Header Ads

LULU AREJEA URAIANI,ADAI MUNGU NDIYE ALIYEMPA DHAMANA






Na Happiness Katabazi
HATIMAYE msanii wa  filamu nchini, Elizabeth Michael ‘Lulu’ amepata dhamana baaada ya kutimiza masharti matano aliyopewa na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, juzi wakati mahakama hiyo ilipokuja kusikiliza ombi lake la kuomba apatiwe dhamana katika kesi inayomkabili ya kuua bila kukusudia aliyekuwa msainii mwenzie Steven Kanumba.

Lulu alitimiza masharti hayo jana saa tisa Alasili kwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Francis Kabwe  na baada ya kutimiza masharti hayo ya dhamana aliwaeleza waandishi wa habari huku akitoka machozi kuwa anamshukuru mungu kwani yeye ndiye alifanya akapata dhamana hiyo na hivyo kumfanya atoke gerezani na kurejea kuishi uraiani.

Lulu ambaye alikuwa ameongozana na wakili wake Peter Kibatara  alisema anawashukuru wale  wote waliyokuwa nae bega kwa bega,tangu kesi yake ilipoanza katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam.

“Ninachoweza kusema ni kuwashukuru wale wote walioniangaikia na kuniombe kwa mungu hadi leo nimepata dhamana narudi kuungana na familia yangu …lakini naomba watu hao waendelee kuniombea kwani leo nimepata dhamana tu na ile kesi yangu ya msingi ya kuua bila kukusudia bado haijaanza kusikilizwa na kutolewa uamuzi hivyo naombeni sana waendelee kuniombea na wasinitupe”alisema Lulu.

Msanii huyo amedhaminiwa na Flolian Matungwa,ambaye anatoka Wizara ya Ardhi na Verus Mboneko,ambaye anatoka Wizara ya Afya.

Lulu alifikishwa eneo la Mahakama Kuu saa 7:58 mchana na gari ya Jeshi la Magereza lenye namba za usajili STK 2823.Baada ya kupatiwa dhamana  aliondoka na gari aina ya Land Cruser VX V8,lenye namba za usajili T480 CFX.
Hata hivyo wakili Kibatara, aliwaeleza waandishi wa habari kuwa kwaniaba ya mteja wake anakanusha uvumi  uliokuwa umeenea kuwa Lulu akiachiwa kwa dhamana jana angeenda moja kwa moja kwenye kaburi alilozikwa Kanumba lilopo eneo la Kinondoni na kuongeza kwa kumshukuru Msajili Kabwe kwa kumpatia dhamana mteja wake kwani muda wa kazi ulikuwa umepita.
Juzi  Jaji Zainabu Mruke muda mfupi baada ya mawakili wa Lulu, Peter Kibatara, Kennedy Fungamtama na Fulgence Massawe kuiomba mahakama hiyo impatie dhamana mshtakiwa huyo ambaye amesota rumande katika gereza la Segerea tangu Aprili mwaka jana  ambapo walieleza kuwa ombi la dhamana wameliwasilisha chini ya kifungu cha
148(1) ,(2) Cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 .

Jaji Mruke alisema ili mahakama impatie dhamana ni lazima asalimishe  kwa Msajili wa mahakama hiyo hati ya kusafiria,  kutotoka nje ya Dar es Salaam  bila ruhusa ya mahakama, kuripoti kwa msajili kila mwezi ,kuwa na wadhamini wawili ambao ni watumishi wa serikali  ambao watasaini bondi ya Sh.milioni 20 kila mmoja.

Baada ya jaji huyo kutangaza masharti hayo Lulu na wakili wake walitoka nje ya ukumbi uliokuwa ukiendeshwa kwa shauri hilo kwa ajili ya kwenda kwa msajili kutimiza masharti hayo lakini kwa bahati mbaya Msajili hakuwepo ofisini na hivyo kufanya Lulu kurudishwa rumande na akarejeshwa jana mchana mahakamani hapo kwaajili ya kuja kutimiza masharti ya dhamana mbele ya msajili huyo Kabwe ambapo aliyatimiza jana na kupatiwa dhamana.

Kufuatia mahakama hiyo juzi  kumpatia masharti ya dhamana Lulu kutoka na ombi lake Na.125/2012 la kuomba mahakama hiyo impatie dhamana, lakini bado kesi ya msingi inayomkabili Lulu ambayo ni ya kuua bila kukusudia bado haijapangiwa jaji wala tarehe ya kuanza kusikilizwa.

Wasanii waliyokuwepo kumuunga mkono Lulu mbali na mama yake mzazi mahakamani hapo alikuwepo Mahsein Awadh maarufu Dk.Cheni, Muna na msanii mwingine mmoja.

Desemba 21 mwaka jana , Hakimu Mkazi Christine Mbando wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu aliifunga kesi ya kuua bila kukusudia Lulu na kuiamishia rasmi kesi hiyo katika Mahakama Kuu, na uamuzi huo wa mahakama ulitokana na upande wa Jamhuri kumsomea maelezo ya kesi yake kwa kina mshtakiwa huyo na kuieleza mahakama kuwa wanakusudia kuleta jumla ya mashahidi tisa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Januari 30 mwaka 2013.







No comments:

Powered by Blogger.