Header Ads

KESI YA MANJI Vs MENGI:KORTI YATUPA NYARAKA ZA MENGI

Na Happiness Katabazi


MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imevikataa vielelezo vya utetezi vilivyowasilishwa na Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Ltd, Reginald Mengi, katika kesi aliyofunguliwa na mfanyabiashara Yusuf Manji.

Uamuzi wa kuvikataa vielelezo hivyo vinavyojumuisha nyaraka 14 zikiwamo zinazoihusu kampuni ya Kagoda Agriculture Ltd ulitolewa mahakamani hapo jana na Hakimu Mkazi, Aloyce Katemana.

Katika kesi hiyo, Manji anamlalamikia Mengi kwa madai ya kumkashfu akimdai fidia ya shilingi moja kwa kumuita fisadi papa.

Hakimu Katemana alisema amefikia uamuzi huo baada ya kusikiliza hoja za kisheria zilizowasilishwa mbele yake na pande zote mbili kwa siku mbili tofauti.

Akisoma uamuzi wake huo, alisema anakubaliana na hoja za kisheria zilizowasilishwa awali na jopo la mawakili wa mlalamikaji ambao wanaongozwa na Mabere Marando, Richard Rweyongeza, Dk. Ringo Tenga na Beatus Malima kwamba mahakama hiyo itupilie mbali maombi ya mdaiwa (Mengi) ya kutaka nyaraka hizo zikiwemo nyaraka vivuli ambazo zinaonyesha ni mali ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na mkataba baina kampuni ya Kagoda Agriculture Ltd na Quality Finance Corporation Ltd.

“Kwa kauli moja mahakama hii inatupilia mbali ombi la mdaiwa (Mengi) kwa sababu nyaraka hizo anazotaka kuzitumia kutolea ushahidi hazihusiani na kesi hii kabisa, na pia nyaraka hizo ni vivuli.”

Baada ya Hakimu Katemana kumaliza kusoma uamuzi wake, Wakili wa mdaiwa Michael Ngaro anayesaidiwa na Deo Lingia aliinuka kwenye kiti alichokuwa ameketi na kuieleza mahakama kuwa uamuzi wa hakimu huyo haukuwa wa kushtukiza.

Wakili Ngaro alidai kuwa kitendo cha hakimu huyo kuzikataa nyaraka hizo ni wazi sasa kimesababisha mteja wake asizitumie nyaraka hizo kama ushahidi wakati siku atakapoitwa na mahakama hiyo kujitetea na kwamba wanaomba nakala ya uamuzi huo na ili kwenda kuupinga Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Hata hivyo hoja hiyo ya wakili Ngaro ya kutaka kwenda Mahakama Kuu kupinga uamuzi wa Mahakama ya Kisutu, ulipingwa vikali na mawakili wa mlalamikaji ambao walimwomba Ngaro asiipotezee muda mahakama hiyo kwani katika mabadiliko ya sheria yaliyofanywa na Bunge mwaka 2002 yanakataza kuyakatia rufaa maamuzi madogo (ruling) yanayotolewa na mahakama za chini kabla kesi ya msingi haijamalizika.

Hata hivyo hoja hiyo ya mawakili wa Manji, ilimfanya wakili wa Mengi kuwasilisha ombi jipya la kuiomba mahakama itumie busara zake kwani siku itakapofika mteja wake kuja kujitetea atakosa nyaraka.

Baada ya ombi hilo, Katemana aliahirisha shauri hilo hadi Februari 15 mwaka huu ambapo atatoa uamuzi.

Mapema asubuhi jana wakili wa Mengi, alianza kujibu hoja za mawakili wa mlalamikaji zilizowasilishwa mahakamani hapo Februali 4, mwaka huu, aliomba nyaraka za mteja wake zipokelewe na pingamizi la Manji kutaka nyaraka hizo zisipokelewe litupwe.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi,Februali 12 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.