Header Ads

NTAGAZWA ALIPONDA JESHI LA POLISI







Na Happiness Katabazi

WAZIRI wa zamani Arcado Ntagazwa ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, analishangaa Jeshi la Polisi na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka nchini kujitwishwa jukumu lisilolao la kuamua kumfungulia kesi ya jinai inayomkabili wakati  kisheria kesi hiyo ilipaswa iwe ni ya madai.

Ntagazwa ambaye hivi sasa ni Kada wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na ni msomi wa taaluma ya sheria alieleza hilo jana mbele ya Hakimu Mkazi Gene Dudu wakati akitoa utetezi wake katika kesi ya kujipaia kofia ,fulana zenye jumla ya thamani ya Sh.milioni 74.9 kwa njia ya udanganyifu.

Ntagazwa ambaye anatetewa na wakili wa kujitegemea Alex Mshumbusi alitoa maelezo hayo wakati akipangua maswali aliyokuwa akihojiwa na wakili wa serikali Charles Anindo  ambapo alidai kuwa kesi hiyo ilipaswa iwe nay a madai na aliyekuwa  na haki ya kuifungua ni mkwe wa Edward Lowassa, Noel Severe ambaye ni mkurugenzi wa kampuni ya Visual Storm na siyo Polisi ,DPP kwani Polisi ,DPP wanajukumu la kufungua kesi ya jinai tu na siyo kesi za madai.

Akiongozwa na wakili Mshumbushi kutoa utetezi wake, Ntagazwa alieleza kuwa  yeye ni miongozi wa wadhamini wa Asasi isiyo ya kiserikali ya FORD na kwamba  mwaka 2010 taasisi hiyo ilikuwa inataka kumuenzi Baba wa Taifa Julias Nyerere ambaye Oktoba 14 mwaka 2010 alikuwa anatimiza miaka 10 tangu afariki dunia na kwamba FORD ilikuwa imeandaa mradi ukiwemo wa kutengeneza fulana, kofia zilizokuwa zinapinga vitendo vya kifisadi kwaajili ya kumuenzi Nyerere na kwamba FORD kwakuwa haikuwa haina fedha, iliamua kuandika mradi na kuupeleka kwa wafadhili mbalimbali ili ziweze kuwapatia fedha za kuweza kufanikisha mradi huo  uliokuwa umebeba dhima ya kumuenzi Nyerere kwa kupinga ufisadi.

“Baada ya kupeleka maombi yetu hayo kwa wafadhili, wafadhili walikubali ombi letu na wakatuambia tuendelee na taratibu nyingine na kwamba watatupatia fedha…na sisi FORD kwa kuanzia tulienda kuona na kampuni ya Visual Storm ambayo mmoja wa wakurugenzi wake ni Mkwe wa Lowassa , Severe na kumwomba atutengenezee fulana na kofia  zenye thamani ya Sh.milioni 74.9  na tulimweleza mapema kuwa wafadhili wakitupatia fedha tutamlipa na Severe alitukubalia akatutengenezea hizo fulana na FORD na Visual Storm haikuwa imeandikishia mkataba wa maandishi kwaajili ya kazi hiyo;

“Lakini ilipofika  Januari 23 mwaka 2010 gazeti la Mtanzania lilichapisha habari iliyokuwa na kichwa cha habari kisemacho ‘ Vigogo walioisaliti CCM wahanikwa’. Na ndani ya habari hiyo zilipigwa picha fulana zetu ambazo zilitengenezwa na Visual Storm na hiyo habari kumbe ilisomwa vizuri na wale wafadhili waliokuwa wametuahidi kutupatia fedha, wale wafadhili wakashtushwa na habari ile wakatuita viongozi wa FORD na kueleza kuwa hawatawafadhili tena fedha kama walivyowaadi kwasababu kutokana na habari hiyo wameona kumbe FORD siyo asasi ya kirai ni chama cha siasa cha upinzani” alidai Ntagazwa.

Ntagazwa ambaye alikuwa akitumia lugha ya Kiingereza  na kisheria kujitetea alieleza kuwa baada ya wafadhili wale kujitoa, FORD wakaamua kwenda polisi kutoa taarifa kuhusu habari hiyo iliyochapishwa na gazeti la Mtanzania lakini baada ya muda mfupi baadaye alishangaa polisi wanakuja kumkamata nyumbani kwake akiwa bafuni na hadi leo polisi hawajawai kumchukua maelezo ya onyo  na jeshi la polisi na akashtukia anafunguliwa kesi hiyo ambayo alilisitiza ni kesi ya madai siyo ya jinai na polisi imekuwa ni jadi yao sasa kudandia mambo hata yasiyowahusu mke na mume wanadaiana polisi wanaingilia kati.

“Kwanza nikuulize wewe wakili wa serikali Charles hivi hata kama kweli kesi hii ilikuwa inatakiwa iwe ya jinai ,minikifungwa jela ndiyo huyo Severe atazipata hizo fedha?,Umesikia wewe kijana nenda kamwambie huyo Severe kuwa  polisi wamemdanga sana kwa kumshauri anifungulie kesi ya jinai….narudia tena hata nikifungwa ndiyo hizo hela atalipwa na polisi? Hizo fulana hadi leo zipo nyumbani kwa mjumbe wa wadhamini wa FORD ,Wakili Steven Thonya  ambaye naye ni wakili na atakuja kutoa ushahidi wake na hata leo hii mahakama ikitaka kuthibitisha hilo iamie nyumbani kwa Thonya na itazikuta hizo fulana” alidai Ntagazwa na kusababisha watu kuangua vicheko.

Baada ya Ntagazwa kumaliza kutoa utetezi wake hakimu Dudu aliarisha kesi hiyo hadi Septemba  17 mwaka huu, itakapokuja kwaajili mshitakiwa wa tatu ambaye ni mtoto wa Ntagazwa, Dk. Webhale Ntagazwa na mshitakiwa wa kwanza Senetor Mirelya (60) alishamaliza kutoa utetezi wake.

Aprili 23 mwaka 2012, ilidaiwa mahakamani hapo na Wakili wa Serikali Ladslaus Komanya  kuwa Oktoba 22 mwaka 2009 huko Msasani Mikoroshini washtakiwa hao kwania ovu walijipatia fulana 5000 na kofia 5000 zenye jumla ya thamani ya Shilingi milioni 74.9 toka kwa Noel Sevele kwa makubaliano kuwa wangemlipa Sevele kiasi hicho cha fedha katika kipindi cha mwezi mmoja tangu walipochukua vifaa hivyo lakini hata hivyo walishindwa kumlipa na washtakiwa walikana shtaka na kwamba upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika. 

Ntagazwa ambaye kwa sasa ni Kada wa Chadema , kabla ya kujiunga na chama hicho miaka minne iliyopita, akitokea chama cha Mapinduzi (CCM).Akiwa mwanachama wa CCM, aliwahi kuteuliwa na rais wa Serikali ya awamu ya pili na ya tatu, Ally Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa kushika nyadhifa za uwaziri katika wizara mbalimbali hadi ilipofika mwanzoni mwa mwaka 2006, Rais Jakaya Kikwete alipounda baraza lake jipya la mawaziri na kuamuacha nje ya baraza hilo. 

Ntagazwa ambaye aliwahi kuwa mbunge wa muda mrefu wa Jimbo la Mhambwe kwa tiketi ya CCM, hadi sasa nakumbukwa kwa msemo wake mmoja maarufu aliowahi kuutoa bungeni akiwa Waziri Nchi ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Mazingira alisema ‘Ipo siku wajukuu zetu watafukua makaburi yetu wachunguze ubongo wetu kama tulikuwa na akili timamu’. Ntagazwa alitoa msemo huo kutokana na kutoridhishwa na baadhi ya maamuzi yaliyokuwa yakifanywa na baadhi ya watendaji waliopewa dhamana.
  
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Agosti 28 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.