Header Ads

PINDA ABURUZWA MAHAKAMANI




Na Happiness Katabazi

HATIMAYE  Kituo cha Sheria na Utetezi wa Haki za Binadamu(LHRC) na Chama Cha  Wanasheria Tanganyika(TLS), jana vilifungua kesi ya Kikatiba katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, vikiomba mahakama hiyo itoe tafsiri za kisheria katika baadhi ya Ibara.

Kesi hiyo ya Kikatiba ambayo imepewa namba 24 ya mwaka huu,na ambayo bado haijapangiwa jaji  ambapo wadaiwa ni  Waziri Mkuu Mizengo Pinda na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Taasisi hizo ambazo zinatetewa na mawakili wa kujitegemea Haroud Sungusia , Francis Stolla na wengine 17, na kwa mujibu wa hati yao ya madai ambayo gazeti hili inayo nakala yake , walalamikaji hao wamewasilisha jumla ya maombi mawili ambao wanaomba mahakama itoe tafsiri ya kisheria katika Ibara hizo na kwamba wamewasilisha kesi hiyo ya Kikatiba chini ya sehemu ya Tatu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  ya mwaka 1977, ambayo inaainisha  Haki na Wajibu Muhimu.

Wakili Sungusia alilitaja ombi la kwanza kuwa ni wanaiomba mahakama hiyo itamke kuwa ibara ya 100(1) ya Katiba ya nchi inayotoa    uhuru wa majadiliano kwa wabunge wawapo ndani ya bunge ambayo inasomeka hivi :  “kutakuwa na uhuru wa mawazo, majadiliano na
utaratibu katika Bunge na uhuru huo hautavunj
wa wala kuhojiwa na chombo chochote katika Jamhuri ya Muungano, au katikaMahakama au mahali penginepo nje ya Bunge”.

Wakili Sungusia anadai kuwa Ibara hiyo ina ubaguzi ndani yake kwani inayoa uhuru kwa mbunge kujadili ndani ya bunge na wakati anajadili jambo hata kama amevunja haki za mtu mwingine hataweza kushitakiwa wala kuhojiwa jambo ambalo anadai linakinzana na Ibara ya 13(2) ya Katiba ambapo Ibara hii inasomeka hivi; “ Ni marufuku kwa sheria yoyote iliyotungwa na mamlaka
yoyote katika Jamhuri ya Muungano kuweka sharti lolote ambalo
ni la ubaguzi ama wa dhahiri au kwa taathira yake’.

‘Hivyo sisi tunaomba mahakama hiyo itamke wazi kuwa Ibara ya 100(1) inakwenda kinyume na matakwa ya Ibara 13(2), zina kinzana kwani Ibara hiyo ya Ibara hiyo ya 100(1) ya Katiba inatoa haki tu kwa upande wa mmoja wa  wabunge uhuru wao kutohojiwa na inawanyima haki ya kuwahoji au kuwashitakiwa wabunge wanaotoa kauli zao bungeni hata kama kauli hizo za wabunge zimevunja haki za wanchi , hivyo tunaomba mahakama itamke kuwa ibara hiyo ya 100(1) ya Katiba inakinazana na ibara hiyo”alidai wakili Sungusia.

Wakili Sungusia alilitaja dai la pili kuwa ni kuiomba mahakama hiyo itamke kuwa kauli ya Pinda ambayo ililitaka Jeshi la Polisi kuwapiga wale wote wanaokiuka amri za jeshi hilo, kama kauli hiyo nayo inalindwa na kinga iliyowekwa katika Ibara ya Ibara ya 100(2) ya Katiba ya nchi ambayo inasomeka hivi ; ‘Bila  ya kuathiri Katiba hii au masharti ya sheria nyingine yoyote inayohusika, Mbunge yeyote hatashtakiwa au kufunguliwa shauri
la madai mahakamani kutokana na jambo lolote alilolisema
au kulifanya  ndani ya Bunge au alilolileta Bungeni kwa njia ya maombi, muswada, hoja au vinginevyo’..



Itakumbukwa kuwa Juni 19 mwaka huu, wakati wa Kipindi cha Maswali ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu bungeni, Waziri Mkuu Pinda akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Kilwa Kaskazini (CCM), Murtaza Mangungu aliyeuliza: “Serikali ipo tayari kiasi gani kubainisha na kuchukua hatua stahiki, badala ya kusakama makundi fulani, tujue chanzo halisi cha vurugu hizi na matatizo haya na jinsi gani vyombo vya dola vinavyoshughulikia kwa sababu yapo malalamiko katika baadhi ya maeneo kama Mtwara kwamba wananchi wanapigwa na vyombo vya dola?”
 
Waziri Mkuu alijibu: “Ni lilelile nililosema... mwishowe unaona anasema vyombo vya dola vinapiga watu. Ukifanya fujo, umeambiwa usifanye hiki, ukaamua kukaidi, utapigwa tu... hamna namna nyingine, maana wote tukubaliane kwamba nchi hii tunaiendesha kwa misingi ya kisheria.
“Sasa kama wewe umekaidi, hutaki unaona kwamba ni imara zaidi... wewe ndiyo jeuri zaidi watakupiga tu.... Mimi nasema muwapige tu, kwa sababu hakuna namna nyingine... maana tumechoka.

Chanzo;Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Agosti 2 mwaka 2013.




No comments:

Powered by Blogger.