Header Ads

KIBANDA ANA KESI YA KUJIBU







Na Happiness Katabazi
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imemuona aliyekuwa Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Tanzania Daima,Absalom Kibanda na wenzake wanaokabiliwa na kesi ya kuandika na kuchapisha makala ya uchochezi wana kesi ya kujibu.

Uamuzi huo ulitolewa jana na Hakimu Mkazi Waliarwande Lema jana muda mfupi baada ya wakili wa serikali Beatha Kitau kuambia mahakama kuwa upande wa jamhuri umeifunga kesi yake na kwamba mashahidi watatu waliowaleta kujenga kesi hiyo wanatosha.

Hakimu Lema alisema alisikiliza ushahidi mashahidi wa upande wa jamhuri amefikia uamuzi wa kuwaona washitakiwa wote wanakesi ya kujibu na hivyo haoni haja ya kutoa nafasi kwa mawakili wa jamhuri na utetezi kupewa mwenendo wa kesi hiyo ili waeende kuandaa majumuisho ya kuwaona washitakiwa hao wanakesi ya kujibu au la.

Hata hivyo wakili wa Kibanda, Isaya Matambo aliomba mahakama impatie mwenendo wa kesi hiyo ili aweze kuupitia na kwenda kujiandaa na kisha awasilishe maombi ya kuiomba mahakama imuone Kibanda hana kesi ya kujibu, lakini hakimu huyo alitupilia mbali ombi hilo na kusema kuwa yeye ndiye ameisikiliza kesi hiyo mwanzo hadi hapo ilipofikia jana na ameona washitakiwa wana kesi ya kujibu na haoni sababu ya kutoa nafasi ya mawakili kwenda kuandaa maombi ya kuwaona wateja wao wana kesi ya kujibu na akaiarisha kesi hiyo hadi Septemba 3 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya washitakiwa kuanza kujitetea.

Mbali na Kibanda washitakiwa wegine ni Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Tanzania Daima, Naibu Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya Mwananchi Communication Ltd, Theophil Makunga, na mchangiaji wa makala kwenye gazeti la Tanzania Daima, Samson Mwigamba.

Desemba mwaka 2011 ilidaiwa mahakamani hapo kuwa Kibanda na Mwigamba wanakabiliwa na kosa la uchochezi kinyume na kifungu cha 32(1)(c) na 31(1)(a) cha Sheria ya Magazeti Sura ya 229 ya mwaka 2002.

Shtaka la pili ni kuchapisha waraka wa uchochezi kinyume na kifungu cha 32(1) ( c) na 31 (1)(a) vya Sheria ya Magazeti namba 229 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 linalomkabili Makunga.
Novemba 30 mwaka 2011 gazeti la Tanzania Daima toleo namba 2552 lilichapisha makala inayodaiwa kuwa ya uchochezi yenye kichwa cha habari ‘Waraka Maalum kwa Askari Wote’.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Agosti 15 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.