thamani hiyo mwaka 2005.

Aidha, wakili alidai shtaka la tatu ni la kutumia madaraka yao vibaya, ambapo watuhumiwa hao kwa pamoja wakiwa na nafasi zao, waliongeza gharama za uchapishaji wa noti zenye thamani ya sh bilioni 1.4 mwaka 2007.

Wakati huo huo Jaji Elian Mushi alisikiliza ombi la kupatiwa lilowasilishwa na mahakamani hapo na Mhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani Michael Wage Karoli na maofisa wenzake tisa ambao wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi na kuisababishia hasara halmashauri hiyo ya Sh 850,108,137 na kusema kuwa Juni 11 mwaka huu, atatoa uamuzi kuhusu ombi hilo.

Mbali na Karoli washtakiwa wengine ni Godwin Mwambashi ambaye Mhasibu, Suleiman Kitenge ambaye ni ofisa Afya
,Felix Ngomano ambaye ni Mhandisi,Cheka Omari ,Aloyce Gabrile ambaye ni Ofisa Mipango, Alex Mwakawago ambaye Ofisa elimu ,Rhoda Nsemwa ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji na Abdul Mwinyi ambaye ni Mhasibu wa Ndani.Washtawakiwa wote ni watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo na wanatetewa na mawakili wa Edgi Mkoba,Ruthi Chiloma ,Asha Nassoro na Juma Nyamugaruri.

Akiwasilisha hoja za upande wa utetezi wakili Mkoba alidai kuwa wateja wake kesi ya msingi inayowakabili wateja wake imefunguliwa katika Mahakama ya Wilaya Bagamayo na kwa mujibu wa sheria mahakama hiyo haina mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo wala kutoa masharti ya dhamana na ndiyo wakaamua kuwasilisha ombi hilo la kutaka wateja wake wapatiwe dhamana katika mahakama yake.

Wakili Mkoba alidai kuwa ukiisoma hati ya mashtaka inaonyesha washtakiwa walitenda makosa katika mwaka wa fedha wa Julai 2000-Februali 2010 jambo ambalo ni la kushangaza kwani kipindi hicho chote ni mwaka mmoja wa fedha na wala mwaka wa fedha bado haujaisha hivyo ni wazi hata hiyo halmashauri bado haijafanya ukaguzi wa mahesabu yake ili uweze kubaini kuna fedha ziliibwa au walipata hasara.

Mei 5 mwaka huu, washtakiwa hao walifikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Wilaya ya Bagamoyo wakikabiliwa na mashtaka mawili.Shataka la kwanza ni la kula njama ambalo linawakabili washtakiwa wote.Wakati shtaka la pili,pia linawakabili washtakiwa wote pia kwamba katika mwaka wa fedha Julai 2009 –Februali 28 mwaka 2010 katika muda tofauti huku Bagamoyo mkoani Pwani ,wakiwa waajiriwa wa halmashauri ya wilaya hiyo waliiba Sh 850,108,137.

Jamhuri ilidai shtaka jingine ambalo ni shtaka mbadala wa shtaka la pili , ni shtaka la kusababisha hasara kinyumbe na kifungu cha 10(1) na (2)(a) na (b) cha Sheria ya Uhujumu Uchumi ya mwaka 2002. Kwamba washtakiwa wote kwa pamoja wakiwa watumishi ,walisababisha halmashauri hiyo ya wilaya ya Bagamoyo ipate hasara hiyo..Na toka kipindi chote hicho hadi leo washtakiwa wanaendelea kusota rumande.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi,Juni 5 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.