Header Ads

TRAFIKI 'FEKI' ATINGA KORTINI




Na Happiness Katabazi

HATIMAYE Trafiki ‘feki’ James Hassan (45) Mkazi wa Kimara  jana alifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala Dar es Salaam,  akikabiliwa na makosa mawili  likiweko kosa la kujifanya  askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani.

Wakili wa Serikali Nassor Katuga mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi,Joyce Minde,alidai kuwa Agosti 14, mwaka huu, eneo la Kinyerezi  katika eneo la mnara wa Voda, mshitakiwa kwa njia ya udanganyifu alijitambulisha kwa Inspekta wa Polisi, Gabriel Chiguma, kuwa ni askari  wa kikosi cha usalama barabarani.

Wakili Katuga alidai siku hiyo kwa njia ya udanganyifu mshitakiwa huyo alikutwa akiwa na sare za Jeshi la polisi ambazo ni kofia, jaketi na mkanda wa kiunoni.
Hata hivyo, mshitakiwa huyo alikana mashitaka, ambapo Katuga alidai upelelezi haujakamilika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa.

Mshitakiwa huyo aliomba apewe dhamana, ambapo Hakimu Joyce alitaja masharti ya dhamana ambayo ni kuwa na wadhamini wawili wenye makazi ya kudumu watakaotia saini dhamana y ash. Milioni saba.

Hata hivyo mshitakiwa huyo  alishindwa kutimiza masharti hayo ya dhamana na hakimu Minde akaamuru  apelekwe gerezani hadi Septemba 5 mwaka huu,  kesi hiyo itakapokuja kwaajili ya kutajwa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Agosti 23 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.