Header Ads

WASHITAKIWA KESI YA GHOROFA WAPATA DHAMANA

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, jana imempatia dhamana mfanyabiashara Razah Hussein Razah na wenzake 10, wanaokabiliwa  na makosa 24 ya kuua bila kukusudia watu walioangukiwa na ghorofa katika mtaa wa Indira/ Gandi hivi karibuni.

Mbali na Razah washtakiwa wengine ni Godluck Mbaga, Wilbroad Mugabisyo, Ibrahim Kisoki, Mohamed Abubakar, Charles Salu, Zonazea Anage, Vedasto Ferand, Michael Hemed, Albert Jones na Joseph  Ringo wanaotetewa na wakili Adronicus Byamungu.

Mawakili waandamizi wa serikali, Bernad Kongora , Tumaini Kweka, Lasdiraus Komanya na Mahugo waliikumbusha mahakama hiyo kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwa ajili ya mahakama hiyo kutolea uamuzi wa ama ina mmlaka ya kutoa dhamana kwa kesi hiyo ya kuua bila kukusudia au la.

Hakimu Devota Kisoka alisema baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili ambapo mawakili wa utetezi siku ya kwanza ilipofunguliwa kesi hiyo Aprili 3, mwaka huu, waliomba washtakiwa hao wapewe dhamana.

Aliongeza kuwa mawakili hao wa utetezi walidai kuwa katika kesi ya jinai No.34/2008, Jaji Thomas Mihayo katika uamuzi wake alizitaka mahakama za chini zinazoendesha kesi zinazotakiwa kusikilizwa na mahakama kuu, zinapokuwa katika hatua za awali, zinatakiwa ziwapatie dhamana washtakiwa hao.

Alisema kuwa mawakili wa serikali, siku hiyo walipinga wakidai kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo ya kuua bila kukusudia na kwamba ni mahakama kuu pekee yenye mamlaka ya kusikiliza na kuitolea uamuzi.

“Nilizisikiliza hoja za pande zote mbili na mahakama hii imefikia uamuzi wa kukubaliana na hoja za mawakili wa utetezi kwamba mahakama hii inao uwezo wa kutoa dhamana katika kesi hiyo, kwani mahakama kuu ni mahakama ya rekodi na inapotoa mwongozo wake katika mahakama za chini, basi ni lazima mahakama za chini ziufuate,” alisema Kisoka.

Alifafanua kuwa ameisoma vizuri kesi hiyo Na 34/2008 ambayo Jaji Mihayo alitoa mwongozo huo kwa mahakama za chini akisema kuwa mahakama hiyo ni miongoni mwa zile za chini, hivyo imefikia uamuzi wa kuwapatia dhamana washtakiwa wote kwa masharti.

Kisoka alifafanua kuwa ili washtakiwa wapate dhamana ni lazima kila mmoja awe na mdhamini atakayesaini bondi ya sh milioni 20, kusalimisha hati ya kusafiria itakayohifadhiwa polisi, kutotoka nje ya mkoa au nchi bila kibali cha mahakama.
Hata hivyo wakili wa serikali Kongora aliomba mahakama kuwa wakati ikitoa dhamana izingatie masharti ya kifungu cha 148(6),(7) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai mwaka 2002 na kwamba upande wa jamhuri unaomba barua zinazowatambulisha wadhamini wapatiwe ili waweze kwenda kuzikagua.

Ombi hilo lilikubaliwa na hakimu Kisoka ambapo alipokea barua za wadhamini na maelezo hayo kisha akaiahirisha kesi hiyo hadi leo kwa ajili ya kutoa nafasi kwa upande wa jamhuri kwenda kujiridhisha.

Itakumbukwa kuwa Machi 29, mwaka huu, jengo la ghorofa 16 lililokuwa linajengwa katika mtaa wa Indira Ghandi lilianguka na kusababisha vifo vya watu 34 na wengine kadhaa kujeruhiwa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Aprili 17 mwaka 2013.


No comments:

Powered by Blogger.