Header Ads

KORTI KUU KUAMUA DHAMANA YA LIYUMBA JUNI 15

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imesema Juni 15 mwaka huu, itatoa uamuzi wake kuhusu rufaa ya Mkurugenzi Mashitaka(DPP),Eliezer Feleshi, dhidi ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi wa Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba, ya kupinga uamuzi wa kulegezewa masharti ya dhamana.


Jaji Geofrey Shaidi ambaye jana alisikiliza rufaa hiyo sambamba na kusikiliza hoja za upande wa DDP na mawakili wa mjibu rufaa ,na kwamba anairisha shauri hilo tarehe hiyo ambapo atakuja kutoa uamuzi kulingana na malumbano ya kisheria yaliyozuka wakati akisikiliza hoja hizo.

“Nimesikiliza kwa kina hoja zote hivyo naomba namimi mnipe muda hadi Juni 15 mwaka huu, saa tatu asubuhi,tukutane pale ukumbi namba moja katika mahakama hii,kwani siku hiyo ndiyo nitautumia kutolea uamuzi wa rufaa hii namba 44/2009” alisema Jaji Shaidi.

Awali jana asubuhi Wakili Mwandamizi wa Serikali Justus Mlokozi akiksaidiana na John Rwabuhanga alianza kwasema hakuliridhishwa na uamuzi huo ndiyo maana wameamua kukata rufaa kwasababu kuu mbili,mosi,wanaamini Mwaseba alikosea kutoa dhamana bila kuzingatia kifungu hicho,pili hakimu huyo alipotosha matakwa ya kifungu hicho.

Huku akionyesha kujiamini, Mulokozi alianza kwa kuichambua sababu ya pili,alidai kuwa shitaka linalomkabili mjibu rufaa ni kusababisha hasara na kwamujibu wa maelezo ya kosa yanaonyesha kuwa kakosa hayo aliyafanya akiwa ni mtumishi wa umma kwani alizidisha kiwango cha fedha cha ujenzi wa Minara Pacha”Twin Towers” bila idhini ya mwenye mali ambaye ni BoT.

“Mtukufu Jaji mradi wa ujenzi wa ujenzi wa Minara Pacha kiwango cha fedha kilichoanishwa rasmi lakini Liyumba akiwa mtumishi wa benki hiyo alikizidisha kiwango kingine cha fedha na kwa kitendo chake hicho mwenye mradi mali ambaye ni BoT aliingia hasara ambayo ni fedha halisi:

‘Hivyo basi katika misingi hiyo shitaka lililopo katika kesi ya msingi pale Kisutu hiki kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 ,kinatakiwa kitumike kikamilifu katika kuamua dhamana ya Liyumba na sivinginevyo.” alidai Mulokozi huku akionyesha kujiamini.

Mulokozi ambaye jana alilazimika kutumia kifungu cha 5 cha Sheria Kanuni ya Adhabu ili kutetea hoja yake, alidai kuwa kifungu hicho kinatoa tafsiri maana ya neno fedha ambapo alisema kwa mujibu wa kifungu hicho kinasema fedha maana yake warrants,funds,hundi ya benki,current notes or request of payment .

“Kwa tafsri hiyo haina maana neno fedha taslimu peke yake kama ilivyodaiwa na Mwaseba kwahiyo hakimu huyo tunaamini kabisa hakimu huyo alipotoka kusema shitaka la kusababisha hasara halihusiani na fedha taslimu” alidai Mulokozi.

Aidha alidai maana halisi ya kifungu cha 284(a)(6) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu,inatamka wazi endapo mahakama inampomtia hatiani mahakama inaanza kuchukua ile nusu ya mali iliyowekwa mahakama na mshitakiwa kama dhamana.

“Kwahiyo kifungu hicho cha 284(a)(6) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kwahiyo sisi tunasema kifungu hicho kinasaidia utekelezaji wa masharti yanayotamkwa katika kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai 2002.

“Kwa hiyo tunaomba Mahakama Kuu iingilie kati kutafsiri kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Makosa ya Jinai kisha itoe itengue uamuzi mahakama ya Kisutu kwasababu kifungu hicho ndicho kinapaswa kitumike kwenye dhamana ya mshitakiwa’ alidai Mulokozi.

Kwa upande wake mawakili wa utetezi Onesmo Michael na Majura Magafu waliendelea kusisitiza msimamo wao kuwa uamuzi wa kulegezwa kwa masharti ya dhamana uliotolewa na mahakama ya Kisutu ni sahii na kutaka rufaa ya DPP itupiliwe mbali.

Mei 28 mwaka huu,Mwaseba alitangaza kumwachia kwa dhamana ya sh milioni 300 badala ya sh bilioni 110 kama ilivyokuwa awali,wadhamini wawili watakaosaini bondi ya sh milioni 50 kila mmoja, zuio la kutoka nje ya Dar es Salaam hadi kwa kibali maalum na kusalimisha hati ya kusafiria mahakamani.

Masharti hayo ni tofauti na yale ya awali, alipotakiwa kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika, ambao wangesaini bondi au kuwasilisha hati yenye thamani ya nusu ya kiasi cha sh bilioni 221, anachotuhumiwa kuisababishia serikali hasara.

Sharti lingine la awali, lilikuwa ni kuacha hati za kusafiria mahakamani hapo, kuripoti katika ofisi za Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kila Ijumaa na zuio la kutoka nje ya Dar es Salaam bila ya kibali maalum cha mahakama.

Hata hivyo, uamuzi wa kulegezewa masharti ya dhamana, ulimfanya Liyumba apumue, hasa pale Hakimu Maseba aliposema amesikiliza hoja za pande zote mbili na kulazimika kukubaliana na hoja za mawakili wa utetezi kwamba, ni kweli kifungu hicho kamwe hakipaswi kutumika katika mashitaka mapya yanayomkabili mshitakiwa huyo.

Liyumba anakabiliwa na makosa mawili ya jinai katika kesi namba 105/2009 kwa matumuzi mabaya ya ofisi ya umma ambapo anadaiwa kuwa kati ya mwaka 2001-2006 akiwa mwajiriwa wa serikali, aliidhinisha ujenzi wa minara pacha, bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa Benki Kuu.

Aidha, anadawa kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 kwa uamuzi wake wa kuidhinisha ujenzi wa minara hiyo pacha kosa linaloangukia kwenye shitaka la kwanza.

Liyumba alisomewa mashitaka mapya baada ya Hakimu Mkazi Walirwande Lema, aliyekuwa akisikiliza kesi namba 27/2009 iliyokuwa ikimkabili mshitakiwa huyo na Meneja Miradi wa BoT, Deogratius Kweka, kuwaachia huru baada ya kubaini hati ya mashitaka ilikuwa ina makosa kisheria.

Hata hivyo, muda mfupi baadaye, walikamatwa tena na Liyumba kusomewa mashitaka mapya, huku Kweka akiendelea kuhojiwa na Takukuru.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi,Julai 11,2009

No comments:

Powered by Blogger.