Header Ads

MHASIBU WA OFISI YA MKEMIA MKUU WA SERIKLI KORTINI KWA WIZI


Na Happiness Katabazi
 
ALIYEKUWA  Muhasibu wa Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Godfrey Mbuilo jana amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, akikabiliwa na makosa ya wizi wa Sh.milioni 153.8 mali ya serikali.


Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tumaini Kweka alidai kuwa mshtakiwa anatuhumiwa kwa mashtaka manne ya wizi wa fedha akiwa mtumishi wa Umma.
Kweka alidai kuwa Agosti 2, 2011,  Mbuilo akiwa katika Ofisi za  wakala wa Mkemia Mkuu wa Serikali aliiba sh. milioni 40 zikiwa ni mali ya Serikali.

Hata hivyo alidai kuwa fedha hizo, ziliingia katika miliki yake akiwa mtumishi wa umma.Katika shtaka la pili mshtakiwa anatuhumiwa Septemba  5, 2011 akiwa katika ofisi hiyo hiyo aliiba sh. milioni 45 mali ya Serikali.

Shtaka la tatu anatuhumiwa, Oktoba 5, 2011 aliiba sh. milioni 40 mali ya Serikali, ambazo aliiba akiwa mtumishi wa umma.

Pia katika shtaka la nne Mbuilo anatuhumiwa  kati ya Januari 31 mwaka jana na Aprili 10 mwaka huo huo, akiwa katika ofisi hizo, aliiba Dola za Kimarekani 18,000, ambazo ni takribani sh. milioni 28.8 za Kitanzania.

Wakili huyo alidai kuwa jumla ya fedha anazotuhumiwa Mbuilo kuiba ni sh. milioni 153.8, baada ya kumsomea mashtaka hayo alikana kuhusika na makosa hayo.

Hata hivyo wakili huyo alidai upelelezi wa shauri hilo haujakamilika na wanaomba tarehe nyingine ili waendelee na upelelezi.

Wakili wa mshtakiwa Deinol Msemwa alidai kuwa mashtaka anayoshtakiwa mteja wake yanadhamana, pia mashtaka hayo hayaangukii katika kifungu namba 148 (5) cha Sheria ya  Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002.

Pia alidai hakuna sheria yoyote inayozuia dhamana, na mshtakiwa hajawahi kushtakiwa na kosa lolote wala hawakuwahi kuruka dhamana yoyote, kwa hiyo anaomba dhamana kwa mteja wake.

Kweka alidai sheria namba 148 (5) (e) cha CPA, kinaeleza wazi kuwa,mtu yoyote anayeshtakiwa kama kiasi cha fedha kinazidi sh. milioni 10, mshtakiwa atatakiwa atoe nusu ya fedha taslimu au hati mali isiyohamishika yenye thamani ya fedha hiyo.

Hata hivyo alidai nusu ya fedha ya Mbuilo ni sh. milioni 76.9, ambazo atatakiwa atoe au awasilishe hati ya mali isiyohamishika yenye thamani hiyo.

Mmbando alisema masharti ya dhama mshtakiwa anatakiwa awe na wadhamini wawili watakaosaini bondi ya sh. milioni  100 au hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya sh. milioni 76.9, na hati hiyo itatakiwa ikaguliwe kama kweli inafikia kiasi hicho.ili

Mbuilo amerudishwa rumande kwa kushindwa kutimiza masharti ya dhamana, kesi yake itatajwa Aprili 24 mwaka huu.

Chanzo:www.katabazihappy.blogspot.com ; Aprili 12 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.