Header Ads

KESI YA PONDA YAIVA


*Masharti ya dhamana yatajwa
*Ulinzi mkali  watanda Kisutu
*Hukumu ya Maranda yayeyuka tena

Na Happiness Katabazi
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, ndani na nje ya mahakama hiyo jana ilitawaliwa na ulinzi mkali toka vyombo  vya ulinzi na usalama kwa ajili ya kuakikisha usalama unakuwepo katika eneo hilo wakati kesi ya uchochezi na wizi wa mali za sh milioni 59 inayomkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Sheikh Issa Ponda Issa na wenzake 49 ilipokuja kwaajili ya kutajwa.

Washitakiwa hao walifikishwa jana saa moja asubuhi mahakamani hapo chini ya ulinzi mkali wa Askari wa Jeshi la Magereza waliokuwa wamebeba silaha nzito na kiunoni wakiwa wamebeba mabomu ya machozi na wengine wakiwa wamevalia vifaa maalumu mwilini kwaajili ya kujikinga na silaha (Riot Wear) wakati askari wa jeshi la Polisi wakiwa nao wamebeba silaha nzito na wengine wakiwa na Mbwa zaidi ya saba ambao walikuwa kwaajili ya kunusa mabomu na polisi wengine walikuwa wamepanda farasi  wawili wakizungunga ndani na nje mahakama hiyo huku askari wanaodhaniwa kuwa ni wa Idara ya Usalama wa Taifa(TISS), wao wakiwa wameweka hema katika mlango wa kuingilia geti la mahakama hiyo pamoja na kufunga vifaa maalum kwaajili ya kuwakagua watu waliokuwa wakitaka kuingia ndani ya mahakama hiyo pamoja na ukuta wa mbele ya mahakama hiyo ulikuwa umefungwa  kamera ya CCTV.

Tanzania Daima  liliwashuhudua washitakiwa  wakiingizwa ndani ya viwanja vya mahakama hiyo saa moja asubuhi huku wakiwa wamebebwa kwenye magari ya jeshi la Magereza matatu yakiwa namba za usajili STK 4480, STK 916 na STK 9160 aina ya Ashoko Layland ambayo yalitanguliwa na Defenda mbili za Polisi zenye namba za usajili  PT 2066,STK 4480 ,PT 1523,PT 2093 na gari lilobeba maji ya kuwasha ‘Kikojozi’ na magari mengine mengi ya wanausalama ambao walikuwa wakiongozwa na Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Kipolisi Ilala, Duani Nyanda na maofisa maofisa wengine toka Jeshi la Magereza  na Usalama wa Taifa.

 Washitakiwa hao saa  waliingizwa moja kwa moja nyumba ya mahakama hiyo na kisha kupandishwa  katika mahakama ya wazi mbele ya Hakimu Mkazi  Victoria Nongwa saa 2:05 asubuhi ambapo wakili Mwandamizi wa Serikali Tumaini Kweka alianza kwa kuimbukusha mahakama kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya kutajwa na akadai kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika.

Hakimu Nongwa  alisema  kwa mujibu wa mashitaka yote yanayomkabili Sheikh Ponda na wenzake 49 yana dhamana kwa mujibu wa sheria isipokuwa mahakama hiyo bado inaendelea kufungwa mkono na hati ya kuzuia dhamana ya Ponda peke yake iliyowasilishwa mahakamani hapo Oktoba 18 mwaka huu, na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Dk.Eliezer Feleshi chini ya kifungu cha 148(4) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, ambacho kina mpa madaraka DPP kuwawasilisha hati hiyo ya kufunga dhamana ya mshitakiwa yoyote wa makosa ya jinai  hata kama mashtaka dhidi ya mshitakiwa huyo yana dhamana na DPP anapoiwasilisha  hati hiyo mahakama inakuwa imefungwa mkono hadi pale DPP atakapojisikia kuiondoa hati hiyo.

“Kwa sababu hadi leo hii(jana) DPP bado hajaiondoa hati hiyo mahakamani hapa, mahakama hii haitaweza kutoa masharti ya dhamana kwa Sheikh Ponda  na hivyo basi leo haitazungumzia dhamana ya Ponda na badala yake inatoa masharti ya dhamana kwa kuanzia kwa mshitakiwa wa pili hadi 50 kama ifuatavyo”alisema Hakimu Nongwa.

Hakimu Nongwa alisema kila  mshitakiwa atatakiwa awe na wadhamini  wawili wa kuaminika  na atasaini bondi ya shilingi Milioni moja na wadhamini hao wawe na vitambulisho toka ofisi zinazotambulika na kwa anaiarisha kesi hiyo hadi Novemba 15 mwaka huu, itakapokuja kwa ajili ya upande wa Jamhuri kuwasomea maelezo ya awali washitakiwa hao.

Baada ya hakimu huyo kuairisha kesi hiyo saa 2:01 asubuhi maofisa usalama waliwaondoa ndani ya ukumbi wa mahakama washitakiwa hao na kisha kuwapeleka nyuma ya mahakama hiyo na kisha kuwaongoza kupanda mabasi ya jeshi la Magereza matatu huku washitakiwa hao wakionekana kuwa na nyuso za upole tofauti na mara ya kwanza washitakiwa hao  walivyofikishwa mahakamani hapo na kuondoshwa kupelekwa gerezani Oktoba 18  mwaka huu, walikuwa wakiimba na kupaza sauti ndani ya magari hayo kuwa ‘Taqbir alhuqabal’.

Wakati muda huo ikiendelea mahakamani na kuarishwa wanausalama zaidi ya 50 walikuwa wametanda ndani ya viunga na nje ya jengo la mahakama hiyo huku wakiwa wamebeba bastora viunoni,wengine mabomu ya machozi wameyafunga kiunoni,na wengine wamevalia vifaa vya kujikinga na silaha (Riot Wear) na wengine wakiwa wameshikilia mbwa wa kunusa mabomu na farasi wakiwa wakilinda usalama na kisha ilipofisa saa 2:46 asubuhi msafara wa uliokuwa umewabeba wa washitakiwa hao uliondoka mahakamani hapo chini ya ulinzi mkali kwaajili ya kuwarudisha  katika gereza la Segerea ,Ponda na wenzake wote ambao wadhamini wao hawakuwa wamewahi kuja kuwadhamini.

Aidha msafara huo ulipoondoka ndipo ndugu na jamaa wa washitakiwa na wananchi wengine waliokuwa wanataka kuja mahakamani hapo kwaajili kusikiliza kesi zao na kuwadhamini washitakiwa walianza kuwasili lakini hata hivyo walikuwa wakitakiwa na wana usalama geti kueleza wanataka kwenda mahakama hapo kufanya nini na magari yalizuiwa kwa muda kuingia ndani ya mahakama hiyo hadi pale washitakiwa hao walipoondoshwa mahakamani.

Hata hivyo Tanzania Daima liliwashuhudia ndugu na jamaa wa shitakiwa hao kuanzia saa tatu asubuhi wakiwasili na wakakutana na wanausalama geti waliowataka wawaonyeshe hizo barua za dhamana wanazotaka kuwazamani washitakiwa na wengine walikuwa hawana barua hizo  hivyo wana usalama waliwazuia wale wote waliodai kuwa wamekuja kuwadhamini wakati hawana barua wasiingie ndani ya geti hilo na walitii amri hiyo bila shuruti.

Lakini hata hivyo wanausalama hao ambao walianza kutanda ndani na nje ya mahakama hiyo tangu saa 12 asubuhi walizuia watu wasipite wala kukaribia eneo la uzuio wa mahakama hiyo kwasababu za kiusalama hali iliyosababisha baadaye kuibuka kwa kikundi cha watu waliojitambulisha kuwa wao ni waumini wa dini ya Kiislamu karibu na uzio wa mahakama na kuanza kupaza sauti kuwa “Serikali inaonea waislamu, waislamu wanagandamizwa, mahakama ni ya wakristo, hakuna haki’.

Hata hivyo askari wa kikosi cha FFU na wale waliokuwa wamepanda Farasi walienda kukitanya kikundi hicho kilichokuwa kikipaza sauti nje ya uzio wa mahakama karibu na Jengo la Maktaba Kuu ya Taifa  ambao walitawanyishwa kwa Farasi wawili na kukimbia hadi Chuo cha Biashara(CBE). Pamoja na hali hiyo shughuli za kimahakama ziliendelea kama kawaida kwani hazikuathirika na kesi na hali hiyo ya usalama.

Baadhi ya watu waandishi wa habari,wanasheria na wananchi wa kawaida waliipongeza serikali kwa hatua yake ya kuimarisha ulinzi wa hali ya juu katika mahakamani hapo wakati kesi hiyo ya Ponda na wenzake ilipokuja kwaajili ya kutajwa na kupendekeza ulinzi huo uwe ni endelevu katika kesi hiyo na kwamba wanaviomba vyombo vya dola vikabiliane na wale wote watakaoandamana leo.

Awali Oktoba 18 mwaka huu, Wakili Mwandamizi wa Serikali Kweka alidai washitakiwa 49 wanakabiliwa na makosa manne na Ponda ana kabiliwa na makosa matano. Makosa hayo ni kula njama kutenda kosa ,kuingia kwa nguvu   kwa nia ya kutenda kosa kuwa Oktoba 12 mwaka huu huko Chang’ombe Markasi, wasipokuwa na sababu za msingi waliingia kwa jinai kwenye kiwanja kinachomilikiwa na kampuni ya  Agritanza, kujimilikisha  kiwanja hicho kwa njia ya iloyopelekea uvunjifu wa amani,wizi  ambapo  baada ya kufamia waliiba vifaa na malighafi  ikiwemo nondo, kokoto zenye jumla ya thamani ya Sh. 59,650,000 mali ya kampuni ya  Agritanza  na kosa la tano ni la  uchochezi ambalo linamkabili Sheikh Ponda peke yake  ambapo anadaiwa kutenda kosa hilo  Oktoba 12 mwaka huu ,katika eneo hilo ambapo aliwaamasisha washitakiwa hao watende kosa hilo.

Wakati huo huo ,Mahakama hiyo imeairisha kutoa hukumu ya kesi ya wizi wa Shilingi milioni 207 katika Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki Kuu ya Tanzania, inayomkabili Kada wa Chama cha Mapinduzi, Rajab Maranda,Faijala Hussein, Ajay Somayi na maofisa wa BoT, Iman Mwakosya,Ester Komu,Sophia Lalika kwasababu idadi ya jopo mahakimu wanaosikiliza kesi hiyo halijakamilika.

Jaji Beatrice Mutungi alisema kama inavyoeleweka kesi hiyo imekuwa ikisikilizwa kwa mtindo wa jopo la mahakimu wa tatu yaani yeye Jaji Mutungi, Jaji Samuel Karua na Hakimu Mfawidhi wa mahakama hiyo Ilvin Mugeta lakini Jaji Karua ambaye kituo chake cha kazi kipo mkoani Mbeya walimtarajia afike jana Dar es Salaam, ameshindwa kufika kwaajili amebanwa na shughuli za kikazi hivyo wanaiarisha hadi Novemba 22 mwaka huu.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Novemba 2 mwaka 2012.  

No comments:

Powered by Blogger.