Header Ads

KORTI KWA KUSHAWISHI NA KUKOJOLEA Q'URAN


Na Happiness Katabazi

WAKAZI watatu wa eneo la Gongolamboto jijini Dar es Salaam,jana walijikuta wakifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu chini ya ulinizi mkali kwa makosa ya kudhalilisha kitabu cha dini ya Kiislamu na kushawishi kutendeka kwa kosa hilo.

Wakili Mwandamizi wa Serikali Tumaini Kweka mbele ya Hakimu Mkazi Bingi Mashabara aliwataja washitakiwa hao kuwa ni David Kapaya(20) ambaye ni muumini wa dini ya Kikristo, Mussa Sule(26) mbaye ni muuzaji wa Vocha za Kampuni ya Tigo na Haruna Mateno(17)  ambao walikuwa hawana wakili wa kuwatetea.

Wakili Kweka alilitaja shitaka la kwanza linamkabili mshitakiwa wa kwanza peke yake (David), ambalo ni la kudhalilisha dini ya Kiislamu ambalo ni kinyume na kifungu cha 125 ambacho kinasomwa pamoja na kifungu cha 35 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 ,kuwa  Oktoba 20 mwaka huu, huko eneo la Mogo, Mikongoro alidhalilisha dini ya Kiislamu  kwa kukikojolea kitabu cha  dini ya Kiislamu(Korani).

Alidai shitaka la pili kwaajili ya mshitakiwa wa pili na watatu (Sule na Haruna) peke yao kuwa wanakabiliwa na kosa la kumshawishi kutendeka kwa kosa la kudhalilisha dini ya kiislamu.Kuwa mnamo Oktoba 20 mwaka huu, huko eneo la Mogo, Mikogore  wakiwa na ufahamu washitakiwa hao walimshawishi mshitakiwa wa kwanza(David) akojolee  kitabu hicho cha dini ya Kiislamu huku wakijua kufanya hivyo ni kosa na kwamba upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.

Hata hivyo washitakiwa walikana mashitaka hayo.Na Hakimu Mashabara bila ya kutaja masharti ya dhamana aliamuru washitakiwa wapelekwe mahabusu hadi Novemba 15 mwaka huu, kesi hiyo itakapokuja kwaajili ya kutajwa.

Hii ni mara ya pili kwa waumini wa dini ya Kikristo kufikishwa katika mahakama hiyo na kushitakiwa kwa kosa la kudhalilisha kitabu cha dini ya Kiislamu.Mara ya kwanza ilikuwa ni Oktoba 18 mwaka huu, ambapo mtoto mmoja mwenye umri wa chini ya miaka 18 alifikishwa katika Mahakama ya Watoto akikabiliwa na kosa la kudhalilisha dini ya Kiislamu kwasababu alikikojolea katika Maeneo ya Mbagala mwezi uliopita.

Itakumbukwa ghasia kubwa na mapambano baina ya baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu na jeshi la polisi yalizuka jijini Dar es Salaam Oktoba 12 mwaka huu, na kusababisha makanisa manne kuchomwa moto,uvunjifu wa amani kutoweka na mwishowe washitakiwa zaidi 70 wamefunguliwa kesi za unyang’anyi wa kutumia silaha, wizi katika mahakama hiyo ya Kisutu  na kesi hizo zinaendelea mahakamani hapo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Novemba 3 mwaka 2012.

No comments:

Powered by Blogger.