Header Ads

VIGOGO WIZARA YA ARDHI KORTINI


Na Happiness Katabazi

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), jana ilimfikisha katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi, Simon Lazaro, kwa makosa ya matumizi mabaya ya madaraka na wizi sh milioni 100 mali ya serikali.

Mbali na Lazaro wakili wa TAKUKURU, Leonard Swai, mbele ya Hakimu Mkazi, Aloyce Katamana, aliwataja washtakiwa wengine kuwa ni Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Matumizi Bora ya Ardhi, Gerald Mango, na Kaimu Mhasibu Mkuu wa tume hiyo, Charles Kijumbe.

Wakili Swai alidai kuwa mshtakiwa wa kwanza, Lazaro peke yake anashtakiwa kwa kosa la kuwasilisha nyaraka za uongo kwa mwajiri wake na kwamba kosa hilo alilitenda  Mei 18 mwaka jana, katika wizara hiyo.

Alidai kuwa akiwa mwajiriwa wa wizara hiyo kwa cheo cha Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango, kwa makusudi aliwasilisha nyaraka hizo za uongo kwa mwajiri wake zinazoonyesha amepokea sh milioni 100 kutoka Tume ya Taifa ya Matumizi bora ya Ardhi kwa ajili ya kufanyia kazi ya upimaji wa ardhi katika wilaya za Babati, Kilolo na Bariadi wakati akifahamu nyaraka hizo ni za uongo.

Kosa la pili ni la matumizi mabaya ya madaraka kinyume na kifungu cha 31 cha Sheria ya TAKUKURU ya mwaka 2007, kwamba washtakiwa wote watatu kati ya Julai 4 na Agosti 5 mwaka 2011, wakiwa ni waajiriwa wa wizara hiyo  walitumia madaraka yao vibaya kinyume cha kanuni ya 87(1) na 86(1) ya kanuni ya fedha za umma ya mwaka 2004.

Wakili Swai alidai shtaka la tatu linalomkabili Lazaro peke yake ni ufujaji na ubadhirifu wa fedha za umma ambalo ni kinyume na kifungu cha 28(1) cha Sheria ya TAKUKURU mwaka 2007, ambalo alilitenda kati ya Julai 4 na Agosti 5 mwaka 2011.

Aliongeza kuwa alitumia fedha za umma sh milioni 100 alizozipokea toka Tume ya Taifa ya Matumizi bora ya Ardhi kwa manufaa yake binafsi wakati fedha hizo zilitolewa na wizara kwa ajili ya kupimia ardhi katika  maeneo ya Arusha, Muleba, Ngorongoro, Songea, Kilosa na Mpanda.

Alilitaja shtaka la nne kuwa ni mbadala wa kosa la tatu linalomkabili Lazaro, kuwa ni la wizi kinyume cha kifungu cha 258 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002.

Swai alidai mshtakiwa alitenda kosa hilo kati ya Julai 4 na Agosti 5 mwaka 2011 akiwa ni Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa wizara hiyo ambapo aliiba sh milioni 100 zilitolewa na tume kwa wizara kwa ajili ya upimaji ardhi katika maeneo tajwa.

Washtakiwa hao walikana mashtaka hayo na wakili Swai alidai upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na kwamba anaiomba mahakama ipange tarehe ya kuja kuwasomea maelezo ya awali washtakiwa.

Hakimu Katemana alisema kuwa makosa yanayowakabili washtakiwa yana dhamana na kwamba Lazaro peke yake anatakiwa awe na wadhamini wawili wa kuaminika ambao watasaini bondi ya sh milioni 50 na barua za utambulisho wa ofisi zinazotambulika.

Mshtakiwa wa pili na wa tatu walitakiwa wawe na wadhamini wa kuaminika ambao watasaini bondi ya sh milioni 25. Na washtakiwa wote walitimiza masharti na wakapewa dhamana huku kesi hiyo ikiahirishwa hadi Aprili 30.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Aprili 17 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.