Header Ads

MCHUNGAJI, MLINZI KANISA LA KKKT MBAGALA WASIMULIA VURUGU ZA KUCHOMA KANISA HILO


Na Happiness Katabazi
MCHUNGAJI Kanisa la Kilutheri la Kiinjili (KKKT), Usharika wa Mbagala jijini Dar es Salaam,  Frank John (32) jana ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jinsi alivyoruka ukuta wa  Kanisa  na kujificha katika Benki ya  CRDB tawi la Mbagala ili kunusuru maisha yake kwa kukwekwa kundi la watu wasiyofahamika kuvamia eneo la kanisa hilo na kufanya uharibifu.

Washtakiwa wanaokabiliwa na kesi hii ni Hamid Senkondo, Shego Shego, Mashaka Iman, Hamza Mohamed, Juma Mbegu, Issa Abdallah, Hamis Kimwaga, Ramadhan Mburu na Mohamed Yusuph, wanakabiliwa na makosa ya kula njama, unyang’anyi wa kutumia silaha,wizi wa vifaa mbalimbali   mnamo Oktoba 10, 2012, ndani ya kanisa hilo.

John alitoa maelezo hayo jana mbele ya Hakimu Mkazi  Waliarwande Lema,wakati alipokuwa akiongozwa na wakili Mwandamizi wa Serikali Tumaini Kweka kutoa ushahidi wake katika kesi  ya kula njama , kuvunja jengo hilo kwa nia ya kutenda kosa, kuharibu mali kwa makusudi, unyang’anyi wa kutumia silaha na kuchoma mali za kanisa hilo kwa makusudi inayowakabili washtakiwa kumi mahakamani hapo.
 
Mchungaji  John alidai kuwa Oktoba 12, mwaka jana  akiwa  ndani ya ofisi za kanisa hilo kwa ajili ya kazi zake za kawaida  alipigiwa  simu na kujulishwa kuwa  kuna vurugu na kwamba wawe makini.
“Baada ya kupata taarifa hiyo nilifikia uamuzi wa kufunga ofisi  na  kumfuata  mlinzi awe tayari  na nipange ulinzi ,lakini ghafla  nilishtukiwa tumeishavamiwa  na kundi kubwa  la watu waliokuwa  wakirusha mawe na  matofali.  Kutokana na uvamizi huo na taarifa nilizozipata moja kwa moja nilijua nipo hatarini.”alidai Mchungaji John. 

Alieleza kuwa kutokana na uvamizi   askari aliyekuwa akilinda  lindo la kanisa hilo siku hiyo , Michael Samuel (30) alipiga risasi moja hewani, na kundi hilo la watu  lilitawanyika ,na mlinzi yule   alipiga risasi ya pili  lakini haikusaidia kwasababu  ganda la risasi ya kwanza lilikwama ndani ya bunduki.

“Wakati mlinzi yule akiangaika kuirekebisha bunduki yake iliyokuwa imekorofisha  , kundi lile la watu ambao hawakuweza kuwatambua lilirudi tena na kuanza  kurusha  vipande vya matofali na mawe , Hivyo ‘nikazunguka nyuma ya kanisa, nikaruka ukuta ili kuokoa maisha yangu  na kukimbilia  katika benki ya CRDB tawi la Mbagala kujificha.” Alidai shahidi huyo.

Mchungaji huyo alidai kuwa yote hayo yalifanyika majira ya mchana lakini hakumbuki ilikuwa ni saa ngapi na kwamba baada ya tukio hilo alimpigia simu Mwinjilisti wa kanisa hilo  ili kuweza kujua kama hali imetulia na baada ya Mwinjilisti kumjulisha   kuwa hali imetulia alikwenda kanisani hapo ambapo aliwakuta askari wa jeshi la polisi  ambao nao walimuweka chini ya ulinzi hadi alipowaonyesha kitambulisho chake kuwa yeye  ni  Mchungaji.

“Nilipoonyesha kitambulisho niliachiwa nikaona milango, uzio wa Kanisa, ofisi ya mchungaji, zimeharibiwa na thamani mbalimbali zimeibiwa huku Membari ikiwa imechomwa moto  na maboksi  sita ya kuwekewa sadaka na mengine niliyaona katika ofisi ya mchungaji yakionekana kuwa yalitumika kukokewa moto  kwenye ofisi ya mchungaji.” Alieleza.

Kwa upande wake  shahidi wa kwanza ,  Michael Samuel ambaye ni mlinzi wa kanisa hilo alieleza mahakama hiyo jana kuwa   Oktoba 11, mwaka jana   aliingia kazini na ilipofika saa 12 jioni hali ilikuwa shwari  na ilipofika   Oktoba 12, mwaka jana,saa 5 asubuhi  watu waliokuwa na vipande vya matofari na mawe walipowavamia na kuyarusha kuelekea ndani ya kanisa hilo na baada ya hali hiyo ya hatari kutokea aliamua kupiga risasi moja kuelekea juu, kundi hilo la watu lilitawanyika  na kukawa na amani.

Samwel alidai  baada ya kundi lile la watu kutawanyika, yeye alianza kufungua bunduki na kuona ganda la risasi likiwe limeganda  hivyo kufanya risasi ya pili kushindwa kutoka na kwamba baada ya saa moja kupita kundi lile la watu lilirudi tena kwa  mara ya   pili na kuanza kufanya mashambulizi makalikwa mashambulizi makali.

“Baada ya kuona hivyo na bunduki imekorofisha nikaamua kujificha  kwenye upenyo na hatimaye nikaruka ukuta na kukimbia ili kuokoa maisha yangu. Hivyo mengine yaliyokuwa yakitokea sikuyajua wala idadi ya watu hao sikuweza kuifahamu  kwa sababu ilikuwa  kama vita, mimi nilichoangalia ni kusalimisha roho yangu.” Alidai.  

Alidai kuwa alipofanikiwa kukimbia kutoka katika eneo hilo, hakurejea tena katika eneo hilo nyakati za  jioni  alipokwenda kufuata nguo zake  ambazo nazo hakuziona  na kuona mazingira  na vitu mbalimbali mali ya kanisa vikiwa  vimeharibiwa ikiwemo uzio wa kanisa ulikuwa umebomolewa, membari imeunguzwa moto, mageti ya milangoni na madirishani yamebomolewa, feni zimevunjwa na  ofisi ya mchungaji imechomwa moto. Hakimu Lema aliiahirisha kesi hiyo hadi Februari 4, mwaka huu itakapoendelea kwa ushahidi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Januari 22 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.