Header Ads

KESI YA LULU YAPIGWA KALENDA

Na Happiness Katabazi MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, jana iliairisha tena kesi ya mauji inayomkabili msanii wa Filamu, Elizabeth Michael ‘Lulu’ dhidi ya aliyekuwa msanii mwenzake Steven Kanumba kwa maelezo kuwa jarada la kesi ya hilo limeitwa Mahakama Kuu. Wakili wa Serikali Lasdilaus Komanya mbele ya Hakimu Mkazi Augustino Mbando aliikumbusha mahakama kuwa kesi hiyo jana kilikuja kwaajili ya kutajwa. Kwa upande wake Hakimu Mbando alisema kesi hiyo haiwezi kuendelea mahakamani hapo kwasasa kwasababu jarada la kesi hiyo limeitwa Mahakama Kuu kwaajili kufanyiwa kazi na kwamba anaiarisha kesi hiyo Juni 4 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya kutajwa. Mei 15 mwaka huu, Lulu kupitia mawakili wake Kenned Fungamtama, Peter Kibatara, Fulgence Masawe na Joaquine De- Melon waliwasilisha ombi Na.46/2012 chini ya hati ya dharula iliyokithiri Mahakama Kuu wakiomba mahakama hiyo ya juu iamuru Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kulishughulikia ombi la msanii huyo lililokuwa likiomba kesi hiyo isikilizwe katika mahakama ya watoto kwasababu mshtakiwa huyo ana umri wa chini ya miaka 18. Mei 18 mwaka huu, uongozi wa Mahakama Kuu ukampangia Jaji Dk.Fauz Twaibu kusikiliza ombi hilo ambapo jaji huyo atalisikiliza ombi hilo Mei 28 mwaka huu mahakama hapo. Kwa mujibu wa ombi hilo la Lulu,anadai kuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu Augustina Mmbando Mei 7 mwaka huu, alikataa kulitoa uamuzi ombi la mawakili wake lilokuwa likidai kesi hiyo iamishiwe katika mahakama ya watoto kwasababu mshitakiwa huyo ana umri chini ya miaka 18 na badala yake hakimu huyo akasema mahakama hiyo haina mamlaka ya kutolea uamuzi ombi hilo na kuwashauri mawakili hao kuwasilisha ombi hilo Mahakama Kuu. Kwa mujibu wa hati hiyo ya madai wakili Fungamtama walidai kuwa hakimu Mmbando alijielekeza vibaya kwa kukusema kuwa mahakama ile ilikuwa haina mamlaka ya kusikiliza ombi lao kwahiyo wanaiomba mahakama Kuu imwelekeze hakimu huyo asilikize ombi lao na alitolee maamuzi na kuwa endapo Mahakama Kuu itabaini vinginevyo basi mahakama hiyo ya juu itoe tafsiri ya umri yake kuhusu ombi hilo. Mei 7,2012 mawakili hao waliwasilisha ombi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakiiomba mahakaam hiyo iamuru kesi ya msanii huyo isikilizwe katika mahakama za watoto wakidai kuwa bado ni mtoto. Mawakili hao walidai mahakamani hapo kuwa msanii huyo ana umri wa miaka 17 na kwamba kwa maana hiyo yeye bado ni mtoto na kesi yake haipaswi kusikilizwa katika mahakama za kawaida kama mtu mzima. Hata hivyo mawakili hao waligonga mwamba baaada ya mahakama hiyo kusema kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kutolea uamuzi ombi hilo na kuwashauri mawakili hao wapeleke ombi hilo katika mahakama kuu kwasababu mahakama ya kisutu haina mamlaka ya kuisikiliza. Katika uamuzi wake, hakimu Mmbando alisema kesi hiyo bado iko kwenye upelelezi na kwamba kulingana na jinsi ilivyo isingekuwa busara kuamua hoja yoyote. Hata hivyo upande wa Jamhuri kupitia wakili wa serikali mwandamizi Elizabeth Kaganda ulipinga maombi hayo na kudai kuwa bado wanaendelea na upelelezi wa kesi hiyo na hivyo kuomba wapewe muda zaidi. Wakili Kaganda pia alidai kuwa hata jina linaloonekana katika cheti cha kuzaliwa cha mshtakiwa huyo linasomeka kama Diana Elizabeth wakati mshtakiwa huyo ametajwa mahakamani hapo kama Elizabeth Michael. Akijibu hoja hiyo, wakili Fungamtama alikiri jina hilo kusomeka Diana Elizabeth na kudai kuwa ni jambo la kawaida hasa kwa wakristo kuwa na majina mawili. Na Lulu upo rumande kwa kosa la mauji linalomkabili halina dhamana kwa mujibu wa Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002. Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Mei 22 mwaka 2012

No comments:

Powered by Blogger.