Header Ads

MAHALU AIBWAGA SERIKALI KORTINI

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, imetamka kuwa kifungu cha 36(4)(e) sura ya 200 cha Sheria ya Uhujumu Uchumi kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002, ni kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.


Sambamba na hiyo, mahakama hiyo, imetoa maelekezo kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ndani ya mwaka mmoja kuanzia jana, awe amefanyia marekebisho kifungu hicho.

Hukumu hiyo ya Kesi ya Kikatiba ya mwaka 2008, iliyofunguliwa mahakamani hapo na aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ilitolewa jana na jopo la majaji watatu lililokuwa likiongozwa na Jaji Kiongozi, Fakhi Jundu, aliyekuwa akisaidiwa na Jaji Agustine Mwarija na Projest Rugazia ambaye hakuwepo mahakamani hapo wakati hukumu hiyo ikisomwa.

Akisoma hukumu hiyo, Jaji Jundu alisema kimsingi Mahakama Kuu inakubalina na hoja za mawakili wa mlalamikaji (Mahalu), aliyekuwa akitetewa na mawakili wa kujitegema, Alex Mgongolwa na Cuthbert Tenga kwamba kifungu hicho cha 36 (4)(e) sura ya 200 cha Sheria ya Uhujumu Uchumi, kinakwenda kinyume na Katiba ya nchi na kinaleta ubaguzi.

Alisema wanakubaliana na hoja za mawakili wa Mahalu, kwamba uwepo wa kifungu hicho unafanya mshtakiwa mwenye fedha ndiye apate dhamana na mshtakiwa ambaye hana fedha hawezi kutimiza masharti hayo ya dhamana hivyo kuishia kusota gerezani.

Hata hivyo, Jaji Jundu alisema kwa mujibu wa Ibara ya 30 (5) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mahakama Kuu inapoona kifungu chochote cha sheria kinakiuka ibara za Katiba , ina mamlaka ya kutoa maelekezo kwa Mwanasheria Mkuu kukifanyia marekebisho kifungu hicho.

Hii ni kesi ya pili ya Kikatiba kufunguliwa na wananchi katika mahakama hiyo dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na mwisho wa siku, wanashinda tangu serikali ya awamu ya nne iingie madarakani.

Mahalu alilazimika kufungua kesi ya Kikatiba Mahakama Kuu, ikiwa ni muda mfupi baada ya mwaka 2006, kufikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi ya sh bil. 3.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Oktoba 5 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.