Header Ads

KIWANJA CHA CHANG'OMBE MARKAS, SI MALI YA WAISLAMU-MASHAHIDI



Na Happiness Katabazi

MWENYEKITI wa Baraza la Wadhamini la (BAKWATA),Masoud Ikome(72), jana ameithibitishia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kiwanja kilichopo Chang’ombe Markas  ni mali halali ya kampuni ya Agritanza Ltd na siyo mali waislamu(Bakwata).

Itakumbukwa kuwa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Sheikh Issa Ponda Issa na wenzake 49 , Oktoba mwaka jana walivamia eneo la Kiwanja hicho kwa madai kuwa kiwanja hicho ni mali ya Waislamu na hivyo polisi kulazimika kuwakamata na kuwafikisha mahakamani kwa makosa mbalimbali.

Ikome ambaye ni shahidi wa nne katika kesi ya  uchochezi na wizi wa mali za sh milioni 59 inayomkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Sheikh Issa Ponda Issa na wenzake 49 ,alitoa maelezo hayo jana wakati akiongozwa na Wakili Mwandamizi wa Serikali Tumaini Kweka kutoa ushahidi wake ,kwasababu jana kesi hiyo ilikuwa imekuja kwaajili ya kuendelea kusikilizwa na Hakimu Mkazi Victoria Nongwa.

Ikome ambaye alianza kwa kuyataja majukumu ya baraza la wadhamini la Bakwata kuwa ni kumiliki mali za waislamu wote nchini ambazo zinaamishika na zisizoamishika kama viwanja, nyumba, magari,vifaa na kwamba baraza analoliongoza linapata nguvu za kuongoza kutoka kwenye Baraza la Maulamaa.

Ikome akijibu swali la wakili Kweka lilomtaka aeleze anafahamu nini kuhusu kiwanja hicho cha Chan’gombe Markas, alidai kuwa anachokifahamu ni kwamba akiwa na Mwenyekiti wa Baraza hilo mwaka 2010 aliitisha kikao cha wajumbe wa baraza na wakazungumzia kuhusu hitaji la Bakwata kupata eneo kubwa la kujenga Chuo Kikuu na kwamba wakafikia uamuzi wa kufanya mabadilishano ya kiwanja hicho kilichopo Markas ambacho awali kilikuwa kikimilikiwa na Bakwata ambacho kina ukubwa wa hekari nne na wakabadilishana na Kampuni ya Agritanza Ltd  ambapo kampuni hiyo iliipatia Bakwata  hekari 40 zilizopo Kisarawe na hatimaye Bakwata lile eneo la Markas wakaipatia kihalali kampuni hiyo.

“Na kabla kikao cha baraza langu hakijafikia uamuzi huo, tayari baraza la Maulamaa lilishaketi na kufikia uamuzi huo wa kubadilisha kiwanja hicho na kampuni hiyo kwa hiyo kikao cha baraza langu nacho kiribariki azimio hilo na mkataba ukaandaliwa na hatimaye makabidhiano ya kubadilishana ardhi hiyo yakafanyika ….kwa hiyo leo hii anapoibuka mtu anasema kiwanja cha Chang’ombe Markas ni mali ya Waislamu anakosea sana kisheria kwani ile si mali tena ya waislamu “alidai Ikome.

Akijibu maswali ya mawakili wa utetezi yaliyokuwa yakiulizwa na Nassor Mansoor na wenzake kuwa nyaraka za kuonyesha vikao vya mabaraza hayo ya maulamaa na baraza la wadhamini vilikaa zikowapi na ataje  kama kiwanja cha Kisarawe kilifanyiwa tathimini, kinathamani gani na kwamba ni kwanini kila jambo analoulizwa anadai hakumbuki.

“Sikiliza wewe wakili, misiwezi kukumbuka kila kitu nimeishakwambia kuwa makubaliano ya kubadilishana kiwanja hicho yalifanyika katika vikao halali na nyaraka hizo zipo ofisini na kuhusu eneo la Kisarawe kama lilifanyiwa tathimini ,linathamani gani,waulize wataalamu watakujibu misiwezi kukujibu ….na ninafahamu kuwa unataka neno sijui,sijui litoke mdomoni mwangu…namimi nakwambia hivi hutalipata neno sijui kutoka mdomoni mwangu minakujibu sifahamu kwani hata wewe huwezi kukumbuka kila kitu ila kuhusu maswali ni rahisi sana kama wewe unavyoniuliza”alidai Ikome na kusababisha watu kuangua vicheko.

Kwa upande wake shahidi wa tano ambaye ni miongoni mwa Wakurugenzi wa Kampuni ya Agritanza Ltd, Afidhi Seif  Othman (42),  aliambia mahakama kampuni yake ya Agritanza Ltd ilibadilisha eneo la Chang’ombe na Bakwata na kwamba yeye ndiye alikuwa mmiliki wa eneo la Kisarawe na ndiye aliyeipatia Bakwata eneo hilo na Bakwata ikawapatia eneo la Chang’ombe na kwamba mabadilishano hayo yalifanyika Oktoba 10 mwaka 2010.

 Othman alidai kuwa baada ya kubadilishana Oktoba mwaka jana kampuni yake ilinunua vifaa mbalimbali kwaajili ya kuanza kujenga ukuta wa kutenganisha kiwanja cha Agritanza Ltd na Chang’ombe Markas ambacho ndicho kampuni yake imepewa na Bakwata na kwamba wakati wakianza kuanza ujenzi huo.

Kwamba mlinzi na mjenzi waliokuwa wakijenga hapo Markas  walinipigia simu asubuhi wakaniambi mshtakiwa wa kwanza(Ponda), yupo katika kiwanja hicho ameambatana na mpigapicha wanakipiga picha kiwanja hicho na kwamba yeye akamwambia mlinzi huyo ampatie simu azungumze na Ponda ambapo alimuuliza Ponda kwanini amefika eneo hilo ,  Ponda alimtaka yeye ampigie simu saa mbili usiku wa siku hiyo.

Akadai ilivyofika saa mbili usiku akampigia Ponda, na Ponda akamtaka akutane nae siku ya tatu yake na siku ya tatu yake shahidi huyo alienda kukutana na Ponda katika Msikiti wa Mtambani na ilikuwa ni siku ya Jumanne wakaanza mazungumzo yao ambapo Ponda alimweleza Bakwata wamekosea kubadilisha kiwanja hicho bila ya kuishirikisha taasisi yake na kwamba shahidi huyo akamwambia kama Bakwata wamekosea basi kampuni yake ipo tayari kuipatia taasisi ya Ponda nayo eneo jingine.
Baada ya kumaliza majadiliano hayo alidai kuwa alhamisi yake alipata taarifa za siri kuwa Ponda na wafuasi wake walikuwa wamepanga kesho yake(ijumaa),kuja kuvamia katika eneo la kiwanja hicho cha Chang’ombe Markas na kwamba yeye alichokifanya alienda Kituo Kikuu cha Polisi Kati kutoa taarifa ambapo mapolisi walimtaka aende kituo cha Chang’ombe akatoe taarifa hizo na akaenda Chang’ombe siku hiyo ya Alhamisi ambapo mapolisi wa Chang’ombe walimweleza kuwa asuburi hadi tukio hilo la uvamizi litendeke.

“Kweli ilipofika Ijumaa, Ponda na  kundi la wafuasi wake walivamia katika kiwanja hicho wakiwa na mbao,nondo na wakaanza ujenzi na wakati wanavamia eneo hilo na sisi tulikuwa tumeweka vifaa vyetu vya ujenzi wa ukuta vyenye thamani ya Sh.milioni 59  ambapo nao walianza kujenga  na upande mmoja wa ukuta waliandika neno linalosomeka Masdji Hassan Bin Amir  na walikaa katika eneo hilo kwa zaidi ya siku mbili hadi Oktoba 12 mwaka jana walivyoondoka na wengine kukamatwa na jeshi la Polisi “alidai Othaman.

Kesi hiyo ambayo ilimalizika jana saa tisa Alasiri iliarishwa hadi Januari 31 mwaka huu,na akaamuru Ponda na Mshtakiwa wa tano warudishwe gerezani kwasababu bado Mkurugenzi wa Mashtaka(DDP),Dk.Eliezer Feleshi bado hajaondoa hati yake ya kuwafungia dhamana, na kwamba siku hiyo kesi hiyo  itakuja  kwa ajili ya shahidi wa sita wa upande wa jamhuri kuanza kutoa ushahidi wake.Hata hivyo kadri siku zinavyozidi kwenda idadi ya wafuasi wa Ponda kuja mahakamani kusikiliza kesi hiyo inazidi kupungua kwa kasi ukilinganisha na awali.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Januari 18 mwaka 2013



No comments:

Powered by Blogger.