Header Ads

KESI YA MARANDA NA EPA YASHIKA KASI

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa Jamhuri katika kesi ya wizi ya sh bilioni 2.2 katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) Benki Kuu ya Tanzania, (BoT), inayomkabili Mweka Hazina wa CCM, Mkoa wa Kigoma, Rajabu Maranda, na ndugu yake, Farijala Hussein, umefunga kesi yake rasmi.


Mbele ya Jaji, Fatma Masengi, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Wakili Kiongozi wa Serikali, Fredrick Manyanda, aliiambia mahakama hiyo kuwa upande wa Jamhuri umefunga rasmi kesi hiyo baada ya mashahidi wake sita kumaliza kutoa ushahidi wake jana.

“Sisi upande wa Jamhuri leo tunatangaza rasmi kuifunga kesi yetu baada ya kuleta idadi hiyo ya mashahidi,” alidai Wakili Kiongozi Manyanda.

Kwa upande wake wakili wa utetezi, Majura Magafu aliomba mahakama iuamuru upande wa Jamhuri umpatie mwenendo mzima wa kesi hiyo ili aweze kwenda kuupitia na kuweza kumsaidia kujenga hoja itakayoweza kuishawishi mahakama iwaone wateja wake hawana kesi ya kujibu na Jaji Masengi alikubaliana na ombi hilo.
Jaji huyo aliiahirisha kesi hiyo hadi Desemba 13 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya kutajwa na kuona kama tayari upande wa Jamhuri umeishawapatia mwenendo huo upande wa utetezi.

Awali shahidi wa sita wa upande wa Jamhuri, ambaye ni Msajili Msaidizi (BRELA), Noel Shani, akiongozwa kutoa ushahidi wake na Manyanda aliambia mahakama kuwa yeye ndiye aliyelisajili jina la Kampuni ya Money Planner ambayo ilitumiwa na washitakiwa kuchota fedha za EPA.

Alisema anachokifahamu yeye ni kwamba alisajili jina hilo la kampuni ambayo wamiliki wake ni Paul Nyingo na Fundi Ayeshi Kitunga na si Maranda na Farijala kama washitakiwa wanavyodai kuwa kampuni hiyo ni yao.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Novemba 17 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.