Header Ads

WANA MTWARA NI KWELI BOMBA LA GESI KUJA DAR?





Na Happiness Katabazi
MWISHONI mwaka jana  baadhi ya wakazi wa Mkoa wa Mtwara walifanya maandamano ya amani wakishinikiza kuwa  gesi iliyogundulika Mtwara iwanufaishe watu wa mkoa huo.

Wananchi hao miongoni mwao walibeba mabango mbali  kwa  lengo la kufikisha ujumbe wao huo ambapo pamoja na madai mengine wanataka bomba la gesi lisijengwe kutoka Mtwara kuja Dar es Salaam.

Kimsingi wananchi wale ambo wengine walikuwa wamebeba bendera za vyama vya siasa  walikuwa wakiitumia haki yao ya Kikatiba iliyoainishwa wazi  kwenye Ibara ya 18(a) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 , inayosomeka hivi ; ‘kila mtu anao uhuru wa kuwa na maoni na kueleza fikra zake’.

Lakini wakati wakazi wa Mtwara mkiifurahia haki  hiyo ya Kikatiba nataka mtambue kuwa Rais wa nchi ndiyo   msimamizi wa ardhi yote hapa nchini kwa niaba ya wananchi wote.Natunapozungumzia ardhi maana yake ni kila kitu kilichopo juu na ndani ya ardhi.Na kifungu cha 45 cha Sheria ya Ardhi ,kinampa mamlaka rais kubadili matumizi ya ardhi fulani kwaajili ya maslahi ya umma.

Nasema kama kweli wananchi wale waliandamana kwa madai hayo,kwa maoni yangu nasema siungi mkono dai lao hilo linalotaka bomba la gesi lisiunganishwe kuja Dar es Salaam  kwani ni wazi kabisa madai hayo yameanza kujenga ubinafsi na ubaguzi baina ya wananchi wa mikoa na mikoa.

Hivi kweli kama leo hii hao baadhi ya wananchi wa Mtwara wanaodai Gesi isije Dar es Salaam,si kesho wakazi wa Ruvu Mkoa wa Pwani nao wataibuka na kuandaa maandamano ya kutaka yale maji ya kunywa tunayokunywa wa kazi wa Dar es Salaam yasiruhusiwe tena kupelekwa Dar es Salaam, kwani maji hayo ni mali ya wakazi mkoa wa Pwani?

Kama ajenda hiyo ya kina ‘Chinga’ itakubaliwa si kesho hapa nao watu wakabira la Wakwere wataibuka na kudai kuwa Rais Jakaya Kikwete ni rais wao na si rais wa makabila mengine yaliyomo ndani   ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania?

Kama ajenda hiyo ya kina ‘Chinga’ ikikubalika basi na sisi  Wayambo, wahaya na Wachaga nao waanzishe maandamano ya kutaka ndizi tunazolima katika mikoa yetu ya Kagera na Kilimanjaro zisije kuuzwa Dar es Salaam?

Na kama ajenda ya kina Chinga’  itakubaliwa basi na sisi wakazi wa Dar es Salaam, tuandae maandamano ya kutaka ‘Chinga’wasiruhusiwe kuja Dar es Salaam, kufanyabiashara ndogondogo?

Nyie wa kina chinga mbona mwaka 2000-2010 mtoto wenu Rais Mstaafu Benjamin Mkapa alivyokuwa rais wa Jamhuri, mbona hamkujitokeza hadharani kusema huyo ni rais wa kina Chinga kwasababu ni mzaliwa wa Mtwara? 

Kwanza tuwaulize hao waandamanaji kama wanaushahidi wowote unaonyesha kuwa  serikali ilishawahi  kutoa azimio ya kuwakataza wawekezaji wasijekuwekeza huko Mtwara? Na je hiyo gesi ikifungwa bomba ikapelekwa Dar es Salaam, ndiyo wakazi wa Mtwara mtakuwa hampati nishati hiyo?

Au wakazi hao wanaweza kutoa ushahidi wowote unaonyesha endapo bomba hilo la gesi likifungwa kutoka Mtwara kuja Dar es Salaam, basi mkoa huo wa Mtwara utarudi nyuma kimaendeleo na gesi wanayoitumia hivi sasa wakazi wa Mtwara itapungua kwa kiasi kikubwa?

Leo baadhi ya wakazi wa Mtwara mmeandamana kutaka gesi isipelekwe Dar es Salaam, kesho basi nao wakazi wa mkoa wa Lindi nao waandamane wakatae gesi iliyopo Kisiwa cha Songongoso  wilaya ya Kilwa isiendelee kuletwa Dar es Salaam?Huu ni ubinafsi na ni tishio la usalama kwa taifa hili siku za usoni.

Kwani huwezi kuwa na wananchi ambao wanatumia gesi hiyo iliyopo kwenye ardhi wanayoishi lakini hawataki gesi hiyo itumiwe na wananchi wenzao wanaishi katika mikoa mingine katika nchi moja.Tusikubali.
Mbona nyie baadhi ya wakazi wa Mtwara hamna shukurani? Hivi Mtwara ya leo ni sawa na Mtwara ya miaka 30 iliyopita?

Nimezunguka Mtwara katika wilaya zake zote kwa zaidi ya mara nne.Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 2004, 2005 mbapo nilizunguka mara mbili na aliyekuwa mgombea urais wa Chama cha NCCR-Mageuzi, Dk.Sengondo Mvungi  na aliyekuwa mgombea urais wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Agustine Mrema na mwaka 2010 nilizunguka tena nchi nzima yaani Tanzania Bara na Zanzibar na aliyekuwa mgomea mwenza wa CCM, Dk.Mohamed Gharib Bilal, hakuna ubishi kuna mabadiliko makubwa sana ya kimaendeleo ukilinganisha na Mtwara ile niliyokuwa nikisiikia na kuona mwaka 2004 yamefikiwa licha bado jitihada zaidi zinatakiwa ziongezwe.
Barabara zinapitika licha nyingine hazijawekwa lami,nyumba za kulala wageni pale Mtwara mjini zimeongezeka, maofisi ya  sekta binfasi na serikali yameongezeka ukilinganisha na zamani na ndiyo maana leo hii ndugu zetu waliohamishiwa Mtwara kikazi wamekuwa wakitutambia kuwa barabara ya kutoka Dar es Salaam, kwenda Mtwara inawapa jeuri kwani imesaidia sana uhakika wa usafiri kwani hivi sasa unatoka Dar es Salaam asubuhi Mtwara unafika saa tisa alasairi.Mbona hatua hii ya maendeleo iliyopigwa hamuisemi?

Tayari kuna habari ambazo zijazithibitisha kuwa maandamano yale yana nguvu nyuma ya wanasiasa  uchwara na wenye hulka za kinyanga’u ambao ndiyo hasa wanawachochea  baadhi ya wananchi ambao hata ukiwauliza wanafahamu hata majina ya wataalamu waliyogundua gesi hiyo ardhini ni nani hawamjui, waandamane.

Watu wa nchi hii siku zote hawanaga siri ,ipo siku itakuja kubainika hadharani kuwa ni manyang’au gani ya kisiasa yanaamasisha chuki hiyo na kuchochoea  maandamano hayo na ubinfasi huo wa kusema bomba la gesi lisiunganishwe kutika Mtwara kuja Dar es Salaam.

Nihitimishe kwa kutofautiana na wale baadhi ya wakazi wa Mtwara wanaokataa bomba la gesi lisijengwe kuja Dar kwani ni ubinafsi wa hali ya juu na ubaguzi na pia naiomba serikali nayo iweke wazi kwa wananchi wa Mtwara faida kama za afya, elimu, mazingira na kiuchumi baada ya bomba hilo kuunganishwa kuja Dar es Salaam.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika
0716 774494
Chanzo: www.katabazihappy.blogspot.com , Januari 3 mwaka 2013
Facebook; happy katabazi

No comments:

Powered by Blogger.