Header Ads

MAWAKILI:MRAMBA HANA KESI YA KUJIBU


Na Happiness Katabazi

ALIYEKUWA Waziri wa Fedha, Basil Mramba ameiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imuone hana kesi ya kujibu na afutiwe kesi inayomkabili ya matumuzi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya Shilingi bilioni 11.7 kwasababu upande wa Jamhuri katika kesi hiyo umeshindwa kuthibitisha kesi yake bila kuacha mashaka.


Mbali na Mramba anayetetewa na mawakili wa kujitegemea Hurbert Nyange na Peter Swai.Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini Daniel Yona na Katibu Mkuu Mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja ambao wanatetewa na Elisa Msuya na Cuthbert Tenga ambapo kesi hiyo inasikilizwa mbele ya Jaji John Utamwa anayesaidiwa na mahakimu wakazi Saul Kinemela na Sam Rumanyika.

Ombi hilo Mramba peke yake liliwasilishwa jana kwa njia ya maandishi na mawakili wake mahakamani hapo kufuatia amri iliyotolewa Februali 17 mwaka huu, na Jaji Utamwa ambapo alisema mwenendo wa kesi hiyo umekamilika na ukautaka upande wa utetezi uwasilishe majumuisho yao ya kuwaona hawana kesi ya kujibu jana na upande wa Jamhuri uwasilishe majumuisho yake Aprili 17 mwaka huu na endapo upande wa utetezi unataka kuwasilisha majumuisho ya nyongeza uwasilishe Aprili 30 na akaiarisha hadi Mei 2 mwaka huu, jopo hilo litakuja kuangalia kama amri hizo zimetekelezwa.

Wakili Nyange anaanza kwa kuikumbusha mahakama kuwa washtakiwa wanakabiliwa na makosa mawili ya ambayo yamegawanyika katika makosa 11 na kosa kumi ni na matumuzi mabaya ya ofisi ya umma kinyume na kifungu cha 96(1) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 na kosa la 11 ni kusababisha serikali hasara ya kinyume na kifungu 284A(1) cha Sheria hiyo ya Kanuni ya Adhabu.

Wakili Nyange alidai mawakili wa Jamhuri wanadai mshtakiwa wa kwanza na wapili (Mramba na Yona) wanadaiwa kutenda kosa la kutumia madaraka yao vibaya kwa uamuzi wao wa kuiruhusu kampuni ya Alex Stewart (Assayers)UK na kampuni mama ya Alex Stewart Government Bussiness Corporation kufanyakazi ya ukaguzi wa dhahabu hapa nchini kinyume na Sheria ya Manunuzi ya Umma Sura ya 410 ya mwaka 2002 na Sheria ya Madini Sura ya 123.

Pia walisaini makubaliano na kampuni hizo ambapo makubaliano hayo yaliiruhusu kampuni hiyo kufanya shughuli hizo hapa nchini kwa miaka miwili kuanzia Juni 14 mwaka 2005-Juni 23 mwaka 2007 bila idhini ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Nyange alidai Mramba na Mgonja wanakabiliwa na shtaka la tano, sita,saba ,nane ,tisa na kumi ambalo ni la kutoa vibali vibali sita vya msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo kinyukme na ushauri wa Mamlaka ya Mapato(TRA), ambayo TRA ilitoa ushauri kwa washtakiwa isitoe msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo na kuongeza kuwa kosa la 11 ni la kusaisababishia serikali hasara ya Sh. 11,752,350,148.00 kwa uamuzi wao wa kuipatia msamaha kutolipa kodi kampuni hiyo.

“Mheshimiwa katika makosa ya jinai ili mshtakiwa atiwe hatiani kwa kosa la jinai anayodaiwa kutenda ni lazima mambo mawili yathibitishwe na upande wa Jamhuri. Mambo hayo ni lazima ithibitike kuwa mshtakiwa walitenda kosa hilo wanalokabiliwa nalo(actus reus),na wakati akitenda kosa hilo walikuwa na nia ovu(means rea).Na kwa mujibu wa kesi hii upande wa jamhuri umeshindwa kuthibitisha vitu hivyo viwili kwa mshtakiwa kwanza na kwa sababu hiyo tunaomba mahakama imuachilie huru Mramba na imuone hana kesi ya kujibu”alidai wakili Nyange.

Akilichambua shtaka la matumizi mabaya ya ofisi ya umma, upande wa Jamhuri umeshindwa kuleta shahidi wa kuthibitisha Mramba alitenda kosa hilo.Kwa sababu Tanzania ni Jamhuri na Mtendaji Mkuu wake ni rais ambaye anafanyakazi zake kwa kusaidiwa na Baraza la Mawaziri na kuongeza kuwa pia Jamhuri imeshindewa kuleta ushahidi hata wa maandishi unaonyesha Rais Mkapa hakuridhia uamuzi wa Mramba kuipatia kampuni hiyo msamaha wa kodi na kwamba shahidi nane wa upande wa Jamhuri aliyekuwa Naibu Waziri wa Fedha,Abdisalaam Issa Khatibu katika ushahidi wake alieleza mahakama kuwa hakuna shida endapo waziri yoyote akiwasiliana na rais moja kwa moja bila bila kupitia kwa Waziri Mkuu.

Wakili Nyange alieleza kuhusu Mramba kudaiwa kutoa msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo kuwa alikiuka ushauri wa TRA alidai wamejiuliza vitu vifuatavyo . “Mramba alikuwa na mamlaka ya kutoa msamaha wa kodi?Ni taratibu zipi za kutoa vibali vya serikali msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo ?Na Mramba kutoa msamaha wa kodi ametumia madaraka yake ?Mramba alikuwa jukumu la kisheria linalomlazimisha kufuata ushauri wa TRA?Je ushauri ule wa TRA kwa kukataa Mramba asitoe msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo unampana kisheria mshtakiwa huyo?

Alikafanua kuhusu maswali hayo alidai kuwa hakuna shahidi hata mmoja wa Jamhuri aliyefika mahakamani hapo na kueleza kuwa mshtakiwa huyo hakuwa na mamlaka ya kutoa msamaha wa kodi kwa Kampuni Alex Stewart na kwamba hakuna shahidi aliyekuwa kueleza mahakama kuwa taratibu zote zilizofanywa hadi kuipatia msamahama kampuni hiyo hazikufuata taratibu za kisheria na kuwa sheria ya Kodi ina mruhusu waziri wa Fedha kutoa msamaha na kwamba shahidi wa 12 alieleza mahakama kuwa Mramba hakuwa na uhusiano wa kirafiki wala hakunufaika na na uamuzi huo wa kuisamehe kodi kampuni hiyo.

Kuhusu kosa la kusababisha hasara ya sh bilioni 11.7 alidai kama serikali ya Tanzania iliipatia msamaha wa kodi kampuni hiyo kwahiyo upande wa Jamhuri hauwezi kudai msahama huo hauwezi kusababisha upotevu wa kiasi hicho cha fedha kwa maana hiyo Jamuhiri ilipaswa ithibitishe kama kampuni hiyo ilikuwa hailipi kodi kama inavyotakiwa kisheria na kuongeza kuwa kiasi hicho kinachodaiwa kuwa ni serikali imepata hasara ni cha kufikilia na kwamba siyo cha kweli.

“Naiomba mahakama hii imfutie kesi Mramba kwasababu upande wa Jamhuri imeshindwa kuthibitisha kesi yake kwasababu ushahidi na vielelezo vilivyotolewa na mashahidi wake ni dhaifu ambao hauwezi kuishawishi mahakama hii imuone mshtakiwa ana kesi ya kujibu”alidai Wakili Nyange.

Mramba na Yona walifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Novemba 25 mwaka 2008 na hati ya mashtaka ilikuwa na jumla ya mashtaka 13.Lakini Januari 2 mwaka 2009 mshtakiwa wa tatu(Mgonja) alipounganishwa mashtaka yakapungua na kufikia 11.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Machi 28 mwaka 2008.

No comments:

Powered by Blogger.