Header Ads

WANAJESHI WALIOHUKUMIWA ADHABU YA KIFO KUKATA RUFAA


Na Happiness Katabazi

IKIWA ni siku moja tu tangu Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, iwahukumu adhabu ya kifo askari wa wiwili wa jeshi la Kujenga Taifa na mmoja wa Jeshi la Wananchi(JWTZ) baada ya kuwatia hatiani kwa kosa la kumuua kwa kukusudia Swetu Fundikira, wafungwa hao jana wamewasilisha katika mahakama hiyo hati ya kusudio la kutaka rufaa kupinga hukumu hiyo.

Wafungwa hao ni MT 1900 Sajenti Roda Robert (42), MT 85067 Koplo Mohamed Rashid  wa JKT Mbweni na MT 75854 Koplo Ally Ngumbe (37) wa kikosi cha JWTZ Kunduchi.  
 
Wakili wa askari wa wafungwa hao Mluge Karoli alisema ameishawasilisha mahakamani hapo jana kwa madai kuwa wateja wake hawakubaliani na hukumu hiyo iliyotolewa juzi na Jaji Zainabu Mruke ambaye aliwatia hatiani kwa kosa kuua kwa kukusudia kinyume na kifungu cha 196 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002.

Karoli alieleza kuwa sababu zilizomsukuma yeye na wateja wake kuwasilisha hati hiyo ya kusudio jana ni kwamba  kesi yoyote ya ugomvi  haiwezi  kuwa na kusudio la kutaka kuua na kwamba hakuna shahidi wa upande wa jamhuri aliyefika mahakamani hapo na kueleza kuwa wateja wake ndiyo wamemuua Swetu Fundikira na kuongeza kuwa washitakiwa hawakuwa na jukumu la kuthibitisha kesi hiyo na kusisitiza kuwa waliomua Swetu siyo wateja wake.
 
Aidha wakili huyo alieleza kuwa aliyepambana na wateja wake ni Swetu Fundikira na uchunguzi wa daktari unaonyesha jina la Swetu Ramadhani Fundikira hivyo ni watu wawili tofauti na kwamba hakuna hata shahidi mmoja  alifika mahakamani na kueleza aliwai kuuona mwili wa marehemu au kuudhulia kwenye msiba.
 
Askari hao kwa pamoja walidaiwa  kuwa walimpiga Fundikira, Januari 23 mwaka huu  saa 7:30 usiku wilayani Kinondoni jijini Dar es Salaam na baadaye kufariki dunia usiku huo huo wa kuamkia Januari 24, mwaka 2010, katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
 
Akisoma hukumu hiyo juzi , Jaji Muruke alisema ingawa hakuna ushahidi wa moja kwa moja kuwa washtakiwa hao ndio waliomuua Fundikira, ushahidi uliotolewa na  upande wa Mashtaka (Jamhuri) ulikuwa ni ushahidi wa mazingira, kwamba Jamhuri imeweza kuthibitisha mashtaka hayo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Novemba 22 mwaka 2012.

No comments:

Powered by Blogger.